AJALI YA MABASI MUSOMA YAMSIKITISHA RAIS KIKWETE



Rais Jakaya Kikwete ameelezea huzuni na masikitiko yake makubwa kufuatia vifo vya watu 39 vilivyotokea katika ajali ya barabarani wilayani Butiama, Mkoa wa Mara, ambako pia watu 75 wameumia, baadhi yao vibaya.
Mara baada ya kupata taarifa hiyo iliyotokea jana asubuhi, Rais Kikwete ambaye yuko katika ziara ya kikazi ya siku tatu mkoani Arusha, amemtumia salamu za rambirambi Mkuu wa Mkoa wa Mara, akielezea huzuni na masikitiko yake.
 “Nakuomba uwafikishie wafiwa wote pole zangu nyingi sana, ukiwajulisha kuwa niko nao katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo. Aidha, napenda uwajulishe kuwa naungana nao kumwomba Mwenyezi Mungu aziweke pema roho za marehemu.”
Kufikia jana, Kamanda wa Polisi mkoani Mara, Phillip Kalinji alisema hakuna watu zaidi waliopoteza maisha. Aidha, alisema wote waliokufa, isipokuwa wawili tu, miili yao imetambuliwa na ndugu zao.
Hata hivyo, alisema hakuwa katika nafasi nzuri ya kuwataja marehemu na majeruhi wa ajali iliyohusisha magari matatu, yakiwemo mabasi yaliyogongana uso kwa uso na gari dogo aina ya Nissan Teranno lililogongwa na kutumbukia mtoni.
Mabasi yaliyogongana juzi majira ya saa 5:30 asubuhi ni Scania lenye namba za usajili T 736 AWJ mali ya Kampuni ya Mwanza Coach lililokuwa linatokea Musoma kwenda Mwanza na lingine aina ya Zoutong, lenye namba za usajili T 677 CYC mali ya Kampuni ya J4 Express lililokuwa linatokea Mwanza kwenda Musoma. Gari dogo lililogongwa aina ya Nissan Terrano lina namba za usajili T 332 AKK.
Mwandishi alifanikiwa kuwafahamu waliokufa kuwa ni daktari wa Hospitali ya Mkoa wa Mara, Dk Anatoria Ntangeki na Sayi Hassan aliyekuwa Mhandishi wa Mradi wa Umwagiliaji mkoani Mara.

No comments: