MAJAMBAZI WABAKA MWALIMU, MWINGINE APORWA MILIONI 20/-


Watu wanaosadikiwa kuwa majambazi wamemteka na kumvamia mwalimu mmoja na kumpora kiasi cha zaidi ya Sh milioni 20 na kisha kumbaka mwalimu mwingine wa kike katika kijiji cha Nassa Ginery wilayani Busega mkoani Simiyu. 
Kwa mujibu wa Jeshi la Polisi katika mkoa wa Simiyu, tukio hilo lilitokea usiku wa kuamkia juzi kijijini hapo. 
Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai mkoani Simiyu, Evance Mwijage ndiye aliyethibitisha kuwapo kwa tukio hilo alipozungumza na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu. 
Hata hivyo, hakuwa tayari kuelezea zaidi taarifa juu ya tukio hilo, akisema alikuwa anasubiri jalada la Polisi kutoka wilayani Busega ambalo lina taarifa za kina, ikiwa ni pamoja na watu wanaohusishwa na tukio zima. 
Lakini kwa upande wa mwalimu aliyetekwa na kuporwa fedha, Samwel Mbochi alisema siku ya tukio, watu anaoamini kuwa ni majambazi waliruka ukuta wa nyumba yake na kumvamia na kumshikilia wakimtaka atoe pesa. 
Anasema alitii amri yao na kutoa kiasi hicho cha fedha alichokuwa amekiandaa kwa ajili ya kununua bidhaa kesho yake, kwani pamoja na kuwa mwalimu, pia amekuwa akijishughulisha na biashara ya duka kijijini hapo. 
Anaongeza kuwa, baada ya kuchukua fedha, walivamia chumba kingine cha mwalimu wa kike ambaye ni mpangaji wake na kumbaka kwa zamu, kisha kutokomea kusikojulikana.

No comments: