HOTUBA YA WAZIRI WA HABARI, VIJANA, UTAMADUNI NA
MICHEZO, MHE. DKT. FENELLA E. MUKANGARA
(MB), AKIWASILISHA BUNGENI MAKADIRIO
YA MAPATO
NA MATUMIZI YA FEDHA KWA MWAKA 2014/2015
A.
UTANGULIZI
1.
Mheshimiwa Spika, kufuatia taarifa iliyowasilishwa leo kwenye Bunge lako Tukufu na
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii sasa naomba kutoa
hoja ya kwamba Bunge lako Tukufu lipokee, lijadili na kupitisha Makadirio ya
Mapato na Matumizi ya Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo na Asasi
zake kwa mwaka wa fedha wa 2014/2015.
2.
Mheshimiwa Spika, awali ya yote napenda kutumia fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa
kunilinda na kunipa nguvu ya kutekeleza majukumu yangu na kuniwezesha kusimama
mbele ya Bunge lako Tukufu kuwasilisha bajeti hii.
3.
Mheshimiwa Spika, kwa heshima na taadhima nitumie fursa hii kuwapongeza Dkt. Jakaya Mrisho
Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais
wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, kwa uongozi wao thabiti ambao
umeendelea kudumisha amani na mshikamano wa Taifa letu. Tunajivunia pia matunda
ya Waasisi wa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ambao mwaka 2014 umetimiza
miaka 50. Uongozi wao umetuwezesha kufikia maendeleo ya kiuchumi, kijamii na
kisiasa tuliyonayo hivi sasa.
4.
Mheshimiwa Spika, napenda kutumia fursa hii kuwapongeza Makamu wa Rais, Mhe. Dkt. Mohamed Gharib
Bilal na Waziri Mkuu, Mhe. Mizengo Peter Pinda (Mb.), kwa kazi nzuri
wanazozifanya za ujenzi wa nchi yetu. Aidha, nikushukuru wewe binafsi Mhe.
Spika, Mhe. Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge wote kwa ushirikiano mnaonipa ambao
unaniwezesha kutekeleza kikamilifu majukumu niliyokabidhiwa ya kulitumikia
Taifa letu.
5.
Mheshimiwa Spika, katika maandalizi ya hotuba
hii, Wizara imezingatia maudhui yaliyotolewa katika Bunge lako Tukufu kupitia
Hotuba ya Mhe. Mizengo Peter Pinda
(Mb.), Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Aidha, hotuba yangu imezingatia
pia maelekezo na malengo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2014/2015.
6.
Mheshimiwa Spika, kutokana na mabadiliko ya uongozi yaliyotokea, natumia fursa hii
kuwapongeza Mawaziri na Naibu Mawaziri wote walioteuliwa kuongoza Wizara
mbalimbali.
7.
Mheshimiwa Spika, nawapongeza Waheshimiwa Wabunge wa Bunge Maalumu la Katiba kwa kazi kubwa
wanayoifanya ya kujadili, kuchambua na kuboresha Rasimu ya Katiba ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania. Ni matumaini yangu kuwa baada ya kukamilika wananchi
watapata fursa ya kupiga kura za maoni kama ilivyopangwa ili Taifa letu liweze
kupata Katiba Mpya iliyo bora.
8. Mheshimiwa Spika, kipekee napenda
kuwapongeza wajumbe wote wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii kwa
kazi nzuri wanayoifanya ya kuishauri Wizara katika maeneo mbalimbali. Wizara
itaendelea kuzingatia na kutekeleza ushauri unaotolewa. Shukrani na pongezi
zangu ziende kwa viongozi wapya waliochaguliwa kuongoza Kamati hii yaani, Mwenyekiti
wa Kamati, Mhe. Saidi Mtanda (Mb.) na Makamu Mwenyekiti, Mhe. John Damiano
Komba (Mb.). Nawapongeza pia wajumbe walioteuliwa kuunda Kamati hii. Ushauri
wao ndio umefanikisha maandalizi ya hotuba hii.
9. Mheshimiwa Spika, napenda kumshukuru aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya
Bunge ya Maendeleo ya Jamii, Mhe. Jenista Joachim Mhagama (Mb.), kwa kazi nzuri
aliyoifanya katika Kamati hii.
10. Mheshimiwa Spika, napenda kutoa pongezi kwa Wabunge wapya waliochaguliwa hivi karibuni kwa
ushindi wa kishindo ambao ni Mhe. Yusuf Salim Hussein, (Mbunge wa Chambani), Godfrey
William Mgimwa, (Mbunge wa Jimbo la Kalenga) na
Mhe. Ridhiwani Jakaya Kikwete, (Mbunge wa Jimbo la Chalinze).
11. Mheshimiwa Spika, nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitawapongeza wanahabari pamoja na wadau
wote wa sekta ya habari kwa kazi nzuri ya kutoa habari na kuchangia kwa kiasi
kikubwa katika kuuelimisha umma wa Watanzania. Aidha, napenda kutambua mchango
mkubwa wa vijana wote katika kuinua
uchumi kwa kuwa wao ni takriban asilimia 70 ya nguvu kazi ya Taifa letu.
Vilevile, niwapongeze wanamichezo wote ambao wameshiriki katika kuliletea
heshima taifa kupitia mashindano ya michezo mbalimbali ndani na nje ya nchi. Kwa
namna ya pekee nachukua fursa hii, kutoa pongezi za dhati kwa Timu ya Mpira wa
Miguu ya Watoto wanaoishi katika mazingira magumu kutoka Mkoa wa Mwanza iliyotwaa Kombe la Dunia la
Watoto wa Mitaani nchini Brazili. Hali kadhalika
nawapongeza kwa dhati kabisa wasanii wote ambao wamekuwa kioo cha jamii katika
kulitangaza taifa letu ndani na nje ya nchi yetu. Nawapongeza hasa kwa jinsi walivyoshiriki kikamilifu katika
kuhamasisha jamii kushiriki katika Maadhimisho ya Miaka 50 ya Muungano wa
Tanzania.
12. Mheshimiwa Spika, naomba kutumia nafasi hii kuungana na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kutoa
pole kwa familia na wananchi wa Jimbo la Kalenga na Jimbo la Chalinze kwa
kuondokewa na Wabunge wao, Marehemu William Augustao Mgimwa aliyekuwa Waziri wa
Fedha, ambaye alifariki tarehe 01
Januari 2014 nchini Afrika Kusini na Marehemu Said Ramadhani Bwanamdogo
aliyefariki tarehe 22 Januari 2014. Aidha, ninawapa pole Watanzania wote
waliopoteza ndugu zao kutokana na ajali, majanga na maradhi mbalimbali. Tunamwomba
Mwenyezi Mungu aziweke roho za marehemu mahali pema peponi, Amina!
13. Mheshimiwa Spika, hotuba yangu imegawanyika katika maeneo makuu matano kama ifuatavyo: eneo
la kwanza ni Utangulizi, eneo la pili ni Majukumu ya Wizara, eneo la tatu linahusu Mapitio ya Utekelezaji
wa Mpango na Bajeti kwa mwaka 2013/2014, eneo la nne linahusu Mpango na Bajeti kwa
mwaka 2014/2015 na eneo la tano ni Hitimisho.
B. MAJUKUMU YA WIZARA
14.
Mheshimiwa Spika, Wizara inatekeleza majukumu ya msingi yafuatayo:-
i) Kuandaa na kusimamia utekelezaji wa Sera za Sekta za Habari, Vijana,
Utamaduni na Michezo;
ii) Kuratibu na kusimamia masuala ya maendeleo ya vijana ili kuwawezesha
kujiajiri, kuajirika na kujitegemea;
iii) Kuwa Msemaji Mkuu wa Serikali
na kusimamia vyombo vya habari nchini;
iv) Kuratibu na kusimamia maendeleo ya utamaduni nchini;
v) Kuratibu na kusimamia maendeleo ya michezo nchini;
vi) Kusimamia utendaji kazi wa Asasi, miradi na programu zilizo chini ya Wizara
na
vii) Kuendeleza, kuwezesha na kuratibu masuala ya kuwajengea uwezo watumishi wa
Wizara.
C. MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA MPANGO NA BAJETI KWA MWAKA WA FEDHA 2013/2014
Mapato
na Matumizi
15.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2013/2014, Wizara
ilipanga kukusanya mapato ya jumla ya Shilingi
882,203,000 kutoka vyanzo mbalimbali. Hadi kufikia mwezi Aprili, 2014
jumla ya Shilingi 663,029,569 zilikusanywa ambazo ni
sawa na asilimia 75 ya lengo la makusanyo kwa mwaka. Mchanganuo wa makusanyo upo kwenye Kiambatisho Na. I.
16.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/2014, Wizara ilitengewa jumla ya Shilingi 17,628,045,000
kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida. Fedha hizo zilijumuisha Mishahara shilingi 9,257,125,000 (Wizara ni Shilingi 2,617,598,000 na
Asasi ni Shilingi 6,639,527,000). Matumizi Mengineyo (OC) shilingi 8,370,920,000
(Wizara ni Shilingi 4,941,920,000 na Asasi ni Shilingi
3,429,000,000). Hadi
mwezi Aprili, 2014 jumla ya Shilingi 13,292,539,498 za
Matumizi ya Kawaida zilipokelewa na kutumika ambapo kati ya fedha hizo Matumizi
Mengineyo ni Shilingi 4,740,957,000
na Mishahara ni Shilingi 8,551,582,498.
Miradi ya Maendeleo
17.
Mheshimiwa Spika,
katika kipindi cha mwaka wa fedha 2013/2014, Wizara ilitengewa jumla ya Shilingi
12,700,000,000 kwa ajili ya kutekeleza Miradi ya
Maendeleo. Hadi kufikia mwezi Aprili, 2014 jumla ya Shilingi 4,327,500,000 zilipokelewa ambazo ni sawa na asilimia 34 na Shilingi 2,310,021,000 zilitumika. Miradi iliyotekelezwa ni pamoja na Upanuzi wa Usikivu wa
Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), Ujenzi wa Ofisi - BAKITA, Programu ya
Urithi wa Ukombozi wa Bara la Afrika na Mfuko wa Maendeleo ya Vijana.
SEKTA YA HABARI
18.
Mheshimiwa
Spika,
katika
mwaka 2013/2014, Wizara imeendelea na utendaji wa kazi zake huku ikikabiliana na changamoto mbalimbali. Miongoni mwa changamoto hizo ni
baadhi ya vyombo vya habari kukiuka sheria kwa kuandika na kutangaza habari ambazo hazizingatii kanuni
na maadili ya taaluma ya uandishi wa habari. Aidha, kuongezeka kwa mifumo na
njia za mawasiliano kama mitandao ya kijamii kwenye “internet” kumeathiri
maudhui ya habari zinazotolewa.
19.
Mheshimiwa Spika, pamoja na changamoto hizo, Wizara imechukua hatua mbalimbali za
kukabiliana nazo, zikiwemo kutoa onyo na kufungia baadhi ya vyombo vya habari
vilivyokiuka maadili. Wizara pia imeelekeza Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania
(TCRA) kutekeleza kikamilifu mpango wa kusajili wamiliki wote wa mitandao hiyo.
Vilevile, Wizara inaendelea kutoa elimu na kuwaelekeza wamiliki na wahariri wa
vyombo vya habari kufuata sheria, kanuni na miongozo iliyowekwa.
20.
Mheshimiwa Spika, kwa kushirikiana na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Wizara
imekamilisha maandalizi ya Muswada wa Sheria ya kusimamia Vyombo vya Habari na sasa
uko katika hatua nzuri. Kwa
kuzingatia utaratibu uliopo, Muswada huu utafikishwa katika Bunge lako Tukufu
lijalo la kutunga Sheria.
21.
Mheshimiwa Spika,
ili kuweza kuimarisha njia za mawasiliano kati ya Serikali na Wananchi wake,
Wizara inafanya maboresho ya Tovuti ya Wananchi ili kuweza kuimarisha mifumo na
monekano wa Tovuti hiyo. Maboresho hayo yakikamilika, yatawawezesha Wananchi
popote walipo
kuwasiliana na Serikali kwa kutumia njia za kisasa. Aidha itawapunguzia
wananchi gharama za kuwasilisha
kero, hoja na maoni mbalimbali katika Taasisi za Serikali. Kazi ya kuijenga
upya na kuimarisha Tovuti hiyo ili kuwa na muonekano mpya unaokidhi mabadiliko
ya sasa ya Sayansi na Teknolojia inatarajiwa kukamilishwa mwisho wa mwaka wa fedha 2013/2014.
22.
Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kukusanya habari, kupiga picha za matukio mbalimbali ya
Serikali na kuzihifadhi katika maktaba; pamoja na kuzisambaza kwenye vyombo
mbalimbali vya habari kwa lengo la kutoa habari na kuelimisha jamii. Wizara kama
Msemaji Mkuu wa Serikali, ilifafanua masuala na hoja mbalimbali zinazohusu
Serikali.
23.
Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kuratibu na kusimamia Vitengo vya Mawasiliano Serikalini
kwa lengo la kutoa habari na kuelimisha umma juu ya utekelezaji wa majukumu ya
Serikali. Wizara imetoa mwongozo ulioainisha taratibu za kuendesha Vitengo
hivyo na kuhimiza Wizara na Asasi zote za umma kuajiri Maafisa Mawasiliano
Serikalini. Hali kadhalika, Wizara imeratibu jumla ya mikutano 255 ya wasemaji
wa Asasi za Serikali na Vyombo vya Habari. Mikutano hii imesaidia kuwaelimisha
Wananchi kuhusu shughuli za Serikali zinazofanyika kwa maendeleo yao.
24.
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2013/2014, Wizara imeendelea kuratibu ushiriki wa vyombo vya
habari katika vikao vya Bunge vilivyofanyika Dodoma na pia kuhakikisha
inawapatia vitambulisho waandishi wa habari wa ndani na nje wenye sifa za
taaluma ya uandishi wa habari.
25.
Mheshimiwa Spika, Wizara yangu kwa kushirikiana na Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na
Teknolojia kupitia TCRA,
ilikamilisha awamu ya kwanza ya uhamaji wa kutoka katika mfumo wa utangazaji wa
analoji kwenda dijiti. Baada ya
zoezi hili tathmini imefanyika ambayo ilionesha mwitikio mzuri wenye
mafanikio. Hivi sasa zoezi hili
limeingia katika awamu ya pili iliyoanza tarehe 31 Machi 2014. Ni matarajio yetu kwamba uhamaji huu utakamilika kwa kuzingatia ratiba iliyopangwa
kabla ya tarehe
30, Juni 2015.
26.
Mheshimiwa Spika, katika
mwaka wa fedha wa 2013/2014, Wizara kwa kushirikiana na TCRA imesajili vituo nane
(8) vya redio na vituo viwili (2) vya televisheni na hivyo kuwezesha Tanzania
kuwa na jumla ya vituo 93 vya redio na 28 vya televisheni. Aidha uhamaji kutoka mfumo wa utangazaji wa analoji kwenda mfumo wa dijiti
umesadia kupanua wigo wa masafa na kuongeza ubora wa matangazo.
27.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2013/2014, Kamati ya Maudhui ilipokea na
kushughulikia malalamiko 7 ya vituo vya televisheni na redio kutokana na
kurusha vipindi ambavyo vilikiuka maadili ya utangazaji. Kituo binafsi cha
televisheni kilicholalamikiwa kwa kurusha kipindi kilichokiuka kanuni na
maadili ya utangazaji kilipewa onyo. Aidha, vituo 6 vya redio vilivyolalamikiwa
kwa kurusha vipindi vilivyokiuka kanuni za utangazaji na maadili ya uandishi wa
habari vilipewa onyo na vingine kutozwa faini kati ya Shilingi 200,000 na Shilingi
5,000,000.
28.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2013/2014, TBC imeendelea kuimarisha upanuzi
wa usikivu wa Redio na Televisheni ya Taifa. TBC pia ilirusha matangazo ya
vikao vya Bunge moja kwa moja. Aidha, TBC ilirusha matangazo ya Bunge Maalum la
Katiba kwa lugha za alama kwa ajili ya watu wenye mahitaji maalum. Pamoja na
kazi hizo, TBC inakabiliwa na tatizo la uchakavu
wa vifaa vya kurushia matangazo. Uchakavu huo wakati mwingine umesababisha tatizo
la kukatika kwa matangazo yakiwemo matangazo ya Bunge.
29.
Mheshimiwa Spika, naomba waheshimiwa wabunge wawe wavumilivu kwani Wizara imejipanga katika
kuendelea kutatua changamoto hizo ili kuboresha huduma zitolewazo na TBC.
Kupitia Bunge lako Tukufu niwaombe Waheshimiwa Wabunge watuunge mkono
kufanikisha malengo tuliyojiwekea.
30.
Mheshimiwa Spika, katika kuendelea kutatua changamoto za TBC, mwezi Aprili, 2014 imepokea gari
jipya la kisasa la matangazo kutoka Serikali ya Watu wa China. Gari hili
litasaidia sana kuongeza nguvu katika kupunguza tatizo la uchakavu wa vifaa.
Sambamba na hatua hizo, Wataalamu watano (5) wa TBC walipelekwa nchini China
kupata mafunzo maalum ya namna ya kutumia gari hilo pamoja na vifaa husika.
31.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2013/2014, Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN)
imeendelea na mkakati wa upanuzi wa kiwanda cha uchapaji. Katika mkakati huo, makubaliano
na Benki ya Rasilimali Tanzania (TIB) yamekamilika ambapo TIB itaipatia TSN
mkopo wa Shilingi bilioni 2.7 kwa ajili ya kujenga jengo la kitega uchumi.
32.
Mheshimiwa Spika, katika kupanua wigo wa mapato, TSN na Mamlaka ya
Mawasiliano Tanzania (TCRA) wameingia mkataba wa ubia wa kuendeleza kiwanja
kilichopo Kitalu Na. 27, Central Business Park, Dodoma, kwa ajili ya kujenga
jengo la kupangisha. Maandalizi ya ujenzi yameanza.
33.
Mheshimiwa Spika, katika kuboresha magazeti, TSN imeongeza kurasa za habari katika magazeti
ya ‘Daily News’ na Habari Leo. Vilevile, imeongeza weledi katika uhariri wa taarifa
ndani ya magazeti hayo. Uchapaji wa magazeti hayo unazingatia sera na maadili
ya uandishi wa habari.
34.
Mheshimiwa Spika, katika kuboresha usambazaji wa
magazeti, Kampuni imepata pikipiki 20 toka Serikali ya Watu wa China kwa ajili
ya usambazaji wa mijini. Aidha, TSN, imeingia makubaliano na kampuni za usafirishaji kusafirisha magazeti ndani
na nje ya nchi ili kuwezesha upatikanaji wa habari kwa wakati.
SEKTA YA
MAENDELEO YA VIJANA
35.
Mheshimiwa Spika, katika kushughulikia masuala ya vijana mwaka 2013/2014, Wizara
imekabiliana na changamoto mbalimbali zikiwemo, baadhi ya Sekretarieti za Mikoa
na Halmashauri za Wilaya kutokuajiri Maafisa Vijana, uelewa mdogo wa vijana katika
kubuni, kutayarisha maandiko ya miradi, kuanzisha na kutekeleza miradi endelevu.
36.
Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine ni vijana wengi kukosa ujuzi na maarifa ya
ujasiriamali na biashara ikiwa ni pamoja na kukosa ujuzi wa matumizi sahihi ya
fedha za mikopo wanazopata kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana.
37.
Mheshimiwa Spika, pamoja na changamoto hizi, Wizara imeendelea kuwajengea
vijana uwezo wa kiuchumi kwa kuwapa mafunzo na ujuzi katika maeneo ya
ujasiriamali, uanzishaji wa miradi endelevu ya uzalishaji mali, uongozi, stadi
za maisha na matumizi sahihi ya mikopo. Mafunzo haya yametolewa kwa vijana 668 katika ngazi ya Mikoa na Wilaya katika mwaka wa fedha 2013/2014.
38.
Mheshimiwa Spika, kutokana na kupungua kwa nafasi za ajira katika sekta
rasmi ikilinganishwa na idadi ya vijana wanaoingia katika soko la ajira kila
mwaka, Wizara kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo ya vijana imeendelea
kuhamasisha vijana kuunda makampuni binafsi ya biashara na vikundi vya kuzalisha
mali ili waweze kujiajiri. Mpango huu utasaidia kupunguza tatizo la ukosefu wa
ajira kwa vijana.
39.
Mheshimiwa Spika, ili kuimarisha na kuongeza mitaji katika miradi na
kampuni za vijana zinazoanzishwa, Wizara imeratibu mpango wa kuanzisha Benki ya
Vijana na tayari Mshauri Mwelekezi amepatikana. Mshauri huyo anaendelea na
upembuzi yakinifu wa uanzishwaji wa Benki hiyo.
40.
Mheshimiwa Spika, kuhusu Mfuko wa Maendelo ya Vijana, napenda kulitaarifu
Bunge lako Tukufu kwamba mwongozo wa kusimamia Mfuko huu umeandaliwa na
kusambazwa kwa Makatibu Tawala wa Mikoa yote tangu mwezi Agosti 2013. Kulingana
na Mwongozo huu, kila Halmashauri inahitajika kuanzisha SACCOS ya Vijana ambayo
itashughulikia utoaji wa mikopo hii. Hadi kufikia Aprili, 2014, Halmashauri 22 kati
ya 151 zimeanzisha SACCOS za Vijana.
41.
Mheshimiwa Spika, jumla ya Shilingi bilioni 6.1 zilitengwa kwa ajili ya Mfuko huu. Hadi
Aprili, 2014, Wizara imepokea kiasi cha Shilingi 2,000,000,000. Kati ya fedha hizo zilizokopeshwa ni Shilingi 172,609,000 kwa Miradi ya vikundi vya vijana 25. Hata hivyo, Wizara inaendelea na
uchambuzi wa maombi ya vikundi 1,178 yenye thamani ya Shilingi 8,421,906,750
ili kuweza kuvikopesha vikundi vitakavyotimiza vigezo
vilivyobainishwa kwenye mwongozo.
42.
Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kutekeleza Programu ya “Elimu ya Stadi
za Maisha kwa vijana walio nje ya shule”. Katika kipindi hiki, Wizara imeandaa
mafunzo kwa waelimishaji 75 wa kitaifa ambao watatoa mafunzo kwa waelimishaji
rika kuanzia ngazi ya Wilaya hadi Kata. Programu hii itawasaidia vijana
kujitambua na kufanya maamuzi sahihi yanayohusu maisha yao.
43.
Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kuhamasisha maendeleo ya wananchi, kudumisha umoja,
amani, upendo na mshikamano wa kitaifa kupitia Mbio za Mwenge wa Uhuru. Kwa
mwaka 2013, Mbio za Mwenge wa Uhuru zilizinduliwa tarehe 5 Mei, 2013 katika
kijiji cha Chokocho, Mkoani Kusini Pemba ambapo Mgeni Rasmi alikuwa Mhe. Dkt. Ali
Mohamed
Shein, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Maadhimisho ya
kilele cha mbio hizo yalifanyika mkoani Iringa tarehe 14, Oktoba, 2013 na Mgeni
Rasmi alikuwa Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania. Kupitia mbio hizo, jumla ya miradi ya maendeleo 1229 yenye thamani ya Sh. 158,587,667,613.40 ilizinduliwa au
kuwekewa mawe ya msingi. Uzinduzi
wa Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2014 umefanyika tarehe 2, Mei 2014 Mkoani
Kagera; na Mgeni Rasmi alikuwa Mhe. Dkt. Mohamed Gharib Bilal, Makamu wa Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
44.
Mheshimiwa
Spika,
sambamba na maadhimisho ya kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru, Wizara iliratibu
maadhimisho ya Wiki ya Vijana kitaifa ambayo yalianza tarehe 8 Oktoba na
kuhitimishwa tarehe 14 Oktoba, 2013 mkoani Iringa. Lengo la maadhimisho hayo ni
kuwakutanisha vijana kutoka sehemu mbalimbali hapa nchini na kuwapa fursa ya
kubadilishana uzoefu, ujuzi, kuonesha vipaji na ubunifu wa kazi zao, pamoja na kujenga
mtandao na wadau mbalimbali wa maendeleo ya vijana.
45.
Mheshimiwa
Spika, Maonesho katika Wiki ya Vijana yalishirikisha
wadau mbalimbali ikiwa ni pamoja na ofisi za mikoa 10, Idara za Serikali 16,
Halmashauri za Wilaya 21, Asasi za Kiraia 14, Vikundi vya Vijana Wajasiriamali
53, Vyuo Vikuu vya Elimu 3 na Taasisi za Kibenki 3. Jumla ya watu waliotembelea
mabanda ya maonesho ya Wiki ya Vijana ilikuwa ni 39,361. Aidha, katika Wiki
hiyo, Vijana 300 kutoka makundi mbalimbali ya Vijana walishiriki katika
midahalo ambapo pia walipatiwa mafunzo ya aina tofauti yenye lengo la
kuwajengea uelewa wa masuala mbalimbali ya maendeleo ya vijana.
46.
Mheshimiwa
Spika, washiriki
wa Wiki ya Vijana pia walipata fursa ya kupewa huduma ya ushauri nasaha na
upimaji wa VVU/UKIMWI kwa hiari kupitia taasisi zinazojihusisha na afya
zilizoshiriki katika maadhimisho hayo, kama vile WAMATA, AMREF – ANGAZA, HOSPITALI
YA RUFAA IRINGA na JHPIEGO - UHAI CT. Jumla ya Vijana 613 walipima afya zao
wakiwemo wanawake 397 na wanaume 216, kati yao vijana 27 sawa na asilimia 4.4
waligundulika kuwa na maambukizi ya VVU. Vijana waliogundulika kuwa na
maambukizi walipatiwa huduma ya ushauri wa namna ya kuishi vizuri na kwa
matumaini na jinsi ya kuendelea kupata huduma za afya.
SEKTA
YA MAENDELEO YA UTAMADUNI
47.
Mheshimiwa
Spika,
athari za utandawazi na maendeleo yenye kasi kubwa ya sayansi na teknolojia
vimeendelea kuwa ni changamoto kubwa inayokabili Maendeleo ya Utamaduni. Mmomonyoko wa maadili ulio dhahiri
nchini, sio tu miongoni mwa watoto na vijana bali pia hata baadhi ya watu
wazima, ni matokeo ya athari hasi za utandawazi na maendeleo ya kisayansi na
kiteknolojia yanayoambatana na matumizi mapana ya televisheni na mitandao
anuwai ya kijamii. Kwa upande mwingine, upatikanaji kirahisi wa mitambo ya kurudufu
kazi za wasanii, hasa wa filamu na muziki, umeendeleza dhuluma ya kipato kwa
wasanii wengi huku ukiwaneemesha mapromota na wasambazaji wa bidhaa za filamu
na muziki ambao sio wasanii.
Pamoja na changamoto
hizi, Wizara kupitia Sekta ya Maendeleo ya Utamaduni imetekeleza kazi zifuatazo
katika mwaka wa fedha wa 2013/2014.
48.
Mheshimwa Spika, katika kuimarisha ukusanyaji na uhifadhi wa takwimu za tasnia ya
utamaduni, Maofisa wawili walipata mafunzo ya namna ya kuainisha namba za
misimbo (code numbers) za sekta ya utamaduni ambazo zitatumika kitaifa na
kimataifa. Aidha, Wizara ilifanya tafiti za maktabani za lugha za jamii 10 na utafiti
wa uwandani katika Mikoa ya Dar es Salaam na Pwani ili kuhifadhi sarufi, misamiati
na istilahi za lugha ya Taifa - Kiswahili.
49.
Mheshimiwa Spika, mintaarafu utafiti wa mila na desturi, Wizara ilifanya utafiti wa kina kuhusu mila za jando na unyago miongoni
mwa jamii za Wamakonde, Wamakua na Wayao. Utafiti huo umewezesha kukamilisha maandalizi ya pendekezo la elementi ya urithi
usioshikika ambao hatimaye Serikali itaomba urithi huo uingizwe kwenye orodha
ya urithi wa utamaduni wa Dunia unaotambuliwa na UNESCO. Elementi hiyo ni ya
ngoma ya “Nankachanga” kutoka kijiji cha Namahonga, Wilaya ya Tandahimba, Mkoa
wa Mtwara.
50.
Mheshimwa Spika, Wizara imeendelea kuhakikisha kuwa Tanzania inanufaika ipasavyo na fursa
za ajira zinazotokana na nchi yetu kuteuliwa kuwa Makao Makuu ya Kamisheni ya
Kiswahili ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. Katika hili, Wizara kwa kushirikiana
na Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo ya Serikali ya Mapinduzi
Zanzibar, iliratibu zoezi la kuwapata Watanzania wenye sifa stahiki za
kuajirika katika Kamisheni hiyo. Ajira katika Kamisheni zitashindaniwa na nchi
zote wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, hivyo ni muhimu kwa Tanzania
kuwa na wagombea sadifu ili kuhimili vishindo vya kinyang’anyiro hicho.
51.
Mheshimiwa Spika, kuhusiana
na Programu ya Urithi wa Ukombozi wa Bara la Afrika, kazi ya ukusanyaji wa kumbukumbu za mapambano ya kupigania uhuru nchini
iliendelea kufanywa kwa kushirikiana na Maofisa Utamaduni wa Mikoa na Wilaya.
Kwa kipindi cha mwaka 2013/2014, jumla ya kumbukumbu 63 zimerekodiwa katika
kanzi data ya Programu. Programu hii ni muhimu sana katika kutunza na kuhifadhi
kumbukumbu za Ukombozi wa Bara la Afrika. Wizara inaendelea kutafuta ufadhili
kufanikisha malengo ya Programu.
52.
Mheshimiwa Spika, Wizara ilifanya kikao cha Makatibu Wakuu wa Wizara ambazo ni wadau wakuu
ili kujenga uelewa zaidi wa Programu. Aidha, washirika katika Programu hii
kutoka Namibia, Afrika Kusini na Msumbiji walikuja nchini kujifunza namna
Tanzania inavyotekeleza shughuli za uhifadhi na utunzaji wa kumbukumbu za
historia ya Ukombozi wa Nchi za Kusini mwa Bara la Afrika.
53.
Mheshimiwa
Spika,
katika
kipindi cha mwaka wa fedha wa 2013/2014, Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA)
liliandaa na kurusha vipindi 52 vya ‘Lugha ya Taifa’ kupitia TBC Taifa,
vipindi 52 vya ‘Kumepambazuka’ kupitia Radio One na vipindi 52 vya ‘Ulimwengu wa
Kiswahili’
kupitia Televisheni ya Taifa-TBC1. Vilevile, Baraza lilisoma jumla ya
miswada 24 ya vitabu vya taaluma na kuvipatia ithibati ya lugha.
54.
Mheshimiwa
Spika, Baraza limeratibu na
kutoa huduma ya tafsiri kwa Asasi 14 za Serikali, Mashirika ya Umma, pamoja na
watu binafsi. Aidha, huduma ya ukalimani ilitolewa kwenye Mkutano wa Wakuu wa
Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika huko Addis Ababa, Ethiopia, mwezi Julai,
2013 na mwezi Januari, 2014. Vilevile,
ukalimani ulifanyika kwenye Mkutano wa Bunge la Afrika nchini Afrika Kusini
mwezi Novemba, 2013 na Machi, 2014.
55.
Mheshimiwa
Spika, Baraza limeendelea
kufuatilia matumizi ya Kiswahili na kubaini jumla ya makosa 75 yaliyofanywa na
vyombo vya habari na watumiaji wengine wa Kiswahili kwa kusahihisha na kutoa
ushauri wa matumizi stahiki. Baraza katika kujiimarisha, limeongeza wigo wa
kiutendaji kwa kuandaa Kamusi Kuu ambapo fafanuzi za maneno (utomeshaji)
zimeingizwa na warsha tatu za kuhakiki zimefanyika.
56.
Mheshimiwa
Spika,
katika
kipindi cha mwaka wa fedha 2013/2014, Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA)
limeendesha midahalo 52 ya Jukwaa la Sanaa kwa wasanii, waandishi wa habari na
wadau wa sanaa 3,850. Vilevile, Baraza kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa
sanaa, limeendesha mafunzo ya utambaji wa hadithi, ngoma za asili kwa watoto
200 wa shule za msingi katika Mkoa wa Dar es Salaam kati ya Februari na Machi,
2014 kwa lengo la kuibua na kuendeleza vipaji vyao katika fani husika.
57.
Mheshimiwa
Spika,
Baraza
limeendesha mafunzo na kuhamasisha
watumishi 34 wa Baraza, wasanii na wadau 98 kupitia Jukwaa la Sanaa kuhusu
umuhimu wa kujikinga na maambukizi ya VVU na UKIMWI. Baraza limeendelea kuingiza taarifa muhimu za wasanii na
wadau wa sanaa za muziki katika mfumo wa kielektroniki unaounganisha Taasisi za
TRA, COSOTA, Bodi ya Filamu na BASATA. Hii itaimarisha urasimishaji wa tasnia
ya muziki. Aidha, Baraza limeendelea na hatua za awali za uandaaji wa mfumo wa
kanzi data za wasanii mahiri na kukusanya taarifa zao muhimu.
