WABUNGE EAC WAKUNWA NA UFANISI BANDARI, TRA



Wabunge wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA), wamepongeza ufanisi wa kazi unaofanywa kwa pamoja baina ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Mamlaka ya Bandari (TPA), huku wakizitaka nchi wanachama wa Jumuiya hiyo, kuhakikisha wanaunganisha reli za nchi zao ili kuongeza kasi ya uchukuzi na usafirishaji wa mizigo.
Hayo yalibainishwa jijini Dar es Salaam jana na Spika wa Bunge hilo kwa niaba ya wabunge hao, Dk Margaret Zziwa wakati walipofanya ziara kwenye bandari ya Dar es Salaam, kuona jinsi kazi zinavyoendeshwa.
Zziwa alisema ni wazi kwamba TPA na TRA wanafanya kazi nzuri inayohitaji pongezi na kwamba kwa ufanisi huo wameona mafanikio ya kuwa na jumuiya hiyo.
Alishauri nchi za jumuiya hiyo ambazo hazina reli zinazofanya kazi kuhakikisha zinafufuliwa au kujengwa na kuhakikisha zinajengwa na kuunganisha na reli za nchi nyingine ili kufanikisha huduma za uchukuzi na usafirishaji wa mizigo kutoka na kwenda bandarini.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bandari wa TPA, Awadh Massawe alisema ufanisi wa kazi bandarini umeongezeka na kwamba hivi sasa uondoshaji mizigo katika bandari hiyo hutumia kati ya siku mbili hadi tano, na kwamba hiyo inasaidia kupunguza gharama zisizo za msingi wa wafanyabiashara na ndani na wa nchi jirani.
Hata hivyo, alisema pamoja na ufanisi wa sasa bado Mamlaka hiyo inakabiliwa na changamoto nyingi ikiwamo ya usafirishaji wa mizigo, ambapo kwa hivi sasa asilimia 99 ya mizigo yote bandarini inabebwa kwa njia ya magari.
Akizungumzia mfumo mpya wa Himaya Moja ya Forodha (SCT) kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Kamishna Mkuu wa TRA, Lusekelo Mwaseba alisema mfumo huo ulioanza kufanya kazi mwezi Julai mwaka huu, utapunguza gharama za wafanyabiashara na pia utaondoa ufanyaji mara mbili wa taratibu za uondoshaji mizigo.

No comments: