Serikali imetoa taarifa rasmi kuhusu uhalifu
uliotikisa mkoani Tanga, ikisema hali ni shwari na umma wa Watanzania upuuze
taarifa zinazosambazwa kwenye mitandao ya kijamii zikitia hofu.
Aidha, imesema
watu kadhaa wanashikiliwa wakihusishwa na uhalifu huo.
“Tunawashikilia ila mpaka sasa siwezi
kukueleza idadi yao na kwamba ni wa kikundi cha ugaidi au la. Hao watu
tunafanya nao mahojiano ili kuweza kuelewa kama wanahusika kwenye tukio
hilo,” alisema Kaimu Kamanda wa
Polisi wa Mkoa wa Tanga, Juma Ndaki.
Akitoa taarifa kwa waandishi wa habari, Ndaki
alisema hali katika kitongoji cha Majimoto, Amboni na mkoa wa Tanga kwa ujumla
iko shwari. “Tunaendelea kufanya uchunguzi kubaini hao wahalifu pamoja na
silaha zilizoibwa,” alisema.
“Tunaomba wananchi waendelee kutoa ushirikiano
wao hasa wanapoona watu wenye majeraha au wanaowahisi kwamba ni wahalifu ili
nasi tuweze kuwachunguza kama wanahusika kwenye tukio hili”, alisema.
Ingawa Kamanda hakuelezea mazingira ya
kukamatwa kwa watuhumiwa, waandishi wa habari waliozuru eneo la Amboni yalikotokea mapigano, waliarifiwa kwamba
baadhi ya wavuvi kwenye Mto Zigi, walimkamata mtu wakimtuhumu kukutwa akifua
nguo zenye damu.
Katika mapigano hayo baina ya askari na
wahalifu, yalisababisha kifo cha askari wa JWTZ, Sajenti Said Kajembe na wengine kujeruhiwa.
“Asubuhi wavuvi kadhaa walikuwa hapo mtoni
ghafla walikutana na mtu pembeni ya mto akiwa anafua kanzu pamoja na vifaa
fulani kama nguo za kufunika uso ..’maski’ ikabidi wawapigie haraka polisi simu
lakini hawakuweza kupatikana na ndipo wakawapigia askari wa JWTZ ambao walifika
haraka eneo la tukio na kumkamata mhusika”, alisema mkazi mmojawapo.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Magalula Said Magalula aliwataka wakazi wa
Tanga na vitongoji vyake, kuondoa hofu kwa kuhakikisha wanaendelea na shughuli
zao za uzalishaji kwa sababu ulinzi umeimarishwa na hali ya usalama ni shwari.
Pia, aliwataka wananchi na wageni wenye mpango
wa kutembelea eneo la kihistoria la Mapango ya Amboni, kuendelea na ratiba zao
kwa sababu eneo hilo liko salama na tangu awali halikuhusika kwenye vurugu
hizo.
Magalula ambaye pia alikutana na waandishi wa
habari, alisema “Hali ni nzuri ulinzi na usalama uko imara… naomba wananchi
waondoe hofu, wawe na amani na waendelee na shughuli zao za uzalishaji… hakuna
tatizo kabisa usalama umedhibitiwa vizuri.”
Mkuu huyo wa mkoa ambaye Mwenyekiti wa Kamati
ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa, alisisitiza
“Naomba Watanzania wenzangu muelewe kwamba eneo lilipofanyika tukio la
mapigano na wahalifu si pale yalipo mapango ya Amboni ... maeneo hayo yapo
mbali na nitoe mwito kwa wageni wenye mpango wa kutembelea hapo wawe huru
kufanya hivyo mahali hapo ni salama.”
“Naomba Watanzania nchini kote kwa ujumla wawe
na amani kwa sababu Tanga iko shwari hakuna tena hizo vurugu za wahalifu…
naomba wasiamini sana taarifa zinazosambazwa kwenye mitandao ya kijamii… sisi
tuko shwari na shughuli za kijamii zinaendelea kama kawaida ikiwemo Amboni,”
alisema.
Akizungumzia mapigano hayo yaliyotokea Februari 14,
alisema licha ya majibizano ya kurushiana risasi yaliyofanywa na askari
wa Polisi kwa kushirikiana na wa JWTZ , uchunguzi unaendelea kuwapata wahusika.
“Vikosi vya usalama vinaendelea na juhudi za
kuwasaka pamoja na kutafuta silaha zetu lakini hakuna mtu yeyote anayeshikiliwa
… zipo simulizi mbalimbali zinazoendelezwa kwenye mitandao ya kijamii ila sisi
serikali ya mkoa bado hatujathibitisha kwamba watu hao ni wa kikundi gani ila
ninachokifahamu hao watu ni wahalifu”, alisisitiza.
Kuhusu kuongezeka kwa matukio katika maeneo mbalimbali mkoani humo, alisema kila tukio linachukuliwa kwa uzito
mkubwa na linashughulikiwa kwa namna linavyotokea.
Aidha, amewataka wakazi wa Tanga hususan
wanaoishi eneo la Amboni na vitongoji vyake kuhakikisha wanaendelea kutoa
habari sahihi kuhusu watu mbalimbali wanaowatilia shaka . Alisema taarifa hizo
zina umuhimu wa kipekee kwa askari katika kufanikisha kukamatwa kwa wahalifu
hao.
Kutokana na maswali mengi ya wanahabari na
wananchi, kudai kutoridhishwa na mwenendo
wa utoaji taarifa kuhusu tukio hilo, Mkuu wa Mkoa aliruhusu watembelee
eneo la tukio kuthibitisha kama hali ni
shwari katika eneo husika.
Timu ya wanahabri takribani 10 kutoka vyombo
mbalimbali vya habari, wakiwa chini ya ulinzi wa askari walipelekwa eneo la
tukio, ambalo liko umbali wa takribani kilometa tano kutoka yaliko Mapango ya
kihistoria ya Amboni.
Eneo hilo limetawaliwa na miamba ya mawe
makubwa yenye mapango, ambayo hayatumiki kwa shughuli za kihistoria, kama
ilivyo katika kitongoji cha Kiomoni yalipo mapango ya kihistoria ya Amboni.
Shughuli zinazoonekana kufanyika jirani na
eneo hilo, ni ulipuaji wa miamba kwa kutumia baruti ambao hufanywa na
wachimbaji wadogo kisha kuvunja kokoto
kwa ajili ya viwanda vya kutengeneza chokaa pamoja na mawe kwa shughuli
za ujenzi mjini hapa.
Eneo wanakodaiwa kuishi wahalifu hao, liko umbali wa meta 300 kutoka upande wa pili
zinapofanyika shughuli za upasuaji
kokoto zinazoendeshwa na wakazi wa kitongoji cha Majimoto na Mafuriko
huko Amboni.
Katika eneo hilo, kulikuwa na ukimya kutokana na kutokuwapo
shughuli yoyote hususani uvunjaji kokoto iliyozoeleka kutokana na wananchi
kusimamishwa kutokana na tukio hilo.
Waandishi wa habari walilazimika kufuata
maelekezo yaliyokuwa yakitolewa na wanausalama waliokuwa wakiwaongoza kufika ndani ya pango husika.
Mwonekano wa eneo hilo, ulidhihirisha ni la
hatari kutokana na mapango kufunikwa na vichaka. Ndani ya pango hilo, upo uwazi
mkubwa unaoashiria uwepo wa shughuli za kibinadamu zilizokuwa zikiendelea.
Ndani ya pango hilo, zilikutwa nguo; hususan
suruali, madumu ya kuhifadhia maji, vikombe kadhaa vya plastiki, chupa za maji
ya kunywa zilizotumika hatua ambayo imedhihirisha kuwapo binadamu waliokuwa
wakikaa humo licha ya kwamba, kufika kwake ni kwa shida.
Wakazi wazungumza
Wakizungumza na waandishi, baadhi ya wakazi wa
maeneo jirani na eneo hilo, walisema hawajaruhusiwa kufika eneo hilo kwa kuwa
linaendelea kulindwa na askari wa Polisi
wa kikosi cha kutuliza ghasia (FFU) kwa
kushirikiana na JWTZ.
“Muda mfupi tu kabla ya ninyi kwenda huko,
askari wa FFU walitoka huko , ninyi mnaelezwa kwamba pako shwari lakini sisi
bado hatujaruhusiwa kufika kule kwa sababu panalindwa muda wote na askari… ,”
alisema mkazi aliyejitambulisha kwa jina
moja la Mrisho.
Katika hatua nyingine, askari wa JWTZ
aliyefariki wakati akitibiwa kwenye Hospitali ya Bombo baada ya kujeruhiwa
kwenye mapigano hayo ya mwishoni mwa wiki,
mwili wake uliagwa jana mjini hapa kabla ya kusafirishwa kuelekea
wilayani Korogwe kwa maziko yaliyofanyika katika kijiji cha Bungu.
No comments:
Post a Comment