58.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka wa fedha 2013/2014, Bodi ya Filamu imeendelea kusimamia
utekelezaji wa Sheria ya Filamu na Michezo ya Kuigiza pamoja na Kanuni zake.
Bodi, kwa kushirikiana na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), imeendelea kuhimiza
matumizi ya stempu za kodi. Hadi sasa, jumla ya wadau 86 wamechukua Stempu
4,380,000 zilizotolewa kwa upacha (duplicate) kwa ajili ya kuweka kwenye kazi
za filamu na muziki. Kati ya hizo 3,810,000 ni kwa kazi za filamu na 570,000 ni
za muziki.
59.
Mheshimiwa
Spika,
Bodi imepitia miswada 139 ya kutengenezea filamu kwa watengenezaji wa ndani na
nje ya nchi. Hadi kufikia Aprili,
2014, jumla ya filamu 1,206 sawa na CD 2,412 zilikaguliwa na kuwekewa madaraja.
Kati ya filamu hizo, 127 zilifanyiwa marekebisho. Filamu 7 hazikuruhusiwa
kuonyeshwa hadharani. Aidha, kati ya filamu 215 za nje zilizowasilishwa, filamu
2 zilielekezwa kufanyiwa marekebisho. Jumla ya filamu 5 za nje zilizowasilishwa
zilizuiliwa kuonyeshwa hadharani. Aidha, Bodi imekagua na kuidhinisha maeneo 13
ya uzalishaji wa filamu.
60.
Mheshimiwa
Spika,
Bodi imeendelea kutoa elimu kuhusu urasimishaji wa tasnia ya filamu kupitia
matangazo kwenye magazeti, vipeperushi, mabango ya barabarani, maadhimisho na
sherehe mbalimbali, vipindi mbalimbali vya TV na Redio na vikao vya wadau.
61.
Mheshimiwa Spika, Bodi ilihamasisha
wadau kushiriki katika tuzo mbalimbali za filamu kitaifa na kimataifa ambapo
hadi kufikia Aprili 2014, jumla ya filamu 10 ziliingia katika tuzo mbalimbali
na filamu ya Mdundiko ya Kitanzania ilishinda katika tuzo ya kimataifa huko
Marekani.
62.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2013/2014, Taasisi ya
Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) iliendesha mafunzo ya stashahada kwa
wanachuo wapatao 238 na mafunzo ya muda mfupi kwa wasanii 255 walio kazini.
Vilevile, inaendelea na kazi ya kukamilisha
mitaala ya shahada ya kwanza ya sanaa za maonyesho na ufundi.
63.
Mheshimiwa Spika, TaSUBa ilisimamia na kuendesha tamasha la 32 la Sanaa na Utamaduni wa
Mtanzania ambapo vikundi 40 vya sanaa za maonyesho na vikundi 12 vya sanaa za
ufundi vya ndani na nje ya nchi vilishiriki. Aidha, TaSUBa ilishiriki mikutano
ya Jumuiya ya Afrika Mashariki iliyoitishwa kujadili mustakabali wa vituo vya
Jumuiya vyenye ubora uliotukuka (Centre of Exellence), ambapo TaSUBa ni
kimojawapo cha vituo hivyo.
SEKTA YA MAENDELEO YA MICHEZO
64.
Mheshimiwa
Spika, katika kipindi cha
mwaka wa fedha 2013/2014, Wizara imeendelea kukabiliana na changamoto
mbalimbali zikiwemo uchache wa wataalamu waliobobea katika fani mbalimbali za
michezo, upungufu wa miundombinu inayokidhi mahitaji ya sasa, mwamko mdogo wa
jamii kushiriki katika michezo na udhaifu wa uongozi katika baadhi ya vyama
mbalimbali vya michezo.
Pamoja na changamoto
hizo, Wizara katika kipindi cha mwaka wa fedha wa 2013/2014 imetekeleza kazi
zifuatazo.
65.
Mheshimiwa
Spika, Wizara imeendelea kutoa
mafunzo ya Stashahada ya Elimu ya Ufundishaji Michezo na Stashahada ya Uongozi
na Utawala kwa wanachuo 40 katika Chuo cha Maendeleo ya Michezo, Malya, mkoani
Mwanza. Aidha, Wizara imeendesha Mafunzo ya muda mfupi ya fani mbalimbali za
michezo kwa vijana 200, walimu 100 wa shule za Msingi, walimu 100 wa shule za
Sekondari, Viongozi wa Michezo na Makocha 102 katika Vituo vya Michezo vya
Kanda ya Kaskazini (Arusha) na Kusini (Songea). Hivi sasa zaidi ya asilimia 50
ya walimu ambao hushiriki katika uendeshaji na ufundishaji wa michezo kwa ajili
ya mashindano ya shule za msingi (UMITASHUMTA) na shule za sekondari (UMISETA)
ni wahitimu wa Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya, Vituo vya Michezo na Mpango wa Michezo kwa Jamii.
66.
Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kutafuta maeneo mapya ya ushirikiano wa kimataifa na
kufuatilia utekelezaji wa Mikataba kati ya nchi marafiki na Tanzania katika
Sekta ya Michezo. Kwa kushirikiana
na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China, Wizara imekamilisha hatua za awali za
kujenga miundombinu ya Mchezo wa kupanda Majabali (Rock Climbing) katika Chuo
Kikuu cha Dar es Salaam. Aidha, kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, Wizara
iliendesha Kongamano la Kimataifa la Viongozi Wanawake wa Michezo lililofanyika
Dar es Salaam tarehe 16 – 18 Desemba, 2013 na kushirikisha jumla ya nchi 17 za
Bara la Afrika na Ulaya.
67.
Mheshimiwa Spika, Wizara, kwa kushirikiana na Vyama vya Michezo,
imeendelea kufanya maandalizi ya timu za Taifa zitakazoshiriki kwenye michezo
ya Jumuiya ya Madola itakayofanyika Glasgow, Scotland, mwezi Julai, 2014. Timu za Michezo ya Riadha, Ngumi,
Kuogelea, Mieleka, Baiskeli, Judo, Paralimpiki na Mpira wa Meza zinatarajiwa
kushiriki katika mashindano hayo. Aidha, kwa kushirikiana na Wizara ya Mambo ya
Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, timu sita za Taifa za mchezo wa Riadha, Ngumi,
Kuogelea, Judo, Kunyanyua Vitu vizito na Mpira wa Meza zimepata fursa ya kuweka
kambi za mazoezi nchini China, Uturuki, Ethiopia na New Zealand kwa ajili ya
maandalizi ya michezo ya Jumuiya ya Madola.
68.
Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kusimamia ukamilishaji wa ukarabati wa Uwanja wa Uhuru
ambao ni sehemu ya eneo Changamani la Michezo lililoko Dar es Salaam. Ukarabati huu
unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwaka 2014.
69.
Mheshimiwa
Spika, Wizara ilitoa huduma
ya Kinga na Tiba kwa wanamichezo na wadau wa michezo 108,000 wa timu za michezo
mbalimbali. Vilevile, Wizara imeendelea na upimaji na utoaji wa elimu kwa
wanamichezo kuhusu udhibiti wa matumizi ya dawa na mbinu haramu za kuongeza
nguvu katika michezo.
70.
Mheshimiwa
Spika,
katika juhudi za kupambana na dawa na mbinu haramu za kuongeza nguvu michezoni,
Wizara imeendelea kutumia matukio ya michezo kama vile Ligi Kuu ya Vodacom, Kambi
za Timu za Taifa na Mashindano ya Riadha na Ngumi ya Kitaifa na Kimataifa,
kuchukua sampuli mbalimbali (damu, mate, jasho n.k) za wanamichezo kwa ajili ya
vipimo vya matumizi ya dawa za kuongeza nguvu katika michezo kwa uchunguzi
zaidi kwenye maabara zilizoko nchini Afrika Kusini. Hadi kufikia Aprili, 2014
wanamichezo 27 walichukuliwa vipimo. Hata hivyo, hakuna aliyegundulika kutumia dawa
na mbinu haramu baada ya majibu ya maabara.
71.
Mheshimiwa
Spika, katika kipindi cha
mwaka wa fedha 2013/2014, Baraza la Michezo la Taifa (BMT), kwa kushirikiana na
“UK Sport” na “British Council”, kupitia mradi wa “International Inspiration”,
limekamilisha uandaaji wa mifumo rasmi ya Elimu na Ithibati ya Ufundishaji wa Michezo
Nchini; Michezo Shirikishi kwa Jamii; Ufuatiliaji na Tathmini ya Maendeleo ya
Michezo Nchini; na Utambuzi na Ukuzaji wa Vipaji vya Michezo Miongoni mwa Vijana.
Mifumo hiyo inalenga kuinua maendeleo ya michezo nchini na inaendelea kufanyiwa
majaribio kwa ajili ya utekelezaji.
72.
Mheshimiwa
Spika, Baraza
limeendesha mafunzo ya utawala bora kwa vyama vya michezo 17, na kusimamia
uchaguzi kwa vyama na mashirikisho ya michezo 14. Aidha, kwa kushirikiana na
Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI, Baraza, limeendesha mafunzo ya michezo kwa
jamii kwa walimu 76 wa shule za msingi na sekondari katika Wilaya ya Mtwara
Vijijini.
73.
Mheshimiwa
Spika, Baraza liliandaa na
kuendesha Kongamano la Kimataifa kuhusu Mfumo wa Elimu ya Michezo kwa Jamii kwa
Nchi za Kanda ya V ya Michezo Barani Afrika. Kongamano hilo lilikuwa na lengo
la kuangalia namna ya kuwa na mfumo mmoja wa utoaji wa Elimu ya Michezo kwa Jamii
miongoni mwa nchi wanachama.
Kongamano hilo lilifanyika mwezi Novemba, 2013 huko Arusha na
kuhudhuriwa na nchi saba ambazo ni Uganda, Kenya, Rwanda, Ethiopia, Misri,
Zimbabwe na Tanzania.
74.
Mheshimiwa
Spika, Baraza
limeendesha mafunzo ya uamuzi na ukocha kwa walimu na wanafunzi 761, kati ya
hao walimu ni 421 na wanafunzi ni 340. Mafunzo haya, yaliyo katika majaribio ya
mradi wa “International Inspiration” yamefanyika katika mikoa ya Dar es salaam,
Arusha, Ruvuma, Mwanza na Mjini Magharibi, Zanzibar.
75.
Mheshimiwa
Spika, Baraza, kwa kushirikiana na Asasi ya Kimataifa ya
“Tackle Africa” inayojishughulisha na utoaji wa elimu ya kinga dhidi ya
maambukizi ya Virusi vya UKIMWI kwa kutumia mchezo wa soka, liliendesha mafunzo kwa wanawake 140 na
wasichana 8,000 katika Mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Morogoro na Lindi.
UTAWALA
NA MENEJIMENTI YA RASILIMALI WATU
76.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2013/2014, watumishi 51
wamehudhuria mafunzo katika fani mbalimbali. Kati ya hao, watumishi thelathini na wawili (32),
wamehudhuria mafunzo elekezi ambayo yaliandaliwa na Wizara kwa kushirikiana na
Taasisi mbalimbali za Serikali.
Aidha, watumishi kumi na saba (17) wamehudhuria mafunzo ya muda mrefu
ndani ya nchi na watumishi wawili (2) wanahudhuria mafunzo ya muda mrefu nje ya
nchi.
77.
Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha Utawala Bora na
ushirikishwaji watumishi sehemu za kazi, Wizara imeandaa na kuendesha vikao
viwili vya Baraza la Wafanyakazi pamoja na kusimamia uendeshwaji wa vikao
mbalimbali vya kiutawala katika kuimarisha utendaji kazi.
78.
Mheshimiwa Spika, katika usimamizi wa haki na maslahi ya watumishi, Wizara
imewapandisha vyeo watumishi 32 wanaostahili kwa kuzingatia miundo ya kada zao,
Sera ya Menejimenti na Ajira katika Utumishi wa Umma toleo la mwaka 1999 na
2008 pamoja na taarifa za Upimaji Kazi wa Wazi (OPRAS).
D: MPANGO NA
BAJETI KWA MWAKA WA FEDHA 2014 / 2015
79.
Mheshimiwa Spika, Mpango na Bajeti ya Wizara kwa mwaka
2014/2015 umezingatia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025; Mpango wa Taifa wa
Maendeleo wa Miaka Mitano 2011/2012 – 2015/2016; Malengo ya Taifa ya MKUKUTA
II; Ilani ya Uchaguzi ya Chama Tawala ya mwaka 2010 – 2015; Mpango Mkakati wa
Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo 2011/2012 – 2015/2016; Maagizo
ya Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
aliyoyatoa kwa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kwa nyakati
tofauti; Mwongozo wa Utayarishaji wa Mpango na Bajeti kwa mwaka 2014/2015 na
ushauri uliotolewa na Bunge pamoja na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maendeleo ya
Jamii kwa nyakati tofauti.
SEKTA YA HABARI
80.
Mheshimiwa Spika, katika
mwaka wa fedha 2014/2015, Wizara imepanga kutekeleza yafuatayo:-
(i) Kuisemea Serikali katika masuala muhimu yanayohitaji ufafanuzi kwa wananchi;
(ii) Kukusanya habari mbalimbali za matukio ya kiserikali na kuyasambaza kwa
wananchi;
(iii) Kuratibu Vitengo vya Mawasiliano Serikalini;
(iv) Kusajili magazeti na machapisho;
(v) Kuandaa jarida la Nchi Yetu na kulisambaza;
(vi) Kuratibu waandishi wa habari katika shughuli za kitaifa na kimataifa na
(vii)
Kuratibu utekelezaji wa Mradi wa Habari kwa Umma.
81.
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha wa 2014/2015, Shirika la Utangazaji
Tanzania (TBC) linakusudia:-
(i) Kurusha matangazo ya vikao vya Bunge;
(ii) Kulipia huduma ya kukodi “satellite” kwa ajili ya matangazo ya moja kwa
moja ya televisheni;
(iii) Kuhamisha na kujenga mitambo miwili (2) ya FM katika maeneo ya StarMedia
(T) Ltd ili kuboresha usikivu wa matangazo ya redio. Maeneo yatakayohusika na
zoezi hilo la uhamishaji wa mitambo yake ya FM ni Iringa na Dodoma;
(iv) Kujenga mtambo mpya mmoja (1) wa FM redio kwa ajili ya kuboresha usikivu wa
matangazo katika eneo la Ngorongoro mkoani Arusha na
(v) Kujenga studio mbili (2) za redio katika Mikoa ya Dar es Salaam na Dodoma
pamoja na kufunga vifaa vya kisasa.
82.
Mheshimiwa Spika, Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN) kwa mwaka 2014/2015
imepanga kutekeleza yafuatayo:-
(i)
Kukamilisha mradi wa upanuzi wa kiwanda cha uchapaji na
(ii) Kuendelea na mchakato wa
kuendeleza kiwanja kilichopo Kitalu Na. 27, Central Business Park, Dodoma, kwa
ubia na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA).
83.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2014/2015, Wizara kupitia
Kamati ya Maudhui ya Utangazaji imepanga kutekeleza yafuatayo:-
(i)
Kupitia na kutoa mapendekezo ya marekebisho ya Sheria na
Kanuni za Utangazaji;
(ii) Kutengeneza rasimu ya kanuni ndogo za maudhui ya Utamaduni wa Mtanzania;
(iii) Kutengeneza mwongozo wa
udhamini wa matangazo (Codes of Advertising and Sponsorship);
(iv) Kuanzisha utaratibu wa kutoa motisha (Incentive scheme) kwa watengenezaji
na vituo vya utangazaji vitakavyorusha vipindi vyenye maudhui bora ya
Mtanzania;
(v) Kuendesha warsha za mashauriano na wadau wa maudhui wa kujitegemea na
(vi) Kusimamia awamu ya pili ya uhamaji kutoka mfumo wa analoji kwenda mfumo wa
dijiti katika miji yote ambayo haijafikiwa na mfumo huu mpya.
SEKTA YA MAENDELEO
YA VIJANA
84.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2014/2015 Wizara imepanga kutekeleza
majukumu yafuatayo:-
(i) Kuratibu mafunzo ya Ujasiriamali; Uanzishaji na Uendeshaji wa Miradi na
Kampuni Endelevu, Uongozi na Stadi za Maisha kwa viongozi wa vikundi vya vijana
vya uzalishaji mali na asasi za vijana ili kuwajengea uwezo wa kujiajiri na kuajirika,
hivyo kujikimu kiuchumi na kijamii;
(ii) Kuratibu Mbio za Mwenge wa Uhuru ili kuhamasisha wananchi kudumisha amani,
upendo na mshikamano wa kitaifa. Aidha, Wizara itaratibu maadhimisho ya Wiki ya
Vijana ili kuwapa fursa za kubadilishana uzoefu, ujuzi, kuonesha vipaji na kazi zao za uzalishaji mali, ubunifu
pamoja na kuwawezesha kujenga mitandao baina yao na wadau mbalimbali;
(iii) Kuendelea na maandalizi ya uanzishwaji wa Benki ya Vijana ili kuwezesha
vijana pamoja na SACCOS za vijana kupata mitaji kwa ajili ya shughuli zao za
kiuchumi;
(iv) Kuendelea kuwezesha Vijana kiuchumi kwa kuwapatia mikopo yenye masharti
nafuu kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana ili waweze kujiajiri wenyewe na
hivyo kupunguza tatizo la ajira miongoni mwao na umaskini kwa ujumla na
(v) Kuimarisha vituo vitatu vya mafunzo ya vijana ili viweze kutumika ipasavyo
katika kutoa mafunzo ya ujasiri, ujasiriamali, uongozi na stadi za maisha.
SEKTA YA MAENDELEO YA UTAMADUNI
85.
Mheshimiwa
Spika,
katika kipindi cha mwaka wa fedha 2014/2015, Wizara
itatekeleza majukumu yafuatayo:-
(i)
Kuratibu mjadala wa Kitaifa kuhusu maadili ya Mtanzania;
(ii) Kukuza na kuendeleza matumizi sanifu na fasaha ya lugha ya Kiswahili na
kufanya utafiti wa msamiati wa lugha za jamii;
(iii) Kuratibu mikutano, matamasha ya sanaa na ushiriki wa wasanii katika Sherehe
za Kitaifa;
(iv) Kuratibu utafiti, uhifadhi na uorodheshaji wa urithi wa utamaduni na
(v) Kuratibu utekelezaji wa miradi ya Ujenzi wa Jumba la Utamaduni na Programu
ya Urithi wa Ukombozi wa Bara la Afrika.
86.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2014/2015 Baraza la
Kiswahili la Taifa (BAKITA) limepanga kutekeleza majukumu yafuatayo:-
(i) Kuandaa na kurusha vipindi 52 vya ‘Lugha ya Taifa’ katika TBC Taifa, vipindi 52 vya ‘Kumepambazuka’ katika Radio One na vipindi 52 vya ‘Ulimwengu wa Kiswahili’ katika Televisheni ya Taifa (TBC1) ili kuhamasisha na
kuelimisha matumizi sahihi ya Lugha ya Kiswahili;
(ii) Kusoma Miswada ya vitabu vya taaluma na kuipatia ithibati ya lugha;
(iii) Kuratibu na kutoa huduma za tafsiri na ukalimani katika mikutano ya kitaifa
na kimataifa, shughuli za mashirika, makampuni na watu binafsi;
(iv) Kuchunguza makosa ya Kiswahili yanayofanywa na vyombo vya habari na
watumiaji wengine na kufanya masahihisho ya makosa hayo;
(v) Kuandaa Kamusi Kuu ya Kiswahili Sanifu;
(vi) Kuchapisha Kitabu cha Furahia Kiswahili (Kiswahili kwa Wageni) na
(vii)
Kukarabati majengo ya ofisi yaliyonunuliwa kutoka Shirika
la Bima la Taifa.
87.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2014/2015 Baraza la
Sanaa la Taifa (BASATA) limepanga kutekeleza majukumu yafuatayo:-
(i) Kuendesha mafunzo ya utambaji hadithi, ngoma za asili na uigizaji kwa
watoto 200 wa shule za msingi 5 za Mkoa wa Dar es salaam kwa lengo la kuibua na
kuendeleza vipaji vya watoto katika fani husika;
(ii) Kuendesha mafunzo ya sanaa na ujasiriamali kwa wasanii 100 katika mkoa wa
Tabora;
(iii) Kuendesha midahalo 30 kwa wasanii, waandishi wa habari na wadau wa sanaa
3,000;
(iv) Kusajili wasanii na wadau wanaojishughulisha na shughuli za sanaa katika
Mikoa ya Dar es salaam, Arusha, Mwanza, Morogoro na Mbeya;
(v) Kusanifu, kuboresha na kuhifadhi maelezo ya wasanii katika kanzi data ya
BASATA;
(vi) Kutoa elimu ya urasimishaji wa tasnia ya muziki kwa wadau wa sanaa na
(vii) Kuendelea na ujenzi wa Ukumbi wa Wazi wa sanaa na mafunzo.
88.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2014/2015, Bodi ya
Filamu imepanga kutekeleza majukumu yafuatayo;
(i) Kuendelea na Urasimishaji wa Tasnia ya Filamu;
(ii) Kukagua na
kuweka madaraja ya filamu 600;
(iii) Kupitia
miswada 150 ya kutengeneza filamu na kutoa vibali 150 vya kutengeneza filamu
kwa waombaji wa ndani na nje ya nchi;
(iv) Kuendelea
kutoa elimu ya kulinda Maadili ya Mtanzania kupitia tasnia ya filamu na
(v) Kufanya
utafiti wa masuala ya filamu na kuendesha mafunzo ya kujenga weledi kwa wadau
150 wa filamu.
89.
Mheshimiwa
Spika,
katika
kipindi cha mwaka wa fedha 2014/2015 Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo
(TaSUBa) imepanga kutekeleza majukumu yafuatayo:-
(i) Kuendesha mafunzo ya
stashahada kwa washiriki 250 na mafunzo ya muda mfupi kwa wasanii 270 walio
kazini;
(ii) Kusimamia na kuendesha Tamasha la 33 la Sanaa na Utamaduni wa Mtanzania na
(iii) Kuboresha studio ya picha jongefu na kununua vifaa vya muziki.
SEKTA YA
MAENDELEO YA MICHEZO
90.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2014/2015 Wizara
itatekeleza yafuatayo:-
(i) Kuratibu ushiriki wa timu za Taifa kushiriki Michezo ya Jumuiya ya Madola
itakayofanyika Glasgow, Scotland, mwezi Julai 2014;
(ii) Kutoa mafunzo ya Stashahada ya Elimu ya Ufundishaji wa Michezo na
Stashahada ya Utawala na Uongozi wa Michezo katika Chuo cha Maendeleo ya
Michezo Malya;
(iii) Kutoa huduma ya tiba na kinga kwa wanamichezo na kuendelea na juhudi za
kudhibiti matumizi ya dawa na mbinu haramu za kuongeza nguvu katika michezo;
(iv) Kuendesha mafunzo ya muda mfupi ya fani mbalimbali za michezo kwa wadau 200
katika Vituo vya Michezo vya Kanda ya Kusini (Songea) na Kaskazini (Arusha);
(v) Kusajili Vyama na Vilabu vya Michezo;
(vi) Kuimarisha uendeshaji wa michezo shuleni na ubora wa mashindano ya
UMITASHUMTA na UMISETA kwa kutoa nafasi zaidi kwa walimu wa shule za msingi na
sekondari kupata mafunzo ya ufundishaji wa michezo mbalimbali katika Chuo cha
Maendeleo ya Michezo Malya, Vituo vya Michezo vya Arusha na Songea na fursa
nyingine kwa kadri zitakavyopatikana;
(vii) Kuratibu ukamilishaji wa Uboreshaji wa Uwanja wa Uhuru na
(viii) Kuratibu uendeshaji wa Uwanja wa Taifa na uboreshaji wa miundombinu katika
Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya.
91.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2014/2015 Baraza la
Michezo la Taifa (BMT) litatekeleza yafuatayo:-
(i) Kuandaa na kuendesha mafunzo ya muda mfupi kwa walimu 200 wa michezo kwa
kushirikiana na mamlaka mbalimbali za serikali za mitaa kupitia Mpango wa
Michezo Jumuishi kwa Jamii “Integrated Community Sports”;
(ii) Kutoa mafunzo ya Utawala Bora katika Sekta ya Michezo kwa viongozi wa
Mashirikisho na Vyama Vya Michezo katika ngazi mbalimbali;
(iii) Kuratibu na kusimamia chaguzi za Vyama Vitano (5) vya Michezo na
(iv) Kuhamasisha wadau mbalimbali wa Michezo kushiriki katika majaribio ya
kutumia mifumo rasmi ya michezo katika kutekeleza Programu zao za Maendeleo ya
Michezo nchini.
UTAWALA NA MENEJIMENTI YA RASILIMALI WATU
92.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2014/2015, Wizara imepanga kutekeleza
yafuatayo:-
(i) Kuendelea kuwajengea uwezo watumishi kwa kuendesha mafunzo ya muda mfupi
kwa kuzingatia makundi ya kada zao.
Mafunzo hayo yatalenga katika kuimarisha utendaji kazi. Aidha, Wizara
itatoa elimu ya maadili kwa watumishi ili kuimarisha nidhamu ya kazi;
(ii) Kuendelea kuhamasisha watumishi kukubali kupimwa UKIMWI ili kutambua hali
zao. Aidha, Wizara itaendelea
kutoa msaada wa chakula na lishe kwa watumishi wanaoishi na VVU na UKIMWI ambao
wamejitokeza;
(iii) Kuhakikisha watumishi wanaostahili wanapandishwa vyeo kwa kuzingatia miundo
ya kada zao, Sera ya Menejimenti katika Utumishi wa Umma ya mwaka 1999 na 2008
pamoja na taarifa za Upimaji Kazi wa Wazi (OPRAS) na
(iv) Kuendelea kuimarisha utawala bora na ushirikishwaji watumishi sehemu za
kazi kwa kuendesha vikao vya Baraza la Wafanyakazi pamoja na vikao vingine vya
kiutawala ili kuimarisha utendaji kazi.
E: HITIMISHO
93.
Mheshimiwa
Spika, Wizara itaendeleza mafanikio
yaliyopatikana katika Sekta inazozisimamia ili ziweze kuchangia zaidi katika
maendeleo ya nchi yetu. Hii ni pamoja na kuongeza ajira, kipato, kulinda
mazingira, kudumisha amani na mshikamano katika jamii. Wizara itaendelea
kukabiliana na changamoto zilizoainishwa katika hotuba hii ili zipatiwe
ufumbuzi ili fursa zinazopatikana katika Sekta za Wizara ziweze kutumika
ipasavyo katika kuleta maendeleo ya nchi. Napenda kuwahakikishia wananchi ya kwamba
Wizara ina nia thabiti ya kuzipatia ufumbuzi changamoto zilizopo hatua kwa
hatua kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo.
SHUKRANI
94.
Mheshimiwa Spika, naomba kutoa shukrani za dhati kwa wote walioshirikiana nasi katika
kipindi cha mwaka wa fedha 2013/2014 katika kutimiza malengo yetu. Ushirikiano
huu utaendelezwa na kuimarishwa zaidi kwa manufaa ya Taifa ili kuhakikisha
kuwa umma wa Watanzania unapata
taarifa za kina na za uhakika, vijana
wanaendelea kujiajiri na kuajirika, maadili na utamaduni wa Mtanzania
unazingatiwa, pamoja na kuwa Taifa
lenye ufanisi kupitia michezo. Mafanikio ya utekelezaji wa majukumu na malengo
ya Wizara yamewezekana kutokana na ushirikiano uliopo miongoni mwa viongozi na
watumishi wa Wizara na wadau wengine walio nje ya Wizara.
95.
Mheshimiwa Spika, shukrani zangu za pekee ziende kwa
Mhe. Alhaji Juma Suleiman Nkamia
(Mb.), Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo ambaye amekuwa
msaada mkubwa kwangu, Bibi Sihaba
Nkinga, Katibu Mkuu na Prof. Elisante Ole Gabriel, Naibu Katibu Mkuu. Ninawashukuru kwa uchapakazi wao mahiri na ushirikiano
mkubwa walionipatia katika kutekeleza majukumu yangu. Aidha, nawashukuru
Wakurugenzi, Wakuu wa Vitengo, Watendaji Wakuu wa Asasi, Wataalamu na Watumishi
wote wa Wizara kwa juhudi walizofanya kuhakikisha kwamba tunatimiza ipasavyo
majukumu tuliyokabidhiwa na Taifa.
96.
Mheshimiwa Spika, napenda niwashukuru Wenyeviti na wajumbe wa Bodi za Asasi zilizo chini ya
Wizara kwa jinsi wanavyofanya kazi kwa kushirikiana na Wizara. Asasi hizo zimefanya kazi kwa karibu sana na mimi na nawaomba waendelee kufanya
kazi kwa uadilifu na weledi mkubwa ili kuhakikisha Wizara yetu inafikia malengo
yake.
97.
Mheshimiwa Spika, kwa dhati kabisa nitumie fursa hii tena kuwashukuru washirika wetu wa
maendeleo ambao wametuunga mkono wakati wote wa kutekeleza majukumu ya
Wizara. Shukrani hizi ziwaendee
wahisani waliotusaidia, nikitarajia kuwa wataendelea na moyo huo. Siyo rahisi
kuwataja wote lakini nitaje wachache ambao ni Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China, Finland,
Uingereza, Denmark, Japan, Sweden, Norway, Iran, Cuba, Ethiopia, New Zealand, Turkey,
Korea ya Kusini, Marekani na Ujerumani pamoja na
Mashirika ya Kimataifa ya UNESCO, UNICEF, UNFPA,
IYF, UNDP, ILO, Forum - SYD, BRAC, Balton Tanzania Limited, JICA, CYP, ESAMI, RALEIGH
INTERNATIONAL, VSO, AMREF, Restless Development na BRITISH COUNCIL.
98.
Mheshimiwa
Spika, napenda kuvishukuru vyombo vyote vya habari nchini ambavyo vimefanya kazi nzuri ya kuhabarisha,
kuelimisha na kuburudisha umma. Ninaamini kuwa vyombo hivyo vitaendelea na kazi
hiyo kwa kuzingatia maadili na weledi. Aidha, ninamshukuru sana Mpiga Chapa
Mkuu wa Serikali kwa kuchapisha hotuba hii kwa wakati, bila kuvisahau vituo vya
Televisheni na Redio ambavyo kwa namna ya pekee vinarusha hotuba hii hewani
moja kwa moja.
MAKADIRIO
YA BAJETI KWA MWAKA WA FEDHA 2014/2015
Mapato
99.
Mheshimiwa
Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha
2014/2015 Wizara imepanga kukusanya jumla ya Shilingi
1,149,008,000 kutoka katika vyanzo vyake mbalimbali vya mapato. Mchanganuo
wa makusanyo kifungu kwa kifungu kwa mwaka 2013/2014 na Makadirio kwa mwaka
2014/2015 upo katika Kiambatisho Na. I.
Matumizi ya
Kawaida
100.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2014/2015 Wizara imetengewa
jumla ya Shilingi 20,371,844,000 kwa ajili ya
Matumizi ya Kawaida (Matumizi Mengineyo na Mishahara), fedha hizo zinajumuisha:-
(i)
Mishahara ya Wizara Sh. 3,151,654,000
(ii)
Mishahara ya Asasi Sh. 7,849,270,000
(iii) Matumizi Mengineyo
ya Wizara - Sh. 5,830,920,000.
(iv) Matumizi Mengineyo
ya Asasi Sh.
3,540,000,000.
Mchanganuo wa
makadirio ya Matumizi ya Kawaida ya Wizara na Asasi upo katika Kiambatisho Na. II. Matumizi
ya Kawaida kwa Wizara peke yake rejea Kiambatisho
Na. III na kwa Asasi rejea Kiambatisho Na. IV.
Miradi ya
Maendeleo
101.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2014/2015 Wizara imetengewa jumla ya Shilingi
15,000,000,000 kwa ajili ya kutekeleza Miradi ya
Maendeleo. Mchanganuo kamili upo katika Kiambatisho Na. V.
MAOMBI YA FEDHA
KWA AJILI YA KUTEKELEZA MPANGO WA MWAKA 2014/2015.
102.
Mheshimiwa Spika, ili Wizara iweze kutekeleza majukumu na malengo yake ya mwaka wa fedha
2014/2015, naomba sasa Bunge
lako Tukufu liidhinishe bajeti ya jumla
ya Shilingi 35,371,844,000 ambapo kati ya hizo, fedha za Matumizi ya Kawaida ni Shilingi 20,371,844,000 na Fedha za Miradi ya Maendeleo ni Shilingi 15,000,000,000. Mchanganuo wa fedha hizi upo
katika viambatisho vilivyotajwa hapo awali ambavyo ni sehemu ya Hotuba hii.
103.
Mheshimiwa Spika, napenda nitoe tena shukrani zangu za dhati kwako binafsi na kwa
Waheshimiwa Wabunge kwa kunisikiliza. Hotuba hii inapatikana pia katika tovuti
ya Wizara kwa anuani ya: www.habari.go.tz
na www. tanzaniangovernment.blogspot.com
104.
Mheshimiwa
Spika, naomba kutoa hoja.
No comments:
Post a Comment