Serikali imeingilia kati manyanyaso
wanayopata wafanyabiashara ndogo na mamalishe nchini, kwa kuamua kuunda kikosi
cha kiofisi, kitakachohusisha wajasiriamali hao kwa lengo la kukubaliana juu ya
maeneo na muda mwafaka wa kuendesha shughuli zao.
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda aliliambia
Bunge jana kwamba amepata taarifa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa
na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), ambayo imewasilisha mapendekezo hayo kwake,
juu ya hatua za kutatua tatizo hilo.
Pinda alisisitiza kwamba wazo hilo la
Tamisemi ni jema, na alitaka mkutano kwa ajili ya utekelezaji wake, uanze wiki
ijayo ili waweze kuandaa utaratibu mapema iwezekanavyo.
Alisema hayo akijibu swali la papo kwa
hapo la Mbunge wa Kilwa Kaskazini, Murtaza Mangungu (CCM) aliyesema baadhi ya
wabunge wamekuwa wakihoji juu ya manyanyaso ya wafanyabiashara wadogo, mama
lishe na waendesha pikipiki (bodaboda). Alisema, lakini kwa kipindi chote
Waziri Mkuu amekuwa akitoa maelekezo juu
ya tatizo hilo, lakini mamlaka zinazohusika, haziko tayari kutii amri yake. “Je
unawaambia nini Watanzania?” alisema Mangungu.
Akijibu, Pinda alisema matatizo
yanayokumba wajasiriamali hao ni makubwa na si kwa Jiji la Dar es Salaam pekee, bali nchi nzima
hivyo serikali imeamua kutafuta ufumbuzi wa kudumu na dhamira ipo.
“Jana (juzi) nimepata taarifa kutoka
Tamisemi, wanaleta mapendekezo kwangu
juu ya mapendekezo ya kutatua tatizo hilo. Katika taarifa yao, wamependekeza
kwamba wataunda kikosi cha kiofisi kitakachofanya kazi kupitia makundi ya
viongozi wa wamachinga nchini. Watakubaliana nao juu ya maeneo yatakayotumika
na muda muafaka wa kufanya shughuli,” alisema.
Kwa mujibu wa Waziri Mkuu, kikubwa
alichoona katika mapendekezo ya Tamisemi, wametaka suala la usafi katika maeneo
yatakayotumika kwa biashara, lipewe kipaumbele.
Alisema wataanza na Jiji la Dar es Salaam
kufikia maelewano na vyombo vyote vinavyohusika, vitaeleweshwa juu ya
maafikiano hayo kabla ya mkakati huo kusambaa kwenye majiji na miji mingine.
Alisema suala la kutenga maeneo kwa ajili
ya biashara kwa siku maalumu, si la Tanzania pekee kwani liko kwenye nchi
nyingi. “Hata nchi za nje wana Sunday markets (masoko ya Jumapili). Hakuna tofauti na hili,” alisema Pinda na kusisitiza
kwamba amekubaliana na Tamisemi jambo
hilo walipe kipaumbele tofauti kuliko ilivyokuwa awali.
Kwa muda mrefu, katika miji mikubwa
nchini kumekuwa na msuguano wa mara kwa mara baina ya mamlaka katika miji
husika na wafanyabiashara, kiasi cha kuonekana kama mamlaka husika hufanya
unyanyasaji wa makusudi dhidi ya wafanyabiashara hao.
No comments:
Post a Comment