WASHAURI SUALA LA MAHAKAMA YA KADHI LISIINGIE KWENYE KATIBA



Suala la Mahakama ya Kadhi limeleta mjadala mkali katika majadiliano na wabunge wameamua suala hilo lisiingizwe kwenye Katiba. 
Mjadala huo mkali uliibuka katika Kamati namba Saba ilipojadili sura ya Nne ya kwenye rasimu hiyo inayozungumzia juu ya uhuru wa imani ya dini ambapo Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Hassan Ngwilizi alisema baada ya mjadala mkali wamekubaliana kutoingizwa kwenye Katiba. 
“Changamoto kubwa iliyojitokeza ni wakati tukijadili suala la Mahakama ya Kadhi kuna baadhi ya wajumbe walitaka liingizwe kwenye Katiba na wakanukuu Katiba ya Zanzibar imeruhusu Mahakama hiyo lakini tukaona si kweli na baada ya mjadala mkali tumekubaliana Mahakama ya Kadhi iwe nje ya Katiba,” alisema. 
Ngwilizi alisema jana kuwa Kamati yake imeshakamilisha upigaji kura na akidi kutimia kwa kila sura kwa kupata theluthi mbili kwa upande wa Zanzibar na Bara, wameondoa kipengele cha uraia pacha kwenye rasimu ya Katiba na kupendekeza kutungwe sheria itakayoingiza uraia huo kwa kuzingatia mambo muhimu ya utoaji wa uraia huo. 
Alitaja maoni mapya yaliyozingatiwa kwenye Kamati yake kuwa ni pamoja na ardhi kuundiwa sura yake na masuala ya serikali za mitaa lakini akaongeza “suala la kuwepo machifu au chochote kuhusiana na machifu hatukujadili”.
Juzi Umoja wa Machifu Tanzania uliwasilisha mapendekezo yao wanayotaka yaingizwe kwenye rasimu ya Katiba ikiwemo watambuliwe na washirikishwe kuanzia Serikali za Mitaa kwenye kupanga mikakati ya kijamii, kuundwe Tume  ya Utamaduni na lugha za asili zilindwe na kuendelezwa. 
Kuhusu vipengele vilivyobadilishwa alisema “tumeondoa serikali tatu na kuweka muundo wa serikali mbili na chemba za Bunge tumetaka mbili kama ilivyo sasa yaani Baraza la wawakilishi na Bunge la Jamhuri ya Muungano”. 
Naye Mjumbe Abdallah Bulembo kutoka kamati hiyo namba Saba alisema kwenye muundo wa Bunge kulitokea ubishi mkali kwani wapo waliotaka wabunge watano kutoka Bunge la Jamhuri ya Muungano wakawakilishe Bunge hili kwenye Baraza la Wawakilishi Zanzibar lakini baada ya mjadala mkali wakakubaliana muundo wa mabunge mawili ubaki kama ilivyo sasa.
Alisema kulikuwa na mvutano mkali kwenye suala la ardhi na kusisitiza “wengi waliipongeza Wizara ya Nishati na Madini kwa kuweka sheria kwamba kwenye kiwanja chako kukionekana madini unaweza kuuza asilimia 80 na asilimia 20 inabaki kwa mwenye kiwanja hivyo anakuwa mmoja wa wabia…mtaona bungeni suala la ardhi litakuwa na mjadala mkali na itachukua muda mrefu”. 
Mjumbe Kaika ole Telele alisema suala la mgombea binafsi lilileta mvutano mkali na mwishowe wakakubaliana awepo kwani halina madhara na kuzuia ni kuminya demokrasia kwani hata Marekani wameruhusu na hajawahi kushinda. 
Alisema wamekataa mabunge matatu na kukubaliana mabunge mawili kama ilivyo sasa na serikali mbili na kufafanua “suala hili tulijadili kwa siku mbili na hawa wajumbe kutoka Zanzibar waliridhika tubaki na mabunge mawili baada ya kuvutana sana…tumekubaliana pia Rais apunguziwe madaraka ya uteuzi, asiteue wakuu wa mashirika na taasisi aishie kumteua Mwenyekiti wa Bodi tu”. 
Kuhusu wafugaji alisema wamekubaliana kuwe na ardhi ya wafugaji  ili waache kutangatanga na hata maeneo ya mapori ambayo hayana hata digidigi yarudishwe kwa Rais na wapewe wafugaji ili watulie. 
Kwa upande wa Makamu Mwenyekiti wa Bunge, Samia Suluhu Hassan alisema Kamati ndogo ya Uongozi imeshafanyia kazi juu ya Mahakama ya Kadhi, Uraia pacha na muundo wa Bunge baada ya kukutana na wataalamu katika maeneo hayo na leo wanakutana na makatibu wakuu wa wizara za fedha kwa Zanzibar na Jamhuri ya Muungano kujadiliana juu ya kamati ya pamoja ya fedha ya muungano.

No comments: