AZAM FC YAMALIZANA NA MAKOCHA WAKE

Uongozi wa Azam FC umesema umemalizana na makocha wake Joseph Omog (pichani) na Ibrahim Shikanda na wako huru kuondoka muda wowote kwani hawana wanachodai.

Akizungumza na mwandishi, Meneja wa Azam FC, Jemedari Said alisema kwa kawaida wakisitisha mkataba na kocha ama mchezaji humlipa stahiki zake zote.
“Sisi si kama klabu nyingine tunajua majukumu yetu tukimalizana na mtu tunamlipa haki zake zote kisha anaondoka, sasa makocha hawa tumeshawalipa kila kitu ni wao tu wana uamuzi wa kuendelea kubaki nchini ama kuondoka, wako huru hawatudai hatuwadai,” alisema Saidi.
Uongozi wa Azam FC juzi uliwatimua makocha hao kwa kile inachodaiwa ni kuishiwa mbinu za ufundishaji hali inayosababisha timu hiyo kuyumba kwenye michuano mbalimbali.
Azam FC imetupwa nje ya michuano ya Ligi ya Mabingwa kwa jumla ya mabao 3-2 na El Merreikh ya Sudan.
Awali, timu hiyo ilikuwa kwenye nafasi nzuri ya kufuzu baada ya kushinda mabao 2-0 katika mechi ya kwanza iliyofanyika kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, lakini ilifungwa mabao 3-0 katika marudiano Khartoum.
Azam FC inayoshika nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu ikiwa na pointi 27, ipo chini ya Kocha Msaidizi George Nsimbe mpaka itakapopata kocha mwingine.
Omog, ambaye ni raia wa Cameroon, alianza kazi Desemba 2013 akichukua mikoba ya Stewart Hall kutoka Uingereza,  ameiongoza Azam FC katika mechi 55 kwenye michuano yote, akishinda 30, sare mara 14 na kupoteza mechi 11.

No comments: