ASKARI MAJAMBAZI WAHUKUMIWA KIFUNGO CHA MIAKA 30 JELA

Mahakama ya Mkoa wa Mbeya imewahukumu watu watano wakiwemo askari wawili wa polisi na magereza kwenda jela miaka 30 kila mmoja kwa kosa la unyangÕanyi wa kutumia silaha.
Waliohukumiwa ni aliyekuwa askari wa jeshi la polisi, PC James (32) na askari wa jeshi la magereza Juma Musa(37).
Wengine ni Eli Elinez Eliub maarufu kama Mshana(28),Mbaruku Hamis(29) na Amri Kihenya Amri(38).
Wametiwa hatiani kwa kosa la unyang'anyi wa kutumia silaha walilotenda Januari 3, Mwaka huu saa 11 jioni katika eneo la Mlima Kawetere barabara ya Mbeya/Chunya.
Katika hati ya mashitaka, mawakili wa serikali Basilius Namkambe na Achileus Mulisa mbele ya hakimu mkaazi mfawidhi wa mahakama hiyo,  Michael Mteite walidai washitakiwa hao walitenda kosa hilo kwa pamoja.
Ilidaiwa walizuia gari lenye namba T 756 ABL aina ya Toyota Pick Up lililokuwa likiendeshwa na Ezekia Matatira (34) Mkazi wa Iyunga Jijini Mbeya akiwa na Sreedhar Pasupelet (38).
Kwa mujibu wa hati ya mashitaka, washitakiwa hao wakiwa na pingu na panga moja, waliwateka wafanyabiashara na kuwapora fedha taslimu Sh milioni tatu,mabegi matatu yaliyokuwa na nguo, kompyuta mpakato moja aina ya Samsung ,simu ya kiganjani aina ya Samsung  pia na mablanketi mawili.
Akisoma hukumu, Hakimu Mteite alisema ushahidi uliotolewa na shahidi wa kwanza ambaye alikuwa dereva Ezekia Matatira (34) na shahidi wa pili  Sreedhar Pasupelet(38) haukuacha shaka yoyote na ulishabihiana.
Wakili wa utetezi, Ladilaus Lwekaza, aliomba mahakama kuwapunguzia hukumu washtakiwa kwa kile alichodai ni vijana na hawana rekodi ya makosa ya nyuma.
Hakimu Mteite alifuta adhabu ya viboko kutokana na mshitakiwa namba mbili kujeruhiwa kwa risasi wakati wa tukiona akasisitiza kila mmoja kutumikia adhabu ya kifungu cha miaka 30.

No comments: