HAWA NDIO WALIOFARIKI, MAJERUHI AJALI YA FUSO SUMBAWANGA


Watu wanane  wamekufa papo hapo na wengine 11 kujeruhiwa baada ya gari walilokuwa wakisafiria jana kuacha njia na kupinduka katika Mlima Katete kijijini Milumba wilayani Mlele. 
Akizungumza na mwandishi kwa njia ya simu, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Katavi, Dhahiri Kidavashari  alisema ajali  hiyo iliyotokea saa 11 alfajiri ilihusisha lori aina ya Mitsubishi Fuso lenye namba za usajili T 234 AXK. 
Aliongeza kuwa gari hilo likiwa limesheni bidhaa mbalimbali lilikuwa likitokea kijiji cha Kibaoni wilayani Mlele likielekea mjini Sumbawanga mkoani Rukwa likiwa linaendeshwa na Jamal Mohammed (42) Mkazi wa   Mbagala, Dar es Salaam. 
Kamanda Kidavashari amewataja waliopoteza maisha kuwa ni Peter Lusambo (24), Ngelela Shauritanga (29), John Pius (32). Mwingine aliyetambuliwa kwa jina moja tu la Linus (30) wote wakiwa wakazi wa kijiji cha Kibaoni Wilaya ya Mlele. 
Aliwataja wengine kuwa ni pamoja na  Makono  Kisumu (23), Elias Mussa (28) wakazi wa wilaya ya Geita Mwanza,  Ally (34) mkazi wa Dar es Salaam ambaye alikuwa utingo wa gari hilo na  mwingine aliyetambuliwa kwa jina moja la Abbas (28), mkazi wa Mtaa wa Mpanda Hoteli wilayani Mpanda . 
Majeruhi ambao wamelazwa  kwa matibabu katika Hospitali  ya Wilaya ya Mpanda ni pamoja na Kaswagula  Linus  (25), Peter Mkalala ( 30), Peter Lusambo  (20) Castory Kaombwe (23) Nassor  Ramadhan (22) wote wakiwa  wakazi wa Kata ya Kibaoni Wilaya ya Mlele Mkoa wa Katavi.  Wengine ni Salim Hassan  (42) mkazi wa mjini Mwanza,  Jamari  Mohamed (42) Salumu  Njomoke (22) wakazi wa Dar es Salaam na   John  Chambaneje (32) mkazi wa  Mtaa wa Mpanda Hoteli  mjini  Mpanda. 
Kamanda Kidavashari alisema chanzo cha ajali hiyo ni kukatika kwa chombo aina ya propela, hivyo kumshinda dereva wa gari hilo na kupinduka. 
Kwa mujibu  wa Kidavashari dereva  wa gari hilo amekamatwa  na jeshi la Polisi  ambapo anatarajiwa kufikishwa  mahakamani   baada  ya upelelezi  wa  awali kukamilika.

No comments: