MKUU WA MKOA AHIMIZA WATOTO WASOME SHULE JIRANI


Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadiki ametaka  wazazi kuandikisha watoto wao katika shule zilizo jirani na maeneo wanayoishi kuwaepusha na usumbufu.

Akizungumza na mwandishi,  Sadiki alisema kumekuwa na tabia ya baadhi ya wazazi kuandikisha watoto wao katika shule mbalimbali zilizopo maeneo ya mbali na wanapoishi kwa kigezo cha kufuata ubora wa elimu inayotolewa bila kujali usumbufu wanaopata watoto, ikiwemo suala la usafiri.
Alisema suala hilo linalogeuka kuwa tatizo kwa watoto kwa kusafiri umbali mrefu, linapaswa kuepukwa na wazazi kwa kuwa  yanaweza kumsaidia mtoto kuepuka mambo mbalimbali wakati anapokwenda au kutoka shuleni.
“Ni vyema wazazi wakazingatia suala hili, maeneo yote ya jiji hili yana shule nyingi na nzuri kwa ajili ya kuwaandikisha watoto hawa, umbali siyo mtazamo mzuri kwa kigezo cha kutafuta elimu bora, suala la msingi ni kuwa karibu na wazazi  katika kufuatilia maendeleo ya mtoto kipindi anapokuwa shuleni,” alisema Sadiki.
Alisema kuwaandikisha watoto  katika shule zilizo mbali  na maeneo wanayoishi, kunaweza wakati mwingine athari zake zisitambuliwe na mzazi kwa haraka kutokana na kutomgusa moja kwa moja.
Katika hatua nyingine,  Sadiki amewataka watumiaji wote wa vyombo vya usafiri kuwa makini wakati wanavyoviendesha vyombo hivyo kwa lengo la kuepusha kusababisha madhara yakiwemo ya ajali hususani kipindi hili ambacho shule nyingi zimeanza kufunguliwa.
Alisema kwa kawaida shule zinapofunguliwa, watoto wengi huwa barabarani wakati wanapotoka au kwenda shule hivyo ni vyema kila dereva kwa nafasi yake kuwa makini wakati anapoendesha chombo chake ili kuhakikisha hasababishi ajali.
Aidha, alionya makondakta pamoja na wapigadebe juu ya tabia yao ya kuwabughudhi wanafunzi kwa kuwazuia kupanda katika mabasi na kusisitiza kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao pindi watakapobainika.

No comments: