MAWAKILI WAOMBA KESI YA ESCROW ISIMAMISHWE


Mawakili wa upande wa utetezi katika kesi mbili za kupokea rushwa ya zaidi ya Sh bilioni 2 kutoka katika akaunti ya Tegeta Escrow, wameiomba Mahakama kusimamisha kesi hizo hadi itakaposikiliza hoja zao.

Walidai hayo mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam jana, Frank Moshi baada ya washitakiwa kusomewa upya mashitaka yao.
Washitakiwa hao wanaokabiliwa na kesi mbili tofauti ni Meneja Misamaha ya Kodi TRA, Kyabukoba Mutabingwa na Mhandisi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Theophilo Bwakea.
Katika kesi ya Mutabingwa anayedaiwa kupokea Sh bilioni 2 ambazo ni sehemu ya fedha zilizokuwa kwenye akaunti ya Tegete Escrow, Wakili Deo Ringia alidai kuna hoja za kikatiba ambazo zimejitokeza katika kesi hiyo na zinatakiwa kusikilizwa Mahakama Kuu.
Alidai wamewasilisha notisi ambayo ina nyaraka watakazozitumia kuishawishi mahakama itoe amri watakazoziomba hivyo aliomba kesi ipangiwe tarehe ya kutajwa ili Mahakama iangalie hoja hizo na kama itaridhika isimamishe kesi hadi zitakaposikilizwa.
Hakimu Moshi alisema kesi itatajwa Februari 26 lakini hawatamsomea mshitakiwa maelezo ya awali hadi watakaposikiliza pingamizi la utetezi kuona kama lina msingi.
Awali akisomewa mashitaka na Wakili kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) alidaiwa Januari 27,2014 katika benki ya Mkombozi wilaya ya
Ilala, alipokea Sh bilioni 1.6, kutoka kwa mmiliki wa kampuni ya kufua umeme ya VIP Engineering and Marketing ambaye pia alikuwa Mkurugenzi wa kampuni ya IPTL, James Rugemalira.
Aidha, anadai Julai 15,2014, alipokea Sh milioni 161.7, Agosti 26, 2014 Sh milioni 161.7 na Novemba 14, 2014 Sh milioni 161.7, kupitia akaunti namba 00110202613801 kama tuzo kwa kuiwakilisha kampuni ya Mabibo Beer Winesand Spirits ambayo ni mali ya Rugemalira mahakamani, kitu ambacho ni kinyume cha sheria.
Anadaiwa kupokea fedha hizo ambazo ni sehemu ya zile zilizokuwa kwenye akaunti ya Tegeta Escrow bila kumtaarifu bosi wake ambaye ni Kamishna wa TRA na kwenye Tume ya Maadili ya viongozi.
Katika kesi ya Bwakea Wakili Ringia aliomba pia isimamishwe hadi watakaposikiliza hoja zao.
Bwakea anadaiwa, Februari 12, 2014 katika jengo la Benki ya Mkombozi Ilala alipokea rushwa ya Sh milioni 161,700,000 kutoka kwa Rugemalira akiwa kama mjumbe aliyeandaa sera kuruhusu sekta binafsi kuzalisha na kuliuzia umeme Shirika la Umeme (Tanesco).
Wakili Swai alidai, Bwakea alijipatia fedha hizo kupitia akaunti namba 00410102643901 bila kumtaarifu bosi wake ambaye ni Kamishna wa Tume ya Maadili ya Viongozi. Kesi itatajwa tena Februari 26 mwaka huu.

No comments: