Taasisi ya Kuzuia na Kupambana
na Rushwa (Takukuru), imewapandisha mahakamani Mkuu wa Wilaya ya
Mufindi, Evarista Kalalu na wakurugenzi wawili kwa makosa mawili
yanayohusiana na rushwa kinyume na Kifungu cha 32 cha Sheria ya Takukuru Namba
11 ya mwaka 2007.
Katika kesi hiyo
inayowaunganisha maofisa wengine wawili wa halmashauri ya wilaya ya
Mufindi, wanatuhumiwa kuisababishia
halmashauri hasara ya Sh milioni 3.
Kesi hiyo iliyopewa jina la
kesi ya uhujumu uchumi namba moja ya mwaka 2015,
ilifunguliwa jana katika
Mahakama ya Wilaya ya Mufindi mkoani hapa.
Mkuu wa wilaya hiyo na
watuhumiwa hao wengine kwa pamoja wamekana mashitaka yao mbele ya Hakimu
Mfawidhi wa mahakama hiyo, Victoria Nongwa.
Watuhumiwa wengine katika
shitaka hilo ni Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mikindani mkoani
Mtwara, Limbakisye Shimwela ambaye wakati kosa hilo likitendeka kati ya Desemba
2010 na Februari 2011, alikuwa Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Mufindi
na mwingine ni Mkurugenzi wa halmashauri ya Biharamulo mkoani Kagera,
Nasibu Bakari.
Watuhumiwa wengine
waliofikishwa katika mahakama hiyo, kutokana na ushiriki wao wa makosa
katika kesi hiyo ni Ofisa Mipango wa Halmashauri ya Mufindi, Cosmas Mduda
na Fundi Ujenzi wa wilaya hiyo, Fedrick Zaveri.
Akisoma shitaka
linalowakabili watuhumiwa hao mahakamani hapo, Mwendesha mashitaka wa Takukuru
Mkoa wa Iringa, Imani Mizizi alidai mbele ya Hakimu Mfawidhi wa mahakama
hiyo kuwa kati ya Desemba 2010 na Februari 2011 watuhumiwa hao kwa pamoja
walikula njama ya kutenda kosa la rushwa kinyume na kifungu cha 32 Sheria
ya Kuzuia na Kupambana na rushwa Namba 11 ya mwaka 2007.
Katika kosa la pili,
linalowakabili watuhumiwa watatu katika kesi hiyo, ambao
ni Shimwela ambaye ni
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mtwara/Mikindani, Bakari ambaye ni Mkurugenzi wa
Halmashauri ya Wilaya ya Biharamulo na Cosmas ambaye ni fundi ujenzi, ni lile
la matumizi mabaya ya ofisi kinyume na kifungu cha 31 cha sheria kuzuia na
Kupambana na Rushwa.
Ilidaiwa mahakamani hapo kuwa
kati ya Desemba 2010 na Februari 2011, watuhumiwa hao watatu walitumia
ofisi vibaya kwa kuingia mkataba na Fedrick Zaveri kwa ajili ya ujenzi wa vyoo,
bafu za kuogea na mfumo wa maji katika shule ya sekondari ya Ihalimba bila
kufuata Sheria ya Manunuzi ya Umma ya mwaka 2004.
Ilidaiwa kuwa kutokana na
hatua hiyo, watuhumiwa waliisababishia hasara ya Sh milioni tatu Halmashauri ya
Wilaya ya Mufindi.
Watuhumiwa wote wamekana kosa
na kuachiwa kwa dhamana baada ya kukidhi masharti ya kila mmoja kuwa na
wadhamini wawili na bondi ya Sh milioni
moja kwa kila mdhamini.
Hakimu
Victoria aliahirisha kesi hiyo hadi Machi 13 mwaka huu, watu hao
watakapokuja kusomewa maelezo ya awali.
No comments:
Post a Comment