Baadhi ya watendaji wa Taasisi ya Kupambana na
Kuzuia Rushwa (Takukuru), pamoja na Mamlaka ya Mapato nchini (TRA), ni miongoni
mwa watendaji wa taasisi nne ambao wametajwa katika utafiti kuwa wamekithiri
kwa kupokea rushwa.
Takukuru na TRA zimetajwa kuwa na kadhia hiyo katika ripoti ya Taasisi
ya Afro Barometer iliyofanywa kwa kushirikiana na Taasisi ya Kupunguza
Umasikini (Repoa).
Kwenye ripoti hiyo, Polisi bado wanaongoza kwa kupokea
rushwa wakifuatiwa na TRA, Mahakama na Takukuru inashika nafasi ya nne, jambo
ambalo limewashitua watu wengi waliohudhuria kwenye mkutano huo.
Akiwasilisha ripoti hiyo jana jijini Dar es Salaam mbele ya wadau
mbalimbali, mtafiti wa Repoa, Rose Aiko alisema maofisa wa serikali za mitaa,
maofisa serikalini na baadhi ya wabunge na wananchi wamewataja kuwa wanashiriki
kwenye vitendo vya rushwa.
Ripoti hiyo imeeleza kuwa asilimia 67 ya watu waliohojiwa ambao ni 2,386
walikiri kuwa vitendo vya rushwa vimeongezeka kuanzia mwaka 2013 hadi 2014;
licha ya juhudi zinazofanywa na Serikali za kuajiri maofisa wengi wa kupambana
na rushwa katika taasisi ya Takukuru.
“Habari kwamba rushwa imeongezeka, imeongelewa na watu wa kawaida
mijini, wanaume, wasomi na wakazi wengi wa Zanzibar,” ilieleza ripoti hiyo.
Miongoni mwa walihojiwa, asilimia 50 waliitaja polisi kukithiri kwa
rushwa, TRA (asilimia 37), Mahakama asilimia 36, Takukuru asilimia 29 wakati
maofisa wa Serikali za mitaa ni asilimia 25.
Hata hivyo, utafiti huo umebaini kuwa miongoni mwa watu watatu ambao
wanaenda kupata huduma Polisi na mahakamani, mmoja kati ya watu hao anadaiwa
rushwa.
Mtazamo wa wananchi ambao ni asilimia 53, wanaona kwamba wananchi wa
kawaida wanaweza kusaidia katika mapambano ya rushwa, huku asilimia 33 wakisema
wananchi wa kawaida hawawezi. Pia utafiti huo ulibaini kuwa wananchi wengi hawatoi taarifa
kwa mamlaka husika hata pale wanapodaiwa rushwa.
Watu wanane kati ya 10 ambao walihojiwa ambao tayari walishatoa rushwa,
walikiri kuwa hawakutoa taarifa mahali popote licha ya kutoa rushwa.
Pia utafiti huo ulibaini kuwa asilimia 34 ya wahojiwa, walitoa rushwa
wakati wanatafuta haki mahakamani na wengine asilimia 34 walitoa rushwa kwa
kuepuka usumbufu wa Polisi.
Pia utafiti huo wa Repoa ulisisitiza kuwa, ili jamii iondokane na tatizo
la rushwa, ni lazima watu wakatae kutoa rushwa na wengine wawaripoti kwenye
mamlaka zinazohusika wale wote ambao wanawaomba rushwa.
Sababu ya watu kutoripoti matukio ya rushwa kwenye mamlaka zinazohusika,
utafiti uliainisha kuwa ni mazingira magumu ya upatikanaji wa ushahidi kwa kuwa
watuhumiwa wengi wamekuwa rahisi kukataa kuhusika na vitendo vya rushwa.
Pia mamlaka zinazohusika na kupambana na rushwa, zimetajwa kuwa ziko
mbali, jambo ambalo linawafanya wengi wanaokutwa na janga la kuombwa rushwa,
wasiripoti kwa kuepuka gharama za kwenda huko.
Pia utafiti huo ulibaini kuwa watu wanaamini bila kutoa rushwa, hawawezi
kupata huduma na kwamba mtu ambaye amekusaidia baada ya kupewa rushwa sio
vizuri kumripoti Takukuru.
“Kubwa hapa ni kwamba jamii haina uelewa wa kutosha kwa maana mtu
anaamini kwamba hawezi kupata huduma wakati mwingine atakapokuwa na shida iwapo
ataripoti tukio la rushwa Takukuru au Polisi,” alisema Rose.
Hata hivyo, wananchi wengi walipongeza vyombo ya habari kwa kuwa mstari
wa mbele kutangaza vitendo vya rushwa vinavyofanywa na baadhi ya maofisa wa
Serikali katika taasisi mbalimbali.
Naye Ofisa wa Takukuru, Mary Mosha alipochangia kuhusu ripoti hiyo,
alisema Takukuru imekuwa na mpango mkakati uliowahusisha wadau mbalimbali wa namna ya
kuielimisha jamii ielewe juu ya madhara ya rushwa.
Alisema pia kuwa juhudi nyingi zimefanywa na Serikali kuziba mianya ya
rushwa; “Bahati mbaya ni kwamba juhudi hazionekani na watu wanataka kuona watu
wanapelekwa mahakamani.
Mosha aliwataka wadau wote kuendelea kushirikiana na Takukuru kupambana
na rushwa na akasisitiza kuwa kuna mabadiliko miongoni mwajamii.
“Ila tu matukio kama haya ya Escrow wakati mwingine ndio yameifanya
jamii ione kuwa tatizo hili bado ni kubwa,” alisema. Mkurugenzi wa Masuala ya
Uchumi wa Repoa, Dk Donald Mmari alisema kuitaja Takukuru ni kuwapa fursa
viongozi wa taasisi hiyo kumulika watu wake ili taasisi hiyo isije ikapoteza
imani miongoni mwa wananchi.
“Sisi ndio maana tumemwita hapa ofisa wa Takukuru na kuitaja kwenye
utafiti sio jambo baya, tunataka kumwonesha kinachofanywa na watu wa ofisi yake
na wachukue hatua kuanzia sasa,” alisema Mmari.
Lakini Dk Benson Bana, alikuwa na mtazamo tofauti kuwa utafiti huo ni
mzuri lakini kuitaja Takukuru hadharani, kutakatisha watu tamaa.
“Watu wanajenga imani mbaya kwamba mwizi hawezi kumkamta mwizi
mwenzake,” alisema Dk Bana.
No comments:
Post a Comment