Baraza la Wawakilishi lililazimika jana
kuahirisha kwa muda kikao chake, baada
ya wajumbe wengi kuchelewa na hivyo kuwepo idadi ndogo ya watu 17.
Naibu Spika wa Baraza la Wawakilishi, Ali
Abdalla Ali aliwataka wajumbe wa Baraza la Wawakilishi, kutimiza majukumu yao,
ikiwemo kuhudhuria bila ya kuchelewa katika vikao vya baraza hilo.
“Waheshimiwa wajumbe wa Baraza la Wawakilishi
nawakumbusheni majukumu yenu ikiwemo kuhudhuria vikao vya Baraza la Wawakilishi
kwa wakati ili kutekeleza majukumu yetu kwa mujibu wa katiba ya kuwahudumia
wananchi,” alisema.
Naibu Spika alilazimika kuahirisha kikao
asubuhi na kusubiri wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kwa muda wa dakika tano
hadi walipotimia idadi ya wajumbe 40, ambayo ndiyo inayokubalika kwa ajili ya
kuanza vikao vya baraza.
Akizungumza na mwandishi, Katibu wa Baraza la
Wawakilishi, Yahya Khamis Hamadi alisema kukosekana kwa kanuni zinazotoa adhabu
kwa wajumbe katika suala la kuchelewa kwa vikao ni moja ya kasoro kubwa katika
kuendesha vikao vya Baraza la Wawakilishi.
“Hayo ni mazoea kwa wajumbe kwa sababu hakuna
kanuni zinazowabana na kutoa adhabu kwa wajumbe wa Baraza la Wawakilishi
kukabiliana na tatizo la kuchelewa kuhudhuria vikao hivyo...ndiyo maana tatizo
la kuchelewa lipo mara kwa mara,” alisema.
Mmoja ya wajumbe wa Baraza la Wawakilishi,
alisema wajumbe wengi kutoka CUF wapo kisiwani Pemba, wakishiriki katika
chaguzi mbali mbali zinazofanyika katika ngazi ya chama hicho.
No comments:
Post a Comment