Mtuhumiwa Tissi Mallya ambaye alitoroka
baada ya kumuua askari Polisi G.7168 Koplo Joseph Swai, ameuawa usiku wa
kuamkia jana na wananchi alipokuwa amejificha akiwa na panga lenye damu, lililotumika
kwenye mauaji hayo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, David
Misime alisema hayo jana katika mkutano wake na waandishi wa habari, alisema
mauaji hayo yalitokea juzi asubuhi katika eneo la Chang’ombe Juu.
Kamanda Misime (pichani) alisema baada ya Malya
kutekeleza mauaji hayo alikimbia, lakini ilipofika majira ya saa 5 usiku
wananchi walimuona maeneo ya Mtimkavu Mailimbili akiwa bado na panga alilotumia
kumuua Koplo Joseph.
“Wananchi walichukua sheria mkononi na
kumshambulia sehemu mbalimbali za mwili
wake, polisi walifika eneo la tukio na kumchukua kisha kumkimbiza
Hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Dodoma lakini aligundulika tayari amefariki”,
alisema.
Kamanda Misime alisema katika kumbukumbu
walizonazo ni kuwa mwaka 2006 Malya aliwahi kufungwa miaka mitatu kwa kosa la
kujeruhi, pia mwaka 2009 alifungwa tena miezi sita kwa kosa la kutishia kuua.
“Nawapongeza wananchi walioonesha
kuchukizwa na kitendo alichotendewa askari wetu lakini waache kujichukulia
sheria mkononi,” alisema.
Pia, alitoa wito kwa wananchi kuanza kuchukua
hatua kurekebisha maadili kuanzia ngazi ya familia, kwani imebainika mtuhumiwa
alikuwa mvuta bangi, kiasi cha kumfanya awe anafanya vitendo ambavyo ni kinyume
na maadili wa nchi.
Kwa upande wake, Diwani wa kata ya
Mnadani Steven Masangia alisema alifahamu Koplo Joseph Swai kama kijana
mchapakazi, ambaye alijitolea kutoa elimu hata kwenye mitaa juu ya ulinzi
shirikishi.
Alisema Jeshi limempoteza kijana shupavu,
ambaye alikuwa nguzo na kiungo kikubwa katika
watu wa rika zote.
“Alipokuwa Mnadani, alipambana
kuhakikisha uhalifu unakomeshwa na hata vijana wanaovuta bangi
aliwasambaratisha, na alikuwa akifundisha polisi jamii kwenye mitaa ya kata”,
alisema.
Alisema kijana huyo alikuwa mchapakazi na
alikuwa akiipenda kazi yake na amekufa kama shujaa.
“Alikuwa na cheo kidogo, lakini kazi
alizokuwa akifanya zilikuwa ni kubwa kulinganisha na cheo na umri wake,”
alisema .
Katika mkasa huo, uliotokea juzi asubuhi,
askari huyo aliitikia wito uliofika kwake wa kuwapo kwa dalili ya tendo la
jinai nyumbani kwa mkazi mmoja wa Chang’ombe Juu .
Katika taarifa yake ya awali, Kamanda
Misime alisema askari huyo alipigiwa simu na Mtendaji wa Mtaa wa Chang'ombe Juu
akimjulisha kuwa amepokea taarifa ofisini kwake kutoka kwa Oliver Baltazar (52)
mkazi wa Chang'ombe Juu kuwa mtoto wake aitwaye Tisi Sirili anaonekana anataka
kumuua au ameshamuua mtoto wake wake wa miezi minane, Valerian Tisi.
Alisema baada ya kupokea taarifa hiyo
askari huyo alienda ofisini kwa Mtendaji huyo ambapo waliongozana hadi nyumbani
kwa mtuhumiwa.
"Alipofika askari aligonga mlango
huku akijitambulisha kuwa yeye ni askari ili mtuhumiwa atoke nje, alichofanya
mtuhumiwa ni kumnyanyua mtoto wake mdogo wa miezi minane kwa mkono mmoja kichwa
chini miguu juu na kutaka kumkata kwa panga huku akisema, namkata shingo na
sitaki kuona mtu.
"Askari aliamua kumuokoa mtoto huyo
kwa kumrukia mtuhumiwa lakini kwa bahati mbaya aliteleza na ndipo mtuhumiwa
akamkata kichwani askari wetu,"alisema Misime.
Aidha alisema, pamoja na askari huyo
kuanguka mtuhumiwa aliendelea kumkatakata kwa panga huku Mtendaji na kijana
aliyekwenda naye katika eneo la tukio, wakikimbia huku wakipiga kelele za
kuomba msaada.
Alisema mtuhumiwa baada ya kufanya
kitendo hicho cha kinyama, alikimbia akiwa na panga lake huku nguo zake zikiwa
zimetapakaa damu.
Kasi kukabili uhalifu
Wakati
huohuo, Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini (IGP), Ernest Mangu jana
aliongoza mamia ya wakazi wa Dodoma kumuaga askari Polisi aliyeuawa wakati
akitekeleza majukumu yake na kuliagiza Jeshi la Polisi kuongeza kasi ya
kupambana na uhalifu na wahalifu.
Askari huyo aliyeuawa Koplo Joseph Swai
(27) tayari amesafirishwa kwenda Arusha kwa maziko.
Alisema Jeshi la Polisi linatakiwa
kuongeza kasi ya kupambana na uhalifu, kutokana na kuongezeka kwa vitendo hivyo
ndani ya jamii.
“Kijana amekufa kishujaa wakati akitetea
mtu asiye na uwezo wakati akinyanyaswa, katika kifo hiki askari wapate cha
kujifunza kwani kimewatia nguvu na kuwawezesha kufahamu namna ya kukabiliana na
uhalifu. Msiba huo ni fursa ya kujihami na kukomesha uhalifu,” alisema.
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Chiku Gallawa
alisema ni wajibu wa jamii kufichua wahalifu ili waweze kukabiliana na mikono
ya sheria.
No comments:
Post a Comment