MAWAKILI WA SHEKHE PONDA WAIBUA MAPYA

Upande wa utetezi katika kesi ya jinai inayomkabili kiongozi wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu nchini, Shehe  Ponda Issa Ponda umewasilisha hoja zitakazoifanya mahakama kutoona sababu kwa mshitakiwa huyo kuwa na kesi ya kujitetea.

Mawasilisho hayo yalifanywa mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mkoa wa Morogoro, Mary Moyo kwa zaidi ya saa tatu na mawakili Juma Nassoro na Abubakar Salim, wanaomtetea Ponda.
Akitoa mawasilisho hayo, Wakili Nasoro alidai kuwa ushahidi uliotolewa na upande wa mashtaka pamoja na vielelezo vilivyotolewa mahakamani hapo, unatia shaka na una udhaifu mkubwa, unaomfanya mshitakiwa akose kesi ya kujibu.
Alidai pia hati ya mashtaka yenye makosa matatu, inaonekana kuwa na mapungufu hasa katika shtaka la kwanza, kwani imeshindwa kueleza ni kwa namna gani mshtakiwa huyo alikiuka amri ya mahakama, kama alivyoshitakiwa katika hati hiyo.
Alidai kuwa licha ya kushtakiwa kwa kosa la kutotii amri halali ya mahakama, iliyotokana na hukumu, upande wa mashtaka ulishindwa kuwasilisha hukumu hiyo kama sehemu ya ushahidi.
Wakili huyo alidai kuwa hukumu iliyotolewa Mahakama ya Kisutu dhidi ya Ponda, haina amri yoyote inayoonesha kuwa imetengeneza kosa kwa Shehe Ponda, bali inaweza kuwa ni kukiuka masharti, ambayo sio kosa la jinai.
Baada ya mawasilisho hayo, upande wa mashtaka uliiomba muda mahakama kujibu hoja zilizokuwemo kwenye mawasilisho hayo. Mahakama iliridhia ombi hilo na kuahirisha kesi hiyo hadi Machi 20, mwaka huu na hivyo mshtakiwa kurudishwa rumande chini ya ulinzi mkali wa polisi.

No comments: