UPELELEZI DHIDI YA KIONGOZI WA UAMSHO BADO KUKAMILIKA


Kiongozi wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu Zanzibar (JUMIKI) Shekhe Farid Hadi Ahmed (45) na wenzake wanaokabiliwa na kesi ya ugaidi bado wanasota rumande kwa kwa kuwa upelelezi wa kesi bado haujakamilika.

Kesi hiyo ilitajwa jana mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Janeth Kaluyenda.
Wakili wa Serikali Mwandamizi, Tumain Kweka aliomba tarehe nyingine ya kutajwa kwa kuwa upelelezi bado haujakamilika pia wanasubiri uamuzi wa rufaa waliyoikata Mahakama ya Rufaa dhidi ya uamuzi uliotolewa na Jaji wa Mahakama Kuu, Dk Fauzi Twaib.
Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) alikata rufaa kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam ulioamuru Mahakama ya Kisutu kusikiliza na kutolea uamuzi hoja, zilizowasilishwa na Shekhe Farid na wenzake.
Katika ombi lao, washitakiwa waliomba Mahakama ya Kisutu ifute mashitaka ya ugaidi dhidi yao, pia walihoji uhalali wa kushitakiwa Tanzania Bara wakati Zanzibar ni nchi ambayo ina Mahakama Kuu na kuomba wakashtakiwe katika sehemu walizokamatwa.
Hakimu Kaluyenda aliahirisha kesi hiyo hadi Aprili Mosi ,2015 kwa ajili ya kuangalia kama upelelezi utakuwa umekwisha kamilika pia kusubiri uamuzi wa Mahakama ya Rufaa.
Washitakiwa wanadaiwa kati ya Januari mwaka jana na Juni mwaka huu katika maeneo ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, walikula njama ya kutenda kosa kwa kutafuta watu wa kushiriki vitendo vya ugaidi.
Katika mashitaka mengine, wote wanadaiwa katika kipindi hicho, huku wakijua ni kosa walikubaliana kuwaingiza nchini, Sadick Absalom na Farah Omary washiriki vitendo vya ugaidi.

No comments: