Benki ya Barclays tawi la Iringa imetoa mafunzo ya
utunzaji wa fedha kwa wanafunzi wa shule ya sekondari ya Highlands ya mjini
hapa waliokiri matumizi ya pombe yanazifanya baadhi ya familia zao kukosa
akiba.
Katika majadiliano yao, wanafunzi hao walitaja vipaumbele
vya familia zao kwamba ni malazi, chakula, maji, shule na mavazi hata hivyo
wakasema pamoja na umuhimu wake, matumizi ya pombe na vitu vingine vya anasa
yanadhohofisha upatikanaji wa huduma hizo kwa sababu ya kukosa akiba.
Meneja wa tawi hilo, Shamsa Abdulatif alisema katika
mafunzo hayo yanayotarajiwa kuwanufaisha wanafunzi wa shule nyingine za mkoani
hapa kwamba, kila mtu anaweza kufikia ndoto ya mahitaji yake kama atakuwa na
nidhamu ya matumizi sahihi ya fedha.
Aliyataja mahitaji hayo kuwa ni pamoja na kumudu gharama
za elimu, ujenzi, ununuzi wa vyombo mbalimbali vya usafiri, vyakula na huduma
nyingine muhimu kwa matumizi ya binadamu.
“Wanafunzi mnaweza kujiwekea akiba kutokana na kidogo
mnachopewa na wazazi wenu kwa ajili ya matumizi yenu ya kila siku muwapo
shuleni, lakini pia mnaweza kusaidia kuwashauri wazazi na walezi wenu
kujiepusha na matumizi yasio ya lazima ili mpate akiba,” alisema.
Meneja huyo alitoa mfano akisema katika kila Sh 1,000
anayopewa mwanafunzi kwa ajili ya matumizi yake shuleni anaweza kujiwekea akiba
ya hadi nusu ya kiasi hicho ambacho kwa mwaka kinaweza kuwa kikubwa.
No comments:
Post a Comment