CCM YATANGAZA KUWATOSA WALARUSHWA, WAJENGA MAKUNDI


Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana amezitaka kamati za siasa za wilaya na mkoa za chama hicho, kutowapitisha wagombea wa chama hicho wanaotumia rushwa, kujenga makundi ndani ya chama hicho na kuanza kampeni kabla ya wakati.

Amesema hiyo ni siri pekee, itakayokifanya chama hicho kutenda haki na kushinda kwa kishindo katika uchaguzi mkuu ujao wa madiwani, ubunge na urais.
Amesema kwa kutambua hilo, ndio maana Kamati Kuu ya Taifa ya chama hicho,
imewachukulia hatua, wanachama wa chama hicho wanaotaka kugombea urais katika uchaguzi mkuu ujao lakini wakiwa wameanza kufanya kampeni mapema, na hivyo kukiuka kanuni na taratibu za chama hicho katika kuwapata wagombea.
Akiwahutubia mamia wa wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Jimbo la Mpwapwa, Kinana alisema ni dhambi kwa mgombea uongozi wa CCM kutumia makundi, rushwa na kuanza kampeni mapema kama njia ya kumfanya kushawishi kupata uongozi na kusisitiza kuwa viongozi wanaotumia mbinu hizo kamwe hawawezi kuwaletea wananchi maendeleo.
Kinana yupo katika ziara ya kuutembelea mkoa wa Dodoma, aliyoikatisha kufuatia kifo cha Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, Mbunge wa Mbinga Magharibi na Kiongozi wa Kikundi cha Hamasa cha TOT, marehemu John Komba aliyefariki dunia Februari 28, mwaka huu na kuzikwa Machi 3, mkoani Ruvuma.
"Ukiona CCM imeshindwa katika uchaguzi wowote ule wala usihangaike kutafuta
mchawi. Kushindwa kwa mgombea wa CCM mahala popote pale iwe ni Mpwapwa, Biharamulo au penginepo hutokana na sababu za ndani ya chama si nje, na sababu kubwa ni kutokana na kuwepo kwa makundi haramu ndani ya chama.
"Haiwezekani CCM ikashinda kama viongozi wanaohusika na uteuzi hawatendi haki,
anakuwepo mgombea mzuri, anapendwa na watu, wanamheshimu, lakini yupo kiongozi fulani hamtaki, hii ndio chanzo cha migogoro yote inayotokea nchini.Viongozi wa CCM wanakula njama wanasema huyo tusimchague na badala yake wanakuja na jina la mgombea wa hovyo, hana sifa, mlanguzi au mlevi.
"Imefika mahala mtu anapewa uongozi ndani ya CCM kwa sababu ndani ya vikao vya uteuzi kuna ndugu zake, marafiki zake au watu wanaomhusu.Hili suala la uonevu hatutalivumilia mwaka huu, haiwezekani watu wa chini wanafanyiwa uonevu na viongozi wa juu wapo kimya. Ukiona kiongozi huyu anakaa kimya kwa masuala kama haya jua kuna mambo mawili au anapendelea au kapewa rushwa," alisema Kinana.
Kutokana na hilo, Kinana aliwataka wanaCCM kuwa wakali kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka huu huku akisema viongozi wa chama hicho waliochaguliwa katika nafasi
mbalimbali si wafalme bali ni viongozi waliochaguliwa kuwaongoza wanachama wa chama hicho.
Katika kile kinachoonesha kukerwa na tabia hiyo, Kinana aliutaka uongozi wa CCM Mkoa wa Dodoma chini ya Mwenyekiti wake,  Adam Kimbisa, kuwasaka viongozi wote waliowaonea wagombea katika uchaguzi wa nafasi mbalimbali na kuwajadili katika vikao vya Kamati ya Siasa ya Wilaya na Mkoa na wakithibitika waondolewe haraka kwenye nafasi zao.
"Haiwezekani... mtu hafai, hana sifa, ukiulizwa nini? Kanipa pesa, au ni jamaa yangu mwishowe wanaCCM wanapata hasira wanakwenda kumpigia kura mgombea wa upinzani, hilo sasa mwisho wake umefika, tutapambana," alisema Kinana akitolea mfano wa kiongozi wa upinzani katika mji wa Gairo, aliyechaguliwa kutokana na haki kukiukwa kwa mgombea wa CCM.
Akiongeza Katibu Mkuu huyo wa CCM alisema;"Sifa ya kwanza ya Kamati ya Siasa ya Wilaya na Mkoa ni kutenda haki. Nyie mnasikia mnakaa kimya na baadaye mnakuja na visingizio mara ooh lete barua.Tunakwenda kwenye uchaguzi msingi wa kwanza tenda haki ili wanachama waamue mgombea udiwani, ubunge na urais wanayemtaka.
"Wakati wa uchaguzi ni wakati wa ajabu sana, ni wakati ambao mtu mbovu anapewa lundo la sifa na mtu mzuri hapewi sifa zake. Mtu anatoa fedha ili achaguliwe, ni dhambi
kupokea rushwa, mtu ananunua uongozi! Kuna maendeleo hapo? Alihoji Kinana.
Katika hatua nyingine, Kinana amesema ni marufuku kwa kiongozi yoyote wa Kamati ya Siasa ya Wilaya au Mkoa, kubeba jina la mgombea yeyote kuelekea uchaguzi mkuu ujao na kwamba wanatakiwa kuwabeba wagombea wote kwa usawa na kusema kiongozi atakayebainika kufanya hivyo ataondolewa kwenye nafasi yake mara moja.
"Wapo watu ambao tayari wamechukuliwa hatua kali na Kamati Kuu kwa kubainika kufanya kosa hilo ingawa bado hatujawatangaza.Wapo watu tumewapa adhabu, unashangaa kuona kiongozi wa CCM amebeba jina la mtu mmoja tu eti ndiye anafaa kwa ubunge au udiwani au urais, lazima tutende haki hawa tutawapa adhabu," alisema Kinana.

No comments: