DAWASCO YAOMBA RADHI KWA UKOSEFU WA MAJI


Mamlaka ya Maji Safi na Salama Dar es Salaam (DAWASCO) imewaomba radhi wakazi wa jiji la Dar es Salaam kutokana na kukosekana kwa huduma ya maji tangu juzi baada ya mtambo wa Ruvu Chini kwenda Dar es Salaam kupasuka.

Akizungumza na waandishi wa habari jana katika ofisi za Dawasco, Ofisa Mtendaji  Mkuu Jackson Midala, alisema Ijumaa na Jumamosi mtambo ulizimwa kwa ajili ya matengenezo na kazi ilikamilika na kuanzia Jumatatu maji yalitoka. Lakini, alisema kwa bahati mbaya upande mmoja wa mtambo, ulifyatuka na kusababisha kutopatikana kwa huduma hiyo tangu juzi.
Alisema wamelazimika kuzima mtambo kwa ajili ya marekebisho na mpaka jana jioni mtambo utakuwa umekamilika na utaendelea kutoa huduma kama kawaida, hivyo aliwataka wakazi wa jiji kuwa na subira, kwani mtambo ukizimwa unachukua saa nne hadi tano maji kufika mjini.
“Mtambo ukizimwa maji yanachukua muda kufika, ila tuna imani kuwa kuanzia alfajiri ya leo maji yatakuwa yamefika na watu watapata huduma kama kawaida,” alisema Midala.
Aliongeza kuwa maeneo yaliyoathirika na tatizo hili ni Tegeta, Bagamoyo, Boko, Bunju, Bahari Beach, Sinza, Kinondoni, Sinza, Mwenge, Chuo Kikuu, Ununio, Masaki, Mwananyamala, Magomeni na Msasani.

No comments: