VIFAA VYA KUTAMBUA WENYE EBOLA VYAWASILI



Serikali imeanza kuingiza nchini vifaa vya kuwabaini watu wanaohisiwa kuwa na dalili za ugonjwa wa homa kali ya ebola ambavyo vitawekwa kwenye viwanja vya ndege pamoja na baadhi ya maeneo ya mipakani.
Jana Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Steven Kebwe alikabidhi mashine nne za kuwapima abiria wanaoingia nchini kupitia viwanja vya ndege bila kuwagusa. Vifaa hivyo vinabaini mtu kuwa na dalili za ebola kutokana na joto lake na abiria wanapimwa kwa kumulikwa machoni na kwenye masikio.
Kwa kuanzia mashine hizo ambazo ni mfano wa kamera  zitapelekwa kwenye viwanja vya ndege vya Mwanza, Kilimanjaro, Zanzibar na Dar es Salaam. Maeneo hayo kwa mujibu wa naibu waziri huyo ndiyo yanapokea wagonjwa wengi kutoka nje ya nchi.
Dk Kebwe pia aliagiza shehena ya mashine zingine zitakazoingizwa nchini kuanzia leo zipelekwe kwenye viwanja vingine vya Mtwara, Kigoma na maeneo ya mipakani kuhakikisha kuwa kila abiria anayetoka nje ya nchi anapimwa dalili za ugonjwa huo hatari.
Pia aliagiza wanadiplomasia na viongozi wa kitaifa wanaotoka nje ya nchi ambako wanakwenda kuhudhuria mikutano mbalimbali pia wapimwe kwani ugonjwa hauchagui cheo wala fedha na hadhi aliyo nayo mtu.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya Dawa (MSD), Cosmas Mwaifwani alisema jana kuwa wamenunua mashine hizo nne kutoka Afrika Kusini, lakini  zimetengenezwa nchini Marekani kwa kiasi cha Sh milioni 16.
Alisema katika kipindi hiki ambacho kuna mlipuko wa ugonjwa wa ebola huko Afrika Magharibi, upatikanaji wa vifaa hivyo ni adimu na haiwezekani kupata mashine zote kwa msambazaji mmoja, hivyo akasema leo ziwawasili mashine nyingine mbili kutoka Ubelgiji.
Mkurugenzi wa Manunuzi wa MSD, Heri Mchunga alisema mashine hizo kitaalamu zinajulikana kama thermo scanners ni mashine za mkononi na kila abiria atakayeshuka uwanja wa ndege atapimwa kwenye macho au masikio bila kugusana.

No comments: