Baada
ya kushuka kwa bei ya mafuta nchini, wakati wowote kuanzia leo Shirika la Umeme
Nchini (TANESCO) linatarajiwa kutangaza bei mpya za umeme ambazo zitakuwa na
unafuu kwa wananchi.
Kutangazwa
kwa bei hiyo ni agizo la Waziri wa Nishati na Madini, George Simbachawene la
kuwataka kuangalia uwezekano wa kushusha gharama za umeme ili kushuka kwa
mafuta kuwaguse moja kwa moja wananchi wa kawaida.
Aidha,
Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra) nayo imetakiwa
kuangalia namna itakavyoweza kushusha bei za nauli ili kushuka kwa gharama za
mafuta, kuendane sambamba na kuwagusa wananchi.
Simbachawene
alitoa kauli hiyo jijini Dar es Salaam, baada ya mkutano wa pamoja kati ya
wadau na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) na wizara
hiyo.
Alisema,
ingawa matumizi ya mafuta katika kuzalisha umeme yamepungua, lakini kwa mitambo
na kiasi kinachotumika katika kuzalisha umeme lazima ionekane kushuka kwa bei
ya umeme.
"Tanesco
waangalie ni kwa kiasi gani gharama za uzalishaji, kwa sababu hizo gharama za
uzalishaji wa umeme ndiyo zinazotumika kupanga bei ya umeme.
”Hivyo
lazima tuoneshe Ewura wanapotangaza zile bei, aidha imepanda basi kiasi kile
ambacho wananchi huwa wanajisikia vibaya sasa wajisikie raha kwamba tunaona
bidhaa hii ya mafuta imeshuka bei, kwa hiyo uzalishaji wa umeme nao unashuka
gharama yake," alisema.
Alisema
ni lazima bei hizo zishuke hata kama ni kwa gharama ndogo kutokana na mitambo
mingi inatumia maji na gesi, lakini kiwango hicho ni lazima kionekane kushuka.
Aidha,
alisema angependa kuona kila shughuli inayogusa nishati ya mafuta ikiwemo
mashine za kusaga zinazotumia nishati hiyo zinashusha gharama zake tofauti na
hapo wananchi hawataona kushuka huko na lawama zitaelekezwa kwa serikali.
Akizungumzia
kuhusu suala la usafiri, aliiomba Sumatra iweze kuchukua hatua za haraka za
kutangaza bei mpya za nauli ambazo zitakuwa chini tofauti na ilivyo sasa.
Awali
akijibu maswali na hoja za wadau hao,
Mkurugenzi Mkuu wa Ewura, Felix Ngamlagosi alisema kusimamishwa kwa ufuatiliaji
wa uchakachuaji na wanaokwepa kodi kwa umwagaji wa mafuta ya nje nchini, itarudisha hali ya miaka ya nyuma,
ambapo alisema ni vyema mradi huo ukaendelea kutokana na kuisaidia serikali
kukusanya mapato mengi.
Mkutano
huo ulikuwa unalenga kujadiliana masuala mbalimbali yanayohusu sekta hiyo,
ikiwemo changamoto wanazokumbana nazo.
Tangu
kuanza kwa mwaka huu, bei ya bidhaa za petroli zimekuwa zikishuka bei kutokana
na kushuka kwa bei katika soko la dunia. Tayari unafuu umeanza kuonekana kwa
watumiaji wa petroli, dizeli na mafuta ya taa, bidhaa ambazo kwa muda mrefu
zimekuwa zikiuzwa kwa bei ya juu ya Sh 2000, lakini sasa zimeshuka na kuwa
chini ya Sh 1,800.
Kutokana
na hali hiyo, wadau wamekuwa wakihimiza kuangaliwa kwa uwezekano wa nafuu hiyo
ya bei kugusa pia maisha ya kila siku ya mwananchi, ikiwa ni pamoja na
kupunguza nauli katika vyombo vya usafiri.
No comments:
Post a Comment