MAKUBALIANO YA KIKWETE, UKAWA KUWEKWA HADHARANI KESHO


Mazungumzo kati ya Rais Jakaya Kikwete na viongozi wa vyama vya siasa, yamefanyika vizuri katika Ikulu ndogo ya Dodoma na kufikia makubaliano katika baadhi ya maeneo.
Akizungumza na waandishi wa habari baada ya mazungumzo hayo jana, Mwenyekiti wa Kituo cha Demokrasia (TCD), John Cheyo, alisema mazungumzo yameendelea kuwa mazuri na mara hii wamefikia makubaliano katika baadhi ya mambo.
“Mazungumzo yalikuwa mazuri na kuna baadhi ya maeneo tumekubaliana, lakini taarifa zaidi tutaitoa kesho kwenye mkutano na waandishi wa habari,” alisema Cheyo.
Mkutano huo ambao ni wa pili kati ya Rais Kikwete na viongozi wa vyama hivyo, ulihudhuriwa na viongozi wakuu wa vyama vya CCM, Chama cha Wananchi (CUF), Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na NCCR-Mageuzi, ambavyo vinaunda kundi la Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Viongozi wengine waliohudhuria ni kutoka Tanzania Labour Party (TLP) na United Democratic Party (UDP) na vyama vingine visivyo na wabunge, viliwakilishwa na chama cha UPDP.
Kwa upande wa CCM, waliohudhuria mkutano ni Katibu Mkuu, Abdulrahman Kinana na Makamu Mwenyekiti, Philip Mangula; Chadema iliwakilishwa na Katibu Mkuu wake, Dk Willibrod Slaa na Mwanasheria wake, Tundu Lissu.
CUF iliwakilishwa Mwenyekiti wa Taifa, Profesa Ibrahimu Lipumba wakati NCCR-Mageuzi iliwakilishwa na Mwenyekiti wa Taifa, James Mbatia. TLP iliwakilishwa na Mwenyekiti wake wa Taifa, Augustine Mrema wakati Fahmi Dovutwa wa UPDP aliwakilisha vyama vingine visivyo na wabunge.
Mbali na Cheyo kusema kuwa kuna baadhi ya mambo kimsingi wamekubaliana,  hakuna kiongozi hata mmoja ambaye  alikuwa tayari kusema mambo waliyokubaliana hadharani, zaidi ya Mrema kujipigia debe kuwa ameendelea kumsemea Mbatia kwa Rais, kutokana na kitendo chake cha kunyatia jimbo la Vunjo.
“Nimemkumbusha tena Rais suala la Mbatia na Rais kamwambia Mbatia kuwa amemteua ili aende bungeni na sio aende Vunjo,” Mrema aliwaambia waandishi wa habari nje ya hoteli ya Dodoma, ambako wajumbe hao walikutana kwa muda baada ya kutoka Ikulu ndogo ya Dodoma.
 Mazungumzo ya viongozi hao wa kisiasa, yana lengo la kutafuta muafaka wa mchakato wa Katiba, ambao umesuswa na Ukawa, ambao wanadai kuwa Bunge Maalumu la Katiba, halina mamlaka ya kubadili baadhi ya vifungu katika Rasimu ya Katiba mpya, iliyotengenezwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba mpya. 
Baada ya Ukawa kususa na kutoka nje ya Bunge hilo, wamekuwa wakimtaka Rais Kikwete avunje Bunge Maalumu, kwa madai kuwa limekosa uhalali wa kisiasa, baada ya vyama vinavyounda umoja huo kusisitiza kuendelea kususa.
Hata hivyo, tayari Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Frederick Werema, aliweka wazi kuwa Sheria iliyoanzisha mchakato huo na kuunda Bunge hilo, haikutoa mwanya wa mtu yeyote kuvunja bunge hilo.
Badala yake, sheria imempa mamlaka Rais kuongeza siku za kufanya vikao vya Bunge hilo, iwapo litakuwa halijamaliza kuandika Katiba mpya ndani ya siku 70.
Wananchi wengi wana hamu ya kusikia yaliyojiri ndani ya kikao hicho, kutokana na unyeti wa jambo lenyewe la Katiba. Cheyo aliahidi kukata kiu hiyo ya Watanzania leo mchana, atakapozungumza na wanahabari mjini hapa.

No comments: