KILA MTANZANIA KUPATIWA KITAMBULISHO CHA URAIA


Serikali imeahidi kumpatia kila Mtanzania kitambulisho cha uraia mwaka huu.

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Pereira Ame Silima alisema hayo mjini Dar es Salaam wakati alipokuwa akifungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA).
Alisema Serikali ya Rais Jakaya Kikwete itaendelea kusaidia NIDA ili kufikia malengo ya serikali ya Awamu ya Nne ya kila Mtanzania kuwa amesajiliwa na kupata kitambulisho chake.
Akimkaribisha mgeni rasmi, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa, Dickson Maimu, alisema mpaka sasa NIDA imepiga hatua kubwa katika suala la Usajili na Utambuzi wa watu na ugawaji wa vitambulisho vya taifa.
Mpaka sasa NIDA imefanikiwa kusajili wananchi milioni 6.1, ambapo kati ya hao, wananchi milioni 2.8 tayari wameshakamilisha hatua za usajili kwa maana ya kuchukuliwa alama za kibayolojia kwa Zanzibar na Bara. Jumla ya vitambulisho milioni 1.7 vimezalishwa na kugawanywa kwa wananchi. 
NIDA tayari imekamilisha usajili wa awali Tanzania Zanzibar, mkoa wa Dar es Salaam, Pwani, Lindi, Mtwara, Morogoro na Tanga.
Akielezea changamoto kubwa ya sasa inayoikabili Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa, Maimu alieleza changamoto kubwa kuwa ni rasilimali fedha na rasilimali watu na hivyo kuzorotesha utendaji  na mikakati ya kuendelea na Usajili katika mikoa ya Tanzania.
"Mipango wa sasa ni kuanza rasmi kwa matumizi ya vitambulisho vya taifa, na tayari vikao na wadau wanufaika vimeshafanyika kwa Bara na Visiwani na muda si mrefu Vitambulisho vitaanza kutumika kama nyaraka rasmi ya utambulisho," alisema.
Akizungumza na wafanyakazi hao, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Pereira ameahidi serikali kupitia Wizara yake kuendelea kuongezea nguvu Mamlaka kufikia malengo iliyojiwekea.

No comments: