KIWANDA CHA DANGOTE KUANZA UZALISHAJI SARUJI MWAKANI



Kiwanda cha saruji