Mahakama ya Wilaya ya Mbarali mkoani Mbeya imemhukumu kifungo cha
maisha jela mkazi wa Madibira wilayani hapa kwa kosa la kumlawiti mtoto mwenye
umri wa miaka mitano.
Aliyehukumiwa kutumikia kifungo hicho ni Samwel Mnyonge (30)
ambapo hukumu hiyo imetolewa na hakimu mfawidhi wa mahakama ya wilaya ya
Mbarali, Guwai Sumaye.
Awali ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashitaka wa Polisi,
Mazoya Luchagula mbele ya hakimu mfawidhi Sumaye kuwa mshitakiwa alitenda kosa
hilo Februari 11, 2014 kijijini Madibira.
Alisema awali mshitakiwa alimbeba mtoto huyo wa umri wa miaka
mitano kwenye baiskeli akiwa amempa msaada wa kumrejesha nyumbani alipokuwa
akitokea shuleni, lakini wakiwa njiani, Mnyonge alimpeleka mtoto kwenye shamba
la mahindi na kumlawiti.
Alisema kutokana na majeraha makubwa aliyoyapata mtoto huyo,
alikimbizwa Hospitali ya Mafinga wilayani Mufindi, Iringa na baadaye Hospitali
ya Taifa ya Muhimbili, Dar es Salaam alikotibiwa kwa miezi minane.
Akitoa hukumu baada ya kuridhishwa na ushahidi
uliotolewa mahakamani hapo, Hakimu Mfawidhi Guwai Sumaye alisema anamhukumu
Mnyonge kwenda jela kutumikia kifungo cha maisha ili iwe fundisho kwa wengine
wenye tabia hiyo.
No comments:
Post a Comment