Kamati Kuu ya
CCM (CC) imewasimamisha uongozi wa vikao vya chama, vigogo watatu wa chama
hicho, akiwemo Waziri wa zamani wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi,
Profesa Anna Tibaijuka kutokana na kuhusishwa na sakata la Escrow.
Wengine
waliosimamishwa kuhudhuria vikao vinavyohusu uamuzi wa chama ni pamoja na
Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge na Mbunge wa Sengerema, William
Ngeleja.
Hatua hiyo
inatokana na uamuzi wa Kamati Kuu iliyoketi Januari, mwaka huu Zanzibar,
kuagiza Kamati ndogo ya Maadili kuwaita na kushughulikia suala la viongozi wa
chama hicho, waliokuwemo katika vikao vya uamuzi ya chama hicho waliohusishwa
na sakata la Escrow.
Akitoa taarifa
ya kikao cha Kamati Kuu ya CCM kilichofanyika Ikulu Dar es Salaam jana, Katibu
wa Itikadi na Uenezi wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, Nape Nnauye
alisema hatua hiyo imefikiwa baada ya Kamati ya Maadili inayoongozwa na Makamu
Mwenyekiti wa Chama hicho (Bara), Philip Mangula kuwahoji vigogo hao.
Alisema Kamati
hiyo ya Maadili iliwasilisha ripoti yake kwa Kamati Kuu jana, ndipo ukafikiwa
uamuzi wa vigogo hao kusimamishwa kuhudhuria vikao vya chama vya Kamati Kuu na
Halmashauri Kuu kwa Profesa Tibaijuka na Halmashauri Kuu kwa Chenge na Ngeleja.
"Uamuzi wa
Kamati Kuu ni kuwasimamisha uongozi wao kwenye vikao vya chama, kwamba
wasihudhurie vikao vya chama vya Kamati Kuu kwa yule mjumbe wa Kamati Kuu na
Halmashauri Kuu kwa wajumbe wake, kwa kipindi ambacho Kamati hii ndogo ya Maadili
wakiendelea kupitia nyaraka mbalimbali zinazohusu suala hili," alisema
Nape.
Akizungumzia vigogo sita wa chama hicho
waliokuwa kwenye adhabu baada ya kuthibitika kukiuka maadili ya Chama na kuanza
kampeni mapema, Nape alisema tathimini ya mwenendo wao bado inaendelea.
Vigogo hao ambao tathimini ya mwenendo wao bado
inaendelea, ni pamoja na waliokuwa mawaziri wakuu, Edward Lowassa na Frederick
Sumaye na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe.
Wengine ni Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi
na Teknolojia, January Makamba, ambaye ameshatangaza nia ya kugombea urais,
Waziri wa Kilimo na Ushirika, Stephen Wasira na Mbunge wa Sengerema, William
Ngeleja.
Alisema kanuni za usalama na maadili ya chama
iliyotumika kuwahukumu, ni inayosema onyo kali alilopewa mwanachama, maana yake
atakaa chini ya uangalizi kwa kipindi kisichopungua miezi 12.
"Sasa baada ya ile miezi 12 kuisha, kamati
ndogo ya maadili inaendelea na kazi yake ya kuchunguza mienendo ya hao
waliokuwa wamepewa adhabu, katika kipindi chao cha adhabu ya miezi 12
wametekeleza masharti ya adhabu zao," alisema.
Alisema baada ya hapo, kamati hiyo itawasilisha
ripoti ya uchunguzi wake kwa Kamati Kuu ambapo kama kutakuwa na taarifa yoyote,
itatolewa kwa umma.
Aidha, Nape alitumia fursa hiyo kuwaonya baadhi
ya wanasiasa wengine waliojitokeza na kutangaza nia zao za kugombea urais kwa
kuvunja sheria na taratibu za chama hicho, wasije kukilaumu chama hicho.
"Kila mmoja ambaye atavunja kanuni katika
mchakato mzima wa kutafuta kuteuliwa na Chama Cha Mapinduzi, atachukuliwa
hatua, hakuna atakayepona katika mkono wa sheria na taratibu za chama kama
atazivunja, ni suala la muda kama kuna mtu anaendelea kuvunja.
“Msisitizo wa Kamati Kuu ni kwamba watu wote
wanaotaka uteuzi wa chama, wafuate taratibu ili tusije tukalaumiana baadae, kwa
sababu wakati mwingine wanadhani ni suala la Nape au Katibu Mkuu kuwa mkali,
hii ni kanuni, hakuna atayepona.
“Hili suala la watu sita lilianza muda mrefu,
lakini yapo maneno wako na wengine wanavunja sheria na taratibu lakini, msimamo
wa chama hiki hakuna atakayevunja sheria akaachwa salama," alisema.
No comments:
Post a Comment