MAANDAMANO YA CUF YAPIGWA ‘STOP’


Chama cha Wananchi -CUF kimeamua kuahirisha maandamano yake, yaliyopangwa kufanyika jana, ikiwa ni ishara ya kuadhimisha miaka 14 ya vifo vya wafuasi wake waliopoteza maisha Januari 27, mwaka 2001.

Hatua hiyo iliafikiwa na viongozi wa juu wa chama hicho baada ya Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, kupiga marufuku maandamano hayo na kubainisha kuwa ni batili.
Taarifa ya Jeshi la Polisi iliyotumwa katika ofisi za chama hicho, ilitoa sababu tatu za kuahirisha maandamno hayo.
Sababu hizo ni maandamano hayo yaliyotarajiwa kufanyika jana kuadhimisha mauaji hayo, yangeleta chuki ndani ya jamii, na pia sababu za kiintelijensia zilionesha uwezekano wa kuwepo na vurugu na hali ya uvunjifu wa amani, kutokana na matishio ya usalama na ugaidi, ambayo  yanaweza kuhatarisha maisha ya waandamanaji.
Akitoa maazimio ya kuahirisha maandamano hayo, Mwenyekiti wa chama hicho, Profesa Ibrahimu Lipumba alisema polisi hawajakitendea haki chama hicho, kwani walichelewa kujibu maombi yao ya kufanya maandamano ya amani ya kuadhimisha vifo vya ndugu zao na wafuasi wa chama chao.
“Polisi hawajakitendea haki chama chetu. Tokea siku ya Alhamisi wiki iliyopita tulipeleka barua ya kuomba kibali lakini hadi jana saa kumi na mbili ndio wanaleta taarifa ya kuahirisha maandamano na wakati huo viongozi wote walishaondoka ofisini,” alisema Lipumba.
Alisema kuchelewa kwa taarifa hiyo, kulikuwa na nia mbaya na wananchi, kwani wananchi walishajiandaa tayari kwa ajili ya kuandamana kwenye maadhimisho hayo.
“Wananchi hawakuweza kupata taarifa ya kuahirishwa kwa maandamano hayo na ndio maana leo wamefika hapa kwa wingi,” alisisitiza Lipumba.
Hata hivyo, mwenyekiti huyo alisema chama chake kina mipango mingi ya maendeleo ya taifa, hivyo wameona ni vyema kuahirisha maandamano hayo ili kutochafua taswira ya chama na kuwaomba wafuasi wake wawe watulivu na kuendelea na shughuli zao za kawaida.
“Chama chetu kina malengo mazuri na taifa hili. Haitakuwa vyema kuendelea na maandamano haya kwani yatasababisha kupigwa na kukamatwa na polisi na hivyo kuvuruga kabisa mipango yetu ya maendeleo ya chama na taifa kwa ujumla,” alisema.
Awali, kabla ya kuwasili kwa viongozi wakuu wa chama hicho, wafuasi wake walionekana kuwa na jazba wakiwa wamebeba mabango yenye ujumbe tofauti tofauti na huku wakiwa wamefunga vitambaa vyeusi kwenye mikono yao.
Maandamano hayo yalipangwa kuanzia ofisi za makao makuu ya chama hicho Manispaa ya Temeke mtaa wa Boko na kumalizikia katika viwanja vya Zakhem Mbagala.

No comments: