SERIKALI YARIDHISHWA NA MRADI WA DART



Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Hawa Ghasia ameridhishwa na tathmini ya Mkutano wa Mashauriano wa awamu ya kwanza wa Mradi wa Mabasi Yaendayo Haraka (DART), uliofanyika hivi karibuni.
Mkutano huo ulihusisha Kampuni ya Simon Group inayomiliki mabasi ya UDA na wamiliki wa mabasi ya daladala jijini Dar es Salaam. Lengo  la mkutano huo lilikuwa ni kuungana ili kuleta maendeleo katika sekta ya usafiri Dar es Salaam. 
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam hivi
karibuni, kuhusu maendeleo ya sekta ya usafiri na majadiliano yanayoendelea kufanyika wakati huu kuelekea katika mfumo mpya wa mabasi yaendayo haraka,Waziri Ghasia aliunga mkono jitihada zote, zinazofanywa na wadau katika sekta ya usafiri. 
“Kwa jinsi ambavyo mfumo unatakiwa uendeshwe na kwa jinsi  zabuni zitakapotangazwa bila kuwa na umoja itakuwa ni vigumu Watanzania kupata kazi,” alisema na kuunga mkono makubaliano ambayo yameshafikiwa baina ya pande husika. 
Ghasia alisema uzoefu unaonesha kuwa Watanzania, wamezoea
kufanya kazi mtu mmoja mmoja, hivyo basi wakati umefika  kuwa na kampuni moja, itakayokuwa na nguvu katika sekta ya usafirishaji. 
“Imani walioijenga kwa kuungana italeta tija kubwa kiuchumi katika sekta ya usafiri katika  Jiji la Dar es Salaam na wengine nao wataiga,” alisema Ghasia. 
Alisema  kuwa mfumo  mpya, utakaokuwa unatumika katika uendeshaji utakuwa wa kisasa zaidi na kwa mfumo wetu wa kuchukua nauli ndani ya daladala, hautakuwepo tena, hivyo ni lazima kuwa kitu kimoja. 
“Mimi ningefurahi sana kama huu mfumo ungeshikiliwa na Watanzania kuliko wageni,” Waziri Ghasia.
Alisema wakati umefika kwa Watanzania, wabadilike na kuacha kufanya kazi kwa mazoea. 
Ghasia alisema anaamini wawekezaji wa ndani, wana uelewa mzuri na mfumo huu mpya, hasa kutokana na kushirikishwa kutoka mwanzo wa mradi hadi kufikia sasa, kutokana na kujifunza mambo kadha wa kadha nje ya nchi. 
“ Ninashukuru tumekuwa na wamiliki wa usafiri kutoka zoezi hili linaanza, DARCOBOA tumeenda nao mapaka Bogota nchini Colombia na wameona namna mfumo unavyofanya kazi,” aliongeza Ghasia.
Alisema kuungana kwao ni ishara na namna walivyojifunza nchini Colombia, jinsi wenzao walivyohama kutoka mfumo tulionao sisi na kuingia katika mfumo mpya wa mabasi yaendayo haraka. 
“Wawekezaji wetu waliona namna mfumo ulivyo mzuri na rahisi katika jiji lile, hivyo ni somo tosha kwa wamiliki wetu wa hapa nchini, nashukuru wameliona hilo,” alisema.

No comments: