HATIMAYE ZITTO ALITEMA JIMBO LAKE, AJIPANGA KWA MAJUKUMU MAZITO


Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe amewaaga rasmi wananchi wa jimbo hilo huku akiwataka wananchi hao kutosononeka kwa uamuzi wake wa kutoendelea kugombea ubunge wa jimbo hilo, bali wamwombee na kumuunga mkono katika kila uamuzi atakaouchukua.

Zitto aliwaaga wananchi hao kupitia mkutano wa hadhara mjini Kigoma uliorushwa moja kwa moja na Kituo cha Radio cha Clouds, ambapo alisema, kipindi cha miaka 10 kinatosha kwa yeye kuwa mbunge wa jimbo hilo hivyo kwa sasa ni vyema kijiti akapewa mtu mwingine, ili yeye aweze kusonga mbele katika kuwatumikia Watanzania kwa nafasi kubwa zaidi.
Hatuwezi kuanika kusudio lake la kuwatumikia Watanzania katika nafasi kubwa zaidi, ingawa alidokeza anaweza kuzungumza jambo wakati wowote wiki ijayo.
Alisema amezungumza na wazee wa mkoa huo pamoja na viongozi wa vijiji 45 ambao wamempa baraka juu ya uamuzi wake huo aliochukua, huku akiwataka wananchi hao kukubaliana na baraka hizo alizopewa na wazee.
"Nawaomba kwa sasa mniruhusu nikafanye mambo mengine ili nipishe mtu mwingine ashike hiki kijiti ili tukimbizane, sina maana sitaendelea kukemea mabaya, nitaendelea kukemea, lakini kwa njia nyingine," alisema Zitto.
Alisema hata baada ya uchaguzi mkuu wa Oktoba, mwaka huu ataendelea kukemea mambo mbalimbali ambayo ataona yanalipeleka taifa pabaya, kwa kuwa anapenda kuona Tanzania inasonga mbele.
"Mimi bado Mbunge wenu na nitaendelea hadi hapo watakaposema basi inatosha, ninachowaomba msisononeke, kwani hakuna kiongozi mahiri wa kisiasa asiyepitia kwenye misukosuko.
“Na hata dhahabu haiwezi kuwa dhahabu kama haijapitia kwenye moto,…ninazidi kuimarika kisiasa, hivyo ninayopitia ni ya kawaida kwa mtu anayeelekea kwenye mafanikio," alisema Zitto aliyetumia nafasi hiyo kuwashukuru wanaKigoma kwa kumwamini na kumpa nafasi ya kuwatumikia tangu mwaka 2005 alipokuwa na umri wa miaka 29.
Alisema kwa kipindi chote cha ubunge wake, licha ya kupitia katika milima na mabonde ya kisiasa, anajivunia mambo mbalimbali aliyoyafanya ya kulisaidia taifa ikiwemo kupambana na ufisadi, kwa kuibukia kashfa mbalimbali kupitia Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) anayoiongoza.
Aliwataka wananchi hao kujivunia kuwa na mbunge kama yeye kwa kuwa kwa kipindi chote amekuwa akiwasilisha hoja zenye manufaa kwa taifa, kwani kuna wabunge wengine  tangu wachaguliwe kwa kipindi cha miaka mitano hawajawahi kuleta hoja yoyote.
Aidha, wiki iliyopita Zitto alivuliwa uanachama wa Chadema baada ya Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam kutupilia mbali kesi ya madai aliyofungua dhidi ya chama chake, ambapo kwa mujibu wa katiba ya chama hicho, mwanachama atakayekishtaki chama atakuwa amejivua uanachama mwenyewe.
Mwanasheria wa chama hicho Tundu Lissu alipozungumza na waandishi wa habari alisema, uanachama wa Zitto ulimalizika rasmi baada ya Mahakama Kuu kutupilia mbali zuio la kutaka Kamati Kuu kutojadili uanachama wake.
Zitto ambaye alikuwa Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho, alifungua kesi hiyo dhidi ya Bodi ya Wadhamini ya Chadema na Katibu Mkuu wake, akiiomba Mahakama ikizuie chama kujadili uanachama wake, hadi rufaa anayokusudia kuikata Baraza Kuu la chama kupinga kuvuliwa nyadhifa, itakaposikilizwa.
Hata hivyo, Zitto amekuwa akisema yeye bado ni mbunge halali na mwanachama halali wa chama hicho.

No comments: