MWANAFUNZI AHUSISHWA KUUA MWANAJESHI AMBONI


Wakazi 10 wa jijini hapa, akiwemo mwanafunzi wa sekondari wamefikishwa mbele ya Mahakama ya Hakimu Mkazi wakikabiliwa na makosa matano tofauti kuhusu tukio la kuwanyang’anya polisi silaha pamoja na kumuua  askari wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi Tanzania (JWTZ), Sajenti Mohamed Rashid Kajembe.

Mwanafunzi aliyefikishwa mahakamani ni Rajab Bakari (19) ambaye ni mwanafunzi wa shule ya sekondari na mkazi wa Makorora jijini hapa.
Watuhumiwa tisa wameelezwa kuwa ni wafanyabiashara, nao ni Mbega Seif (25) maarufu 'Abuu Rajab' mkazi wa Kiomoni, Amboni, Ayubu Ramadhani (27) maarufu 'Chiti' ambaye ni fundi umeme na mkazi wa Kona Z Kiomoni, Hassani Mbogo (20) maarufu 'Mpalestina' mkazi wa  Makorora, Mohamed Ramadhani (19) mfanyabiashara na mkazi wa Makorora, Sadiki Mdoe (25) maarufu 'Kizota au Kisaka' mkazi Magaoni.
Washtakiwa wengine ni Saidi Omari (26)  mkazi wa  Magaoni Tairi Tatu, Nurdin Mbogo (27) Makorora, Ramadhan Mohamed (18) mkazi wa  Donge pamoja na Omari Harubu Abdala (55) maarufu 'Ami' mkazi wa Dunia Hoteli Makorora.
Wakisomewa mashtaka yao mbele ya Hakimu Mkazi Aziza Rutala, Wakili wa Serikali, George Barasa akisaidiana na MariaClara Mtengule, walidai kuwa kosa la kwanza hadi la tatu linawahusisha washitakiwa namba moja mpaka nane (1 -8) ambao wanatuhumiwa kushiriki  kula njama ya kutenda kosa kinyume cha sheria.
Barasa alidai kuwa katika maeneo tofauti ya jijini Tanga kati ya Septemba mosi 2014  hadi Januari 26 mwaka huu, washitakiwa wote wanane kwa pamoja walitenda kosa la kula njama na kufanya kosa la unyang’anyi wa silaha.
Katika kosa la pili, Barasa  alidai mahakamani hapo kwamba mnamo Januari 26 mwaka huu, katika mgahawa wa Jamali ulipo kati ya barabara ya Nne na ya Tano jijini Tanga, washitakiwa wote wanane waliiba silaha moja aina ya SMG  namba za usajili 14303545 mali ya  Polisi na muda mfupi kabla ya kutenda kosa hilo walitumia visu kumchoma askari H 501 Mwalimu ili kupata silaha hiyo.
Kosa la tatu la washitakiwa hao ni unyang’anyi wa kutumia silaha, na washitakiwa wote wanane wanadaiwa kuwa  katika mgahawa wa Jamali uliopo kati ya barabara ya nne na ya tano waliiba silaha nyingine yenye namba za usajili 14301230 SMG mali ya  polisi na kwamba muda mfupi kabla ya kutenda kosa hilo walimtishia kwa kutumia nguvu kumnyang’anya silaha PC H Mansoor kinyume na sheria.
Hata hivyo, katika kosa la nne ambalo limemhusisha mshitakiwa namba tisa Nurdin Mbogo wakili huyo wa Serikali, alidai kuwa Februari 6 mwaka huu, katika sehemu isiyofahamika jijini Tanga, mshtakiwa huyo akijua kuwa Hassan Mbogo (Mshitakiwa Na. 4) alitenda kosa Septemba mosi 2014 na Januari 26 mwaka huu alimsaidia kumwezesha kukwepa kushtakiwa na kuadhibiwa kinyume na sheria.
Katika hatua nyingine, Wakili wa Serikali Mtengule alisoma shitaka jingine jipya
ambalo liliwahusisha watuhumiwa watatu akiwemo namba 1 na 2 (Mbega Rajabu na Rajabu Bakari) pamoja na mshtakiwa mwingine Omari Harub Abdallah 'Ami' wakidaiwa kwa pamoja kuhusika  kumuua askari wa JWTZ, Sajenti Mohamed Rashid Kajembe mnamo Februari 13 mwaka huu  katika Mapango ya Amboni Jijini Tanga kinyume cha sheria namba 196 na 197 ya makosa ya adhabu ya mwaka 2002 .
Washtakiwa hao watatu hawakutakiwa kujibu lolote kutokana na mahakama hiyo kutokuwa na uwezo wa kusikiliza kesi hiyo ya mauaji.
Hata hivyo, washitakiwa wote 10  kwa pamoja wamekana makosa yao, na mahakama imewanyima dhamana washitakiwa tisa kutokana na makosa waliyotenda kutokuwa na  dhamana.
Mshitakiwa namba tisa Nurdin Mbogo alishindwa kutimiza masharti ya dhamana baada ya kutakiwa kutoa Sh milioni moja na mdhamini mmoja mwenye mali isiyohamishika yenye thamani ya Sh milioni moja.
Washitakiwa wote wamerudishwa rumande hadi kesi hiyo itakapotajwa tena Machi 23 mwaka huu kwa kuwa upelelezi wake haujakamilika.
Mnamo Februari 13 mwaka huu katika eneo la Amboni Jijini Tanga palizuka mapigano baina ya askari polisi wakishirikiana na JWTZ dhidi ya watu wanaodaiwa kuwa ni majambazi, waliokuwa wamejificha kwenye mapango ya Majimoto.
Katika tafrani hiyo, kulisababish kifo cha askari wa JWTZ na majeruhi watano wakiwemo wanajeshi wawili na Polisi watatu, hali iliyozua hamaki kwa wakazi wa jijini hapa.
Rais Jakaya Kikwete katika hotuba yake mwezi uliopita alielezea matukio hayo kuwa ni ya ujambazi, lakini pia yana mwelekeo wa ugaidi na akalitaka jeshi la polisi  kuwasaka watuhumiwa wote na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria.

No comments: