Ni huzuni kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Jeshi
la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Jimbo la Mbinga Magharibi, Taifa,
marafiki na familia, baada ya kufikwa na msiba mkubwa wa kiongozi, Mbunge,
Kapteni wa Jeshi, Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) na msanii mashuhuri
wa Bendi ya Tanzania One Theatre (TOT), Kapteni John Komba.
Msiba huo ulitokea jana wakati Kamati Kuu ya
CCM, ikiwa katika kikao cha kawaida, kilichokuwa na ajenda muhimu, ikiwemo ya kujadili
makada sita waliokuwa wakitumikia adhabu, baada ya kukiuka maadili ya chama na
kuanza kampeni za urais mapema.
Mbali na makada hao, kikao hicho pia kilikuwa na
ajenda ya kujadili makada wengine watatu, waliokuwa wakikabiliwa na kashfa ya
kupokea fedha zilizokuwa katika iliyokuwa akaunti ya Tegeta Escrow, iliyokuwa
Benki Kuu (BoT).
Lakini kabla hata uamuzi wa kikao hicho
kutangazwa, Kapteni Komba aliaga dunia na taarifa za awali zilieleza kuwa
alikuwa nyumbani kwake Mbezi Beach, akajisikia vibaya na kukimbizwa katika
Hospitali ya TMJ, Mikocheni Dar es Salaam, ambako aliaga dunia wakati akipata
huduma.
Taarifa zilizotufikia zilieleza kuwa mtoto wa
marehemu, Jerry Komba, alisema kifo cha baba yake kilisababishwa na kushuka
ghafla kwa sukari.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, Kapteni Komba
alikimbizwa katika Hospitali ya TMJ Mikocheni ambako alifariki dunia.
Baada yakifo hicho, taarifa kutoka kwa Katibu
wake, Gasper Tumaini, zilieleza kuwa mwili wa Kapteni Komba ulipelekwa katika
Hospitali ya JWTZ ya Lugalo, ambako umehifadhiwa ukisubiri taratibu za mazishi.
Muda mfupi baadaye, Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania na Mwenyekiti wa CCM, Jakaya Kikwete alituma salamu za rambirambi
kwa Spika wa Bunge, Anne Makinda na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana.
Katika salamu hizo, Rais Kikwete alisema
amepokea kwa mshituko mkubwa na huzuni nyingi taarifa za kifo cha ghafla cha
Kapteni Komba, Mbunge, Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM (NEC) na
msanii hodari wa kizazi chake.
“Nimepokea kwa mshituko mkubwa na huzuni nyingi
taarifa za kifo cha ghafla cha Mheshimiwa Kapteni John Komba, ambacho
nimejulishwa kuwa kimetokea mchana wa leo (jana), Jumamosi, Februari 28, 2015,
kwenye Hospitali ya TMJ, Dar es Salaam.
“Kwa hakika, sina maneno ya kutosha kuelezea kwa
ufasaha hasara ambayo Taifa letu na Chama chetu kimepata kutokana na kifo cha
Kapteni Komba.
“Taifa letu limepoteza hazina kubwa na mtu
muhimu. Nimemjua Kapteni Komba kwa muda mrefu sana, nimefanya naye kazi.
Alikuwa msanii ambaye kiwango chake cha usanii kilikuwa hakipimiki, alikuwa na
sifa kubwa za uongozi, alikuwa mpenzi, mzalendo na mtu mwaminifu sana kwa taifa
lake na katika jambo lolote aliloliamini,” amesema Rais Kikwete katika salamu
hizo na kuongeza:
“Akiwa mwalimu, lakini hasa akiwa mlinzi wa
Taifa katika Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Kapteni Komba
alithibitisha sifa zake za mlinzi wa Taifa, kwa kipaji chake cha kutunga na
kuimba nyingi za kuhamasisha wanajeshi wetu katika ulinzi wa nchi yao.
“Alikuwa na uwezo mkubwa wa kisanii kutunga
nyimbo za aina zote ziwe za maombolezo,
za kutoa hamasa, za makaribisho, ziwe za kampeni za kisiasa na kijamii ama ziwe
za kampeni maalumu.
“Mheshimiwa Komba alikuwa Mbunge hodari sana na
wananchi wa Nyasa wamepoteza mtetezi wa uhakika. Mheshimiwa Komba alikuwa
mcheshi, aliyependa sana utani na alikuwa na uongozi mkubwa wa kutambua na
kulea vipaji vya sanaa na wasanii, kama alivyothibitisha katika kuanzisha na
kulea kikundi cha Tanzania One Theatre (TOT) na kabla ya hapo.
“Kupitia kwenu waheshimiwa, naomba mnifikishie
salamu zangu za dhati kabisa kwa wabunge wote ambao wameondokewa na mwenzao na
wananchi wa Jimbo la Nyasa na Mkoa wote wa Ruvuma, ambao wamepoteza mwakilishi
na kiongozi wao.
“Ndani ya chama chetu, naomba salamu zangu
ziwafikie wanachama wetu wote kwa kupoteza mwanachama mwenzao, ziwafikie
viongozi na hasa wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), ambayo imepoteza
mwakilishi mwenzao na wasanii wote wa Tanzania One Theatre (TOT) ambao Kiongozi
wao ameondoka duniani,” alisema Rais.
“Naungana na wanafamilia kuomboleza kifo cha
rafiki yetu, ndugu yetu na kiongozi mwenzetu. Napenda wanafamilia wajue kuwa
natambua uchungu wao katika kipindi hiki na tahayari yao ya kuondokewa na mhimili wa familia.
“Niko nao katika maombolezo na katika kumwomba
Mwenyezi Mungu aiweke peponi roho ya marehemu Kapteni John Damian Komba.
Amina,” alimaliza Rais Kikwete.
Akizungumzia kifo cha Kapteni Komba, Katibu wa
Itikadi na Uenezi wa Halmashauri Kuu (NEC), Nape Nnauye alisema, kifo hicho
kimeleta mshituko mkubwa katika chama hicho na ni pigo kwao.
"Kamati Kuu ya Chama Cha Mapinduzi,
imepokea kwa mshituko mkubwa taarifa za kifo cha Mjumbe wa Halmashauri Kuu, msanii
wetu na kada wa siku nyingi na tegemeo kubwa kwa Chama Cha Mapinduzi,” alisema.
Alimkariri Mwenyekiti wa chama hicho, Rais
Kikwete alipowaambia kuwa “kifo hicho ni pengo kubwa kwa chama hicho na gumu
kuzibika hasa kwa wakati huu wa kuelekea katika Uchaguzi Mkuu”.
Alisema wimbo ambao aliutunga katika sherehe za
miaka 38 ya chama hicho, uliwasisimua wengi na pengine msisimko huo ulikuwa ni
namna ya kuwaaga Watanzania na wanachama wa CCM.
Nape alitoa
pole kwa familia ya Kapteni Komba na wanachama kwa ujumla, ambapo alisema Komba
ataendelea kubaki katika historia iliyotukuka ya chama hicho.
Miongoni mwa waliotuma rambirambi kupitia
ukurasa wake wa Facebook, ni Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Tanzania Bara, Mwigulu
Nchemba.
“Natoa pole sana kwa Wananchi wa Mbinga, WanaCCM
na Watanzania wote kwa Msiba Mzito uliotokea wa kifo cha Mpendwa wetu Mh.
Kapt.John Komba na Mjumbe wa Halmashauri Kuu CCM Taifa. Pumzika kwa Amani,”
aliandika katika ukurasa wake.
Taarifa zingine zilizotufikia, zilieleza kuwa
jana mchana, muda mfupi kabla ya kufikwa na mauti, alifanya kazi ya mwisho ya
kutumikia jimbo lake.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, Kapteni Komba
alikwenda katika viwanda vya bati na chuma vya MMI Steel Industries vilivyoko
Mikocheni, akalipia mzigo wa mabati unaofikia lori mbili, kwa ajili ya kupeleka
jimboni kwake Mbinga.
Inadaiwa baada ya kulipa, aliacha maagizo kwa
Keshia kiwandani hapo aitwae Jastin, kuwa madereva watakuja kuubeba mzigo huo
na yeye anakwenda kupima sukari na shinikizo
la damu katika Hospitali ya TMJ.
No comments:
Post a Comment