KAMPENI KUBWA YA CHUKIA UCHAFU YAANZA ILALA



Wilaya ya Ilala imeanzisha kampeni ya wiki tatu ya usafi  katika maeneo yaliyopo katikati ya jiji la Dar es Salaam kwa lengo la kutoa elimu na kuyaweka maeneo hayo safi na salama.
Kampeni hiyo ilizinduliwa jana katika eneo la Kisutu na Mkuu wa wilaya ya Ilala Raymond Mushi.
Akizindua kampeni hiyo alisema bila  suala la usafi kufanyiwa kazi, wageni wataona kwamba mambo katika Jiji la Dar es Salaam ni hovyo hasa ikizingatiwa kwamba katikati ya Jiji ndio sebule ya Jiji.
Kampeni hiyo inayosimamiwa na kampuni yenye dhamana ya usafi katika eneo hilo la kati ya Green Waste Pro Limited inashirikisha wananchi kwa lengo la kuwafanya wawe washirika wa usafi kwa kujenga utamaduni wa kuchukia uchafu.
Mkuu huyo wa Wilaya pamoja na kushukuru wananchi na wanafunzi wa Shule ya Kisutu waliofika  katika kampeni aliwataka viongozi kujipanga kuhakikisha kampeni hiyo inakuwa endelevu na yenye mafanikio.
Kampeni hiyo inafanyika katika Kata ya Kivukoni, Kisutu na Mchafukoge.
Pamoja na Mkuu huyo wa Wilaya kusema kwamba kampeni hiyo ni chachu kwa kata za pembezoni za kujali  usafi amewataka wananchi kuwa washiriki kwa kuhakikisha hawatupi uchafu hovyo.
Naye Naibu Meya na Diwani wa Kisutu Kheri Kessy alisema kazi ya usafi inakabiliwa na changamoto kubwa hasa kutokana na kuvuja kwa chemba za maji machafu na wananchi kutupa taka hovyo.
Alisema wananchi  na hasa wapitanjia kama wakijifunza kutupa uchafu maeneo wanayotakiwa watakuwa wamesaidia sana kujenga utamaduni wa kuchukia uchafu na pia kufanya maeneo yapendeze.
Alisema wananchi wa Kata yake ya Kisutu ni waelewa tangu kuanza kwa kampeni hizo miaka miwili iliyopita lakini wapitanjia wamekuwa wakivuruga utaratibu wa usafi.
Aliwataka wakazi wa Dar es Salaam kutimiza wajibu wao kwa kuhakikisha hawatupi taka hovyo na kuanza kuuchukia uchafu kutoka katika majumba yao hadi wanakotembea.
Kampuni inayoendesha kampeni hiyo ya Green Waste kupitia kwa Meneja wao Abdallah Mbena amesema kwamba kuna maendeleo makubwa katika kampeni za kuweka Jiji safi na safari hii wamewaalika wenzao kutoka Segerea na Upanga ili waone njia wanazotumia kuweka maeneo yao yenye dhamana safi na ya kupendeza.
Mbena alisema changamoto kubwa zinazokabili juhudi za kuweka maeneo safi ni upungufu wa usimamizi katika sheria kwani wengi hawakubali kuzitii.
Alisema kama wangezitii kungekuwa na usafi kila siku. Kwani wengine wamekuwa wakifika katika majengo yao na kuyasafisha na kutupa uchafu barabarani wakati wafagiaji wameshafanyakazi yao usiku.

No comments: