Sahau
kuhusu matokeo ya watani wa jadi Jumapili iliyopita ambayo Yanga ilifungwa bao
1-0 na Simba. Yanga imezinduka, na imejibu mapigo kwa ushindi mnono katika
michuano ya kimataifa.
Wiki moja baada ya kipigo hicho, Yanga
imeiangushia kipigo Platinum FC ya Zimbabwe cha mabao 5-1 katika mechi ya
kwanza ya raundi ya kwanza ya Kombe la Shirikisho Afrika iliyochezwa leo jioni kwenye
Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Kama Simba shujaa wao ni Emmanuel Okwi, basi
shujaa wa Yanga ni Mrisho Ngasa. Winga huyu mwenye kasi, jana alitengeneza
nafasi nyingi kwa wenzake kufunga, lakini mwenyewe akafunga mabao mawili kati
ya hayo matano.
Ngasa alimtengenezea Amisi Tambwe bao la tatu
huku mengine yakifungwa na Salum Telela na Haruna Niyonzima, kiungo wa Rwanda
aliyekuwa nahodha jana badala ya Nadir Haroub ‘Cannavaro’ ambaye aliumia katika
pambano la watani wa jadi na kulazimika kushonwa nyuzi saba juu kidogo ya
jicho.
Kikosi cha Hans van Pluijm kilianza kuandika bao
la kwanza katika dakika ya 32, likifungwa na kiungo mkabaji, Telela baada ya
kupokea pasi nzuri ya Niyonzima na kuupitisha mpira juu ya kipa wa Platinum FC,
Petros Mhari aliyekuwa ametoka langoni kwake kumkabili mfungaji.
Baada ya kupata bao hilo, Yanga ilichachamaa na
dakika ya 42, Niyonzima aliifungia bao la pili akimalizia kazi nzuri ya Simon
Msuva aliyepiga krosi iliyosababisha piga nikupige langoni mwa Platinum na
mpira kumkuta mfungaji aliyeukwamisha wavuni kwa shuti la kiufundi la
chinichini.
Lakini hata hivyo bao hilo lilidumu kwa dakika
mbili tu kabla ya wageni kupata bao la kwanza dakika ya 45 likifungwa na kiungo
Walter Musoma aliyefunga kwa mpira wa adhabu ndogo kutokana na Telela kufanya
madhambi nje kidogo ya eneo la penalti na kufanya matokeo kuwa 2-1 hadi
mapumziko.
Iliwachukua dakika moja baada ya mapumziko,
Yanga kuandika bao la tatu mfungaji akiwa Tambwe aliyepokea krosi ya Ngasa,
kabla ya Ngasa kufunga bao lake la kwanza dakika ya 56 akimalizia mpira
uliopigwa na Telela.
Platinum ambao walionekana kupotezana kabisa
uwanjani kutokana na mabao hayo kuingia mfululizo kitu kilichosababisha kipa
wao Mhari kumfuata kocha wake Norman Mapeza ili abadilishe safu ya ulinzi ndipo
alipotolewa Wellington Kamudyariwa na nafasi yake kuchukuliwa na Simon Shoko.
Katika dakika ya 64, nusura Platinum ijipatie
bao la pili baada ya mfungaji wa bao lao la kwanza, Musoma kupiga mpira wa
adhabu ndogo uliogonga mwamba wa pembeni na kurudi uwanjani na mabeki wa Yanga
kuokoa.
Wakati mashabiki wakiamini matokeo yatabaki
hivyo, Ngassa alifunga bao la tano katika dakika ya 90, safari hii akimalizia
pasi nzuri iliyochongwa na Kaph Sherman aliyeingia katika dakika ya 68 kuchukua
nafasi ya Msuva.
Awali kabla ya kupata mabao hayo, Yanga
walipoteza nafasi tano za wazi katika dakika za 15, 17, 20 na 22 kupitia kwa
washambuliaji wake Msuva, Ngassa, Tambwe na Niyonzima ambaye jana alionesha
kiwango cha juu.
Yanga ilitinga hatua hiyo kwa kuwatoa BDF XI ya
Botswana kwa jumla ya mabao 3-2 wakati Platinum ambayo sasa ina kibarua kizito
kwao, iliitoa Sofapaka ya Kenya kwa jumla ya mabao 4-2.
Yanga:
Ally Mustapha ‘Barthez,’ Juma Abdul/Hassan Dilunga, Oscar Joshua, Mbuyu Twite,
Kelvin Yondani, Said Juma, Telela, Niyonzima, Tambwe, Ngassa na Msuva/Sherman.
No comments:
Post a Comment