KESI YA SHEHE PONDA KUSIKILIZWA TENA FEBRUARI 16



Kesi inayomkabili kiongozi wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu nchini Shehe Ponda Issa Ponda jana imeahirishwa  hadi  Februari 16, mwaka huu kwa mashahidi wa upande wa mashitaka kuendelea kutoa ushahidi  mahakamani.

Tayari mashahidi saba wa upande huo wameshatoa ushahidi wao mbele ya Mahakama ya Hakimu Mkazi ya Mkoa wa Morogoro, akiwemo aliyekuwa Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo, Faustine Shilogile.
Akiongozwa na Wakili  Mkuu Mwandamizi Serikali, Benard Kongola alieleza jana mbele ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Morogoro, Mary Moyo , kuwa siku hiyo alikuwa na mashahidi  wawili badala ya watatu ambapo  mmoja alishindwa kufika mahakamani  kutokana na kupatwa na udhuru.
Mashahidi ambao wameshatoa ushahidi wao  mbali na aliyekuwa Kamanda wa Polisi Mkoa, ni  aliyekuwa Mkuu wa Polisi wa Wilaya ya Morogoro (OCD), Sadick Tindwa, ambaye kwa sasa ni OCD Wilaya ya Handeni, mkoani Tanga.
Shahidi mwingine  ni  mtaalamu wa kitengo maalumu cha uchunguzi wa picha  Sajini taji Aristides, ambaye aliwasilisha ushahidi wake juzi kwa kuleta mkanda wa video unaodaiwa kuonesha uhalisia wa tukio zima  la kesi yake inayomkabili ya kutoa maneno ya uchochezi.
Mrakibu Mwandamizi wa Polisi, Japhet Mabeyo ambaye ni Mkuu wa Kitengo cha Maabara ya Uchunguzi Makao Mkuu wa Upelelezi Dar es Salaam, alikuwa ni shahidi wa sita jana kutoa ushahidi wake mahakamani hapo.
Katika ushahidi wake akiongozwa na Wakili wa Serikali , Mabeyo alieleza majukumu yake akiwa  Mkuu wa Kitengo cha Maabara ni kusimamia masuala ya utawala ya kila siku ikizingatiwa kitengo hicho kinashughulika na mambo mbalimbali yakiwemo kutoka mikoani.
Shahidi wa saba katika kesi hiyo ambaye ni Mkuu wa Kitengo cha Utambuzi  Polisi Mkoa wa Morogoro Inspekta wa Polisi Jafert Msongole, alitoa ushahidi wake kwa kueleza taratibu alizozifanya katika kuchukua mkanda wa video iliyoonesha namna mshitakiwa alivyotoa maneno ya uchochezi katika kongamano la Eid Pili lililofanyika Agosti 10, mwaka 2013 katika viwanja vya Shule ya Msingi Kiwanja cha Ndege Manispaa ya Morogoro.
Aliendelea kuieleza Mahakama kuwa uchukuaji wa picha za matukio mbalimbali ni utaratibu wa kitengo hicho na kwamba alimtuma askari wake kwenda kuchukua picha kwa kuwa tayari alishapata taarifa kuwa huenda Shehe Ponda angehudhuria katika kongamano hilo.
Hata hivyo upande wa utetezi ukiongozwa na wakili Juma Nasoro ulimuuliza maswali ya msingi shahidi huyo likiwemo la kutaka kujua kama kuwepo kwa Shehe Ponda katika kongamano hilo kungevuruga amani.
Akijibu maswali hayo Shahidi kuyo alieleza kuwa aliamini kuwepo kwa Sheikh Ponda katika kongamano hilo kungeweza kuvuruga amani kwani alishapata taarifa kutoka kwa wakubwa wake wa kazi kuwa Shehe Ponda hakutakiwa kuwepo katika kongamano hilo.

No comments: