Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta amemsimamisha
kazi Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Madeni Kipande
kutokana na kile kilichoelezwa kuwa uendeshaji mbovu wa utoaji wa zabuni.
Aidha, amemteua Awadhi Massawe kushika wadhifa
huo. Kabla ya uteuzi huo, Massawe alikuwa Meneja wa Bandari.
Akizungumza na waandishi wa habari, Sitta
alisema uamuzi huo umetokana na kuwapo malalamiko ya kutofuatwa kwa taratibu za
zabuni na ucheleweshaji wa barua kwa wanaoshinda.
“Ni muhimu sana taratibu zetu za ununuzi
katika bandari ziwe wazi na ziheshimike duniani kote, maana miradi hii ni
mikubwa sana inayopitishwa na bodi ya zabuni ya TPA,” alisema.
Sitta alisema,
aliyekuwa Waziri wa Wizara hiyo Dk Harrison Mwakyembe alianza
kushughulikia masuala hayo, lakini hayajakaa vizuri. Alisema hakuna uwazi na
kumekuwa na ubabaishaji mkubwa, ikiwemo kubadilika majina ya kamati za
kutathmini zabuni.
Wakati huo huo
Sitta ameunda timu ya watu sita itakayochunguza tuhuma za Kipande.
Imepewa wiki mbili iwe imefanya kazi hiyo.
Timu hiyo itaongozwa na Jaji mstaafu, Augusta
Bubeshi na Katibu wake, Deogratius Kasinda ambaye ni mtumishi wa Wizara ya
Uchukuzi.
Wajumbe wengine wa timu hiyo ni Mkurugenzi
Mkuu mstaafu wa Mamlaka ya Manunuzi ( PPRA) Dk Ramadhani Mlinga, Samson Lugigo
, Happiness Senkoro na Flavian Kinunda ambao walishawahi kushika nyadhifa za
juu ndani ya TPA.
“Nimejitahidi kuchukua hawa wastaafu kwa sasa
hivi hawatafuti cheo chochote, naamini watatenda haki, watachunguza tu bila
kufanya uonevu,” alisema Sitta.
Waziri Sitta alisema bandari ni eneo muhimu,
kwani takwimu zinaonesha kwamba asilimia 43 ya makusanyo ya Mamlaka ya Mapato
Tanzania (TRA), yanatokana na kodi ya ushuru wa forodha. Kati ya makusanyo
hayo, asilimia 87 yanakusanywa kupitia Bandari ya Dar es Salaam.
Kwa upande wa Kipande, alisema hawezi kupinga hatua iliyochukuliwa
na waziri .
Hata hivyo, alisema anaamini kipindi chote cha
uongozi wake, alifanya ambayo yalikuwa sahihi na hana wasiwasi na uamuzi huo.
"Mimi sina wasiwasi na hilo sababu huo ni
uamuzi wake; lakini nina imani kuwa katika bandari hii, nimefanya kile ambacho
nilikuwa natakiwa kufanya, hivyo sina
shaka na hilo," alisema Kipande.
Katika hatua nyingine, Mwenyekiti wa Kamati ya
Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Kabwe Zitto ametaka serikali
kujenga matangi ya kuhifadhia mafuta na kujenga bomba la mafuta kwenda mikoani.
Aidha, kamati hiyo imetaka TPA kuangalia
uwezekano wa kununua hisa 50 za Kampuni ya Kuhifadhi Mafuta (Tiper) imilikiwe
kwa asilimia 100 na Serikali.
Kuhusu ujenzi wa matangi, Zitto alisema hatua
ya Serikali kujenga matangi yake ya kuhifadhi mafuta, itasaidia kujua kiasi cha
mafuta yanayoingia na kuweza kukadiria kodi kwa uhakika.
Akitoa mfano wa Kenya, alisema Serikali
inamiliki matangi ya kuhifadhia mafuta,
wanayapima kujua kiasi cha mafuta kilichoingia na kukitoza kodi kabla ya kupelekwa kwenye matangi ya
waagizaji.
“ Walichofanya, wamemtaka kila muagizaji kuwa
na flow meter yake na yakitoka kwenye
meli yanaingia kwenye matangi ya Serikali na baada ya kujua kiasi na kutozwa
kodi hupelekwa kwa walionunua,” alisema.
Zitto
alisema wakati umefika sasa kwa serikali kujenga mabomba ya kusafirishia
mafuta na kwa kuanzia yakawa matatu, ambayo yatasaidia kuondoa mfumo wa sasa wa
kusafirisha kwa magari.
“Linaweza kujengwa bomba moja kwenda Mbeya,
likawa na matoleo kwa ajili ya mikoa ya Morogoro, Iringa na mikoa iliyo jirani,
kwa kufanya hivyo tutaondoka na hali ya sasa ya kusafirisha mafuta kwa magari,”
alisema.
Alisema katika kuimarisha reli, ni vyema
ukaanzishwa mfumo wa kutoza kodi asilimia 1.5 kwa kila bidhaa inayoingia nchini
na fedha hizo ziimarishe usafiri wa reli.
“Kwa sasa asilimia 99 ya mizigo inasafirishwa
kwa barabara, hili si jambo jema kwa uchumi, najua nikisema hivyo wenye malori
watalalamika, lakini wanaweza kufanya biashara nyingine,” alisema.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa TPA,
Awadhi Massawe alisema asilimia 60 ya mafuta yanayoingia nchini hupitia kwenye
boya la Single Buoy Mooring (SBM).
Alisema wamejipanga kujenga mita ya kisasa ya
kupimia mafuta maeneo ya Kigamboni huku ile ambayo haitumiki, wamepanga
kuiboresha na kuwa ya kisasa.
Kuhusu maendeleo ya ujenzi wa gati namba 13 na
14 ambazo zabuni yake iliingia utata,
Massawe alisema ripoti ya maandishi wataipeleka kwa Kamati hiyo ya Bunge
ifikapo Machi Mosi mwaka huu.
Pia, Massawe alisema hatua ya kitengo cha
kupakua kontena kupewa mtu binafsi, inawapunguzia mapato na kuwa hiyo ndio
sekta ambayo inaingiza fedha nyingi.
Alisema ili kupambana na hali hiyo,
wamejipanga kuimarisha gati namba 1 hadi 7 na kuongeza kina cha bahari ili
kuweza kupakua makasha na kuwa kwa mwaka jana waliweza kupakua makasha laki
mbili.
No comments:
Post a Comment