Serikali ya Tanzania imesaini mkataba
wa ukarabati wa Uwanja wa Kimataifa wa Ndege wa Kilimanjaro (KIA) na majengo ya
uwanja huo na kampuni ya ujenzi ya
kimataifa ya Uholanzi, iliyoshinda tenda ya kufanya kazi hiyo ndani ya miezi 23.
Mkataba huo ulisainiwa mwishoni mwa
wiki na Meneja wa kampuni hiyo, Erick
Van Zuthem na mwenzake, Harko Kloeze ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni
hiyo Afrika na Afrika ya Kati.
Kwa upande wa Tanzania, mkataba huo
ulisainiwa na Mkurugenzi Mtendaji wa KADCO na Christopher Mkoma, ambaye ni
Mkurugenzi wa Uendeshaji na Ufundi wa uwanja huo.
Akizungumza mara baada ya kusainiwa
kwa mkataba huo, Mkoma alisema kuwa wanatarajia kutumia Euro milioni 37, sawa
na zaidi ya Sh bilioni 70.
Alisema katika ukarabati huo utafanyika
kwa wakati uliopangwa na bila kuharibu safari za ndege.
"Uwanja huu ulijengwa na Mwalimu
tangu mwaka 1971 tangu wakati huo hadi leo haujawahi kukarabatiwa tena, hivyo
unahitaji matengenezo makubwa ambayo yatakwenda sambamba na kuongeza
miundombinu ya maji safi na salama ili yaweze kuwa ya uhakika na mengi
kulingana na mahitaji ya uwanja huo," alisema.
Alisema maji yanahitajika kwa sababu
mbalimbali, ikiwemo kuhakikisha magari ya zimamoto hayakosi maji kwa usalama wa
ndege zinazotua na kuruka. Mbali na
ndege za kawaida, kwa siku ndege 12 za kimataifa hutua.
No comments:
Post a Comment