CCM YA MWALIMU YAANZA KUREJEA, MATAJIRI KUTUPIWA VIRAGO


Kazi anayofanya Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana katika ziara zake mikoani, sasa ni dhahiri ameanza kurejesha chama hicho katika misingi ya asili yake ya Ujamaa, iliyoasisiwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.

Hilo limejidhihirisha katika kauli na hotuba zake kwa wanachama na wananchi, kwenda kinyume na taswira iliyoanza kujijengea mizizi, kuwa chama hicho kimeanza kuondoka katika misingi ya Ujamaa, iliyojengwa tangu kuasisiwa kwake.
Katika moja ya kauli zake alizotoa jana alipohutubia wakazi wa Mkoka katika wilaya ya Kongwa, akiwa katika ziara ya kutembelea mkoa wa Dodoma, Kinana alisisitiza umuhimu wa uadilifu wa wagombea kwa mtindo uliokuwa ukisisitizwa wakati wa Mwalimu Nyerere.
Kwa mujibu wa Kinana, sifa namba moja inayozingatiwa na wananchi katika kumpata kiongozi wa kuwaongoza, hata kama ni mchapakazi wa kiwango cha juu, uadilifu utasimama kuwa sifa namba moja.
Alisema kutokana na kumomonyoka kwa maadili ya uongozi, tofauti na enzi za utawala wa Mwalimu Nyerere, wananchi sasa hawazingatii suala la uhodari na uchapakazi kama sifa namba moja ya kumchagua mtu kuwa kiongozi wao.
"Wananchi sasa wanaangalia nani muadilifu, nani sio mwizi, nani si mlaji, wapo tayari kukusamehe mambo mengine yote, lakini si suala la uadilifu," alisema Kinana.
Alisema kutokana na kutambua hilo, CCM itakuwa makini na viongozi wake watakuwa wakali, katika kuhakikisha kuwa watu wasio waadilifu wanadhibitiwa wasishike nafasi za uongozi kupitia chama hicho, ili kujenga heshima na imani ya wananchi kwa chama hicho.
Kinana aliweka wazi kuwa moja ya ishara ya  kutetereka kwa uadilifu katika utumishi wa umma, ni tabia iliyoibuka siku za hivi karibuni, ambapo viongozi wanaokiuka misingi ya maadili ya uongozi wa umma, wanapoombwa kukaa kando kutokana na makosa waliyofanya, wanagoma kuondoka madarakani jambo ambalo halikuwepo zamani.
"Siku hizi ukimwambia mtu kaa kando, anakataa au anakwenda kukusanya watu wa kumtetea na kumpigania, watu wanafanya maandamano ya kwenda kutetea watu wasio na maadili ya utumishi wa umma. CCM kuweni wakali katika hili msikubali hata kidogo," alisema Kinana.
Katibu Mkuu huyo pia alielezea kukerwa na hatua ya hivi sasa ya mawaziri, kuandaa sherehe na kuchinja ng'ombe na mbuzi, pale wanapochaguliwa kushika nyadhifa hizo, akisema kitendo hicho kinaonesha mawaziri wa aina hiyo hawatambui uzito wa dhamana wanayopewa.
Amekerwa pia na hatua ya mawaziri hao kutotembelea wananchi vijijini na badala yake wamekuwa wakilundikana kwenye ndege kwenda katika mataifa mbalimbali duniani, kitendo kinachofanya baadhi ya miradi inayotekelezwa chini ya Ilani ya Uchaguzi ya CCM, kutokamilika kwa wakati.
"Siku hizi imeibuka tabia ya ajabu kabisa, mtu anateuliwa kuwa Waziri,  badala ya kusikitika anasherehekea. Pale Wizara ya Nishati na Madini au Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi wameteuliwa mawaziri wangapi na wanaondolewa baadaye?
"Unateuliwa Waziri unafanya sherehe? Unachinja ng'ombe, unachinja mbuzi na unakunywa bia, badala ya kwenda Msikitini au Kanisani kumwomba Mungu akusaidie!" Alihoji.
Alisema viongozi wa aina hiyo wanafanya hivyo bila kufahamu kuwa uelewa wa wananchi wa siku hizi ni mkubwa na wanatambua kila tabia na uwezo wa viongozi wa Serikali.
"Uzuri ni kwamba wananchi wa siku hizi wanatujua, wanajua nani mwongo, wanajua nani anapiga porojo, wanajua nani anajali tumbo lake na wanajua nani mchapakazi kwa hiyo watatuhukumu kwa kile tunachofanya," alisema Kinana.
Juzi Kinana aliunganisha tabia ya ubadhirifu serikalini na uchu wa kupata mali za haraka, pale alipokuwa akikemea matumizi mabaya ya dhana ya utawala bora, ambayo imeonekana kutumika vibaya kutetea wezi.
Alionya wanachama wa CCM kwamba wakilindana na ‘Iyena Iyena’ zao, hawatafika mbali, na kuwataka wawe wakali kwani wanaCCM wengi ni masikini na wachache kama 100 au 20 hivi ndio matajiri. 
Alikumbusha kuwa wanaoiba ndani ya Serikali, wengi wao ni matajiri, ambao ni wachache wanaoishi maisha ya mbinguni, lakini adhabu wanapata masikini wengi wanaoishi duniani na hilo halikubaliki.
"WanaCCM jumla yetu tupo milioni saba, lakini hawa wezi wapo kama 100 au 20, tusiyumbishwe na watu hawa wachache, mimi ni Katibu Mkuu wa Chama cha wakulima
masikini na wafanyakazi masikini, sitakubali kuona chama changu kinageuzwa dampo la walanguzi," alionya Katibu Mkuu huyo wa CCM.
Akizungumza kuhusu adhabu kwa watuhumiwa wa wizi, Kinana alielezea kukerwa na dhana ya utawala bora, ambayo alisema imekuwa ikitumiwa kama kivuli cha kulinda wezi wa mali ya umma, kwa maelezo kuwa ni ngumu kuwafukuza madarakani au kuwaadabisha bila kufuata sheria. 
"Yapo mambo yamewaudhi Watanzania wengi. Kwanza ni suala la wizi serikalini. Eti mtu kaiba halafu sisi tunaanza kupiga maneno mara ooh kaiba au hajaiba? Aondoke, asiondoke?
“Tumwadhibu tusimwadhibu? Ukweli ni kwamba mtu akituhumiwa, tuhuma peke yake inatosha kumfanya aondoke na kama hataki, basi tumuondoe kwa nguvu na si kuleta maneno,” alisema na kuongeza kuwa enzi za Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, dhana hiyo haikupewa nafasi kwa wezi.
"Lazima niseme wazi, Watanzania wametushangaa sana katika hili, mwingine akiiba kuku si sawa… wakubwa serikalini wanasema afungwe, lakini huyu aliyeiba fedha nyingi za umma, tunasema utawala bora!
“Lazima tulikatae hili kwa nguvu zote na mtu wa kwanza anayepaswa kukasirika ni mwanaCCM, kuweni wakali acheni kabisa kulindana," alisema Kinana.
Akionesha wazi kukerwa na hali hiyo, Kinana alisema kinachosikitisha zaidi ni kuona mtendaji ndani ya Serikali anapoiba, wanajitokeza wanaCCM wengine ili kumkingia kifua asichukuliwe hatua, jambo ambalo limekuwa likiwakera Watanzania wengi.
"Mtu ameiba wazi kabisa, wanatokea wanaCCM wenzake utasikia oooh hakujua, ooh tumuonee huruma. Jamani huyu mtu hakujua kwani hana macho kuona anachokifanya ni wizi?
“Naomba wanaCCM simamieni uadilifu, mmechaguliwa na wananchi kutokana na imani yao kwenu na kama tunavyofahamu imani huzaa imani, nataka niahidi CCM tutakuwa wakali sana, ukiiba lazima uondoke.
"Huu utawala bora ni lazima sasa tuutazame kwa macho mawili maana ni kama umeegemea upande mmoja. Mtu anaiba kuku hakuna utawala bora, lakini anaiba mali ya umma, unaambiwa kuna utawala bora! Mwizi dawa yake ni jela si maneno, lazima tujenge utamaduni wa kuwajibishana.
"Lazima tuige wakati wa utawala wa Baba wa Taifa, yeye alisema ukikosea iwe ni sawa na kugusa moto, ukigusa moto adhabu ni palepale, ilikuwa ukibainika tu unastaafishwa kwa manufaa ya umma, lakini sasa unaambiwa utawala bora. Mtu akiiba anahamishwa,” alionya.

No comments: