WANAWAKE 200 WAJITOKEZA AGA KHAN KUCHUNGUZWA SARATANI YA MATITI


Wanawake zaidi ya 200 jana walijitokeza katika kambi ya bure ya uchunguzi wa saratani ya matiti katika Hospitali ya Aga Khan jijini Dar es salaam, kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi pamoja na kupata ushauri kuhusu saratani ya matiti.
Akizungumza katika kambi hiyo jana, Daktari Bingwa wa magonjwa ya saratani, Dk Amyn Alidina alisema hospitali ya Aga Khan inaadhimisha mwezi wa ufahamu wa saratani ya matiti duniani kwa kutoa huduma ya uchunguzi kwa wanawake bila malipo.
Dk  Alidina alisema kambi hiyo ni sehemu ya kampeni ya hospitali hiyo yenye kaulimbiu “Usisubiri hadi Oktoba” iliyolenga kuhamasisha umma kuchukua hatua ya kutunza afya zao sasa badala ya kusubiri muda maalumu wa mwaka.
Dk Alidina alisema saratani ya matiti inachangiwa na sababu mbalimbali ikiwemo historia ya  saratani katika  familia, mfumo wa kazi unaoweza kusababisha kansa, mfumo wa maisha kama vile uvutaji wa sigara, mfumo wa kula, historia ya maambukizi ya virusi, na saratani iliyopita. 
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Hospitali ya Aga Khan, Dk Mustaafa Bapumia alisema kuwa hospitali hiyo imeona umuhimu wa kuweka kambi hiyo ili kuwasaidia wanawake baada ya kuona kwamba tatizo hilo linawakumba wanawake wengi na wanashindwa kujitambua mapema kutokana na kukosa huduma ya uchunguzi.

No comments: