UAGIZAJI MAFUTA KWA PAMOJA KUOKOA MABILIONI



Tanzania inatarajia kuokoa mabilioni ya fedha kutokana na kuanza kutekeleza mfumo wa uagizaji mafuta kwa pamoja na kwa kiasi kikubwa.

Hayo yalibainishwa Dar es Salaam jana na Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Charles Mwijage alipofungua programu ya mafunzo maalumu ya wajasiriamali wanaoagiza nishati ya mafuta, yaliyoandaliwa na First National Bank (FNB).
Mafunzo hayo yanahusu namna ambavyo wagizaji mafuta, wanaweza kupata dhamana za benki na kulipa kwa pamoja mara moja, tofauti na sasa ambapo wanaagiza kwa pamoja, lakini kila mwagizaji analipa kivyake.
Akizungumza katika mafunzo hayo, Mwijage alisema mfumo wa siku za nyuma ambao waagizaji hao mafuta hawakuwa na ushirikiano, ulikuwa na usumbufu na ulikuwa unalipozea taifa zaidi ya dola za Marekani milioni 60 (Sh bilioni 102) kila mwaka. 
Hivi sasa waagizaji hao, wanaagiza kwa pamoja kupitia mfumo huo mpya, ambao umepunguza gharama, umeongeza tija na ufanisi na kuokoa muda na rasilimali nyingine. 
Hata hivyo, alisema taifa linaweza kuokoa fedha zaidi, endapo watakuwa na mfumo wa kulipa kwa pamoja.
Alisema pamoja na mfumo mpya kupunguza gharama kwa waagizaji umekuwa na manufaa kwa watumiaji, ambao ndio wadau wakubwa katika biashara hiyo.
Mkurugenzi wa Umoja wa Waagizaji Mafuta (PIC), Michael Mjinja alisema changamoto kubwa ilikuwa ni gharama za usafirishaji mafuta kwa meli lakini sasa changamoto hiyo haipo tena na vile vile waagizaji wanaaminiwa zaidi kwenye masoko.

No comments: