BOA YATOA MIKOPO NAFUU KWA SEKTA YA AFYA



Benki ya BOA Tanzania imeanza kutoa mikopo ya riba nafuu kwa sekta ya afya, ili kuwezesha zahanati, vituo vya afya na hospitali kutoa huduma bora kwa wananchi.
Meneja Mwandamizi wa Masoko wa benki hiyo,   Solomoni Haule, aliwaambia waandishi wa habari mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam kuwa, mikopo hiyo itawezesha sekta hiyo kutoa huduma bora kwa jamii.
“Benki imeanza kutoa mikopo kwa sekta ya afya, ili kuwezesha sekta hiyo muhimu kutoa huduma bora na  kuleta maendeleo,” alisema. 
Alisema huduma hiyo ya mikopo inayoitwa Tiba Finance, iliyoanza kutolewa Aprili mwaka huu, ni ya riba nafuu na inatolewa kwa  muda mfupi na muda mrefu unaokwenda hadi miaka minne. 
Alisema benki inaamini kuwa changamoto kubwa zinazokabili sekta hiyo kama vitendea kazi, mashine za kisasa, kujenga na kukarabati majengo, na dawa za kutosha, vinaweza kupungua na kuisha kabisa kutokana na huduma za mikopo hiyo.
“Kupitia mikopo hii, tunaamini watamaliza au kupunguza kwa kiasi kikubwa changamoto hizi,” alisema.
Alisema katika kufanikisha azma hiyo, benki inashirikiana na asasi ya Medical Credit Fund, kujengea uwezo taasisi hizo, ili zitoe huduma bora.
“Tumejipanga kwa kushirikiana na asasi hii kwenda katika kila taasisi itakayokopa kutoa elimu. Tutafundisha namna ya kutumia vifaa vya kisasa vya kitabibu, mazingira ya kazi, utendaji na kutengeneza mipango ya mahesabu ya kibiashara,” alisema.
Alisema benki hiyo yenye  matawi katika mikoa ya Dar es Salaam (10) na matawi mengine Arusha, Kilimanjaro, Morogoro, Mtibwa, Mbeya, Tunduma, Mwanza, Kahama na sasa Mtwara,  ilishawapatia semina wafanyakazi wake kutoa mikopo kwa sekta hiyo ya afya. 

No comments: