WATU 10 WAFARIKI MBEYA BAADA YA HIACE YAJIBAMIZA KWENYE FUSO



Watu kumi akiwemo mama na mtoto wake  wamekufa papo hapo na wengine wanane kujeruhiwa baada ya gari aina ya Toyota Hiace waliyokuwa wanasafiria kugongana na lori katika mji mdogo wa Mbalizi, Wilaya  ya Mbeya Vijijini.
Ajali hiyo imetokea majira ya saa 6:00 mchana  imehusisha gari aina ya Toyota Hiace lililokuwa likitokea Jijini Mbeya na Fuso lililokuwa likitokea katika kituo cha mafuta na kuingia barabara kuu ya kutoka Mbeya kwenda Tunduma.
Akizungumzia ajali hiyo, Muuguzi Mkuu wa Hospitali teule ya wilaya ya Mbeya, Sikitu Mbilinyi alisema kuwa wamepokea  maiti 10 wakiwemo wanawake wanne, wanaume  wanne na watoto wawili.
Alisema katika majeruhi wanane waliopokelewa hospitalini hapo, watano ni  wanaume na watatu ni wanawake na kwamba madaktari baada ya kubaini hali za majeruhi hao kuwa mbaya walishauri wapelekwe katika hospitali ya rufaa Mbeya .Tayari majeruhi watatu akiwemo mwanamke mmoja wamehamishiwa katika hospitali hiyo.
Aliwataja waliokufa katika ajali hiyo  ambao  wametambuliwa na ndugu zao kuwa ni pamoja na Mariam Mashambwe na mtoto wake Hamis Chaula, Rebeca Keneth, Petro mgogo, Haruna Jamison na Martin Mwasolikoto.
Aliwataja majeruhi waliofikishwa hospitalini hapo na kulazwa kuwa ni pamoja na kondakta  wa Hiace, Justin Chaula(28)mkazi wa Mabatini, kondakta wa lori Joseph Stephano (22)  mkazi wa Mbalizi , aliyekuwa abiria wa roli Ziona Goa  (20), Newton Patrick na dereva wa lori,  Amoni Mwakoko.
Mmoja wa majeruhi wa ajali hiyo,  Ziona Goa alisema kuwa Hiace waliyokuwa wamepanda ilikuwa na hitilafu katika breki na kusababisha gari kwenda kwa mwendo wa kasi na dereva kushindwa kulidhibiti na kuligonga lori ambalo tayari lilikuwa limeingia barabarani.
“Tulimsikia dereva akisema breki hazifanyi kazi huku gari likiwa kwenye mwendo kasi na ghafla mbele yetu kukawa na lori limekwisha ingia barabarani na tukaligonga ubavuni,” alisema.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Ahmed Msangi amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kwamba uchunguzi wa ajali hiyo unaendelea ili kubaini  chanzo cha ajali  hiyo.

No comments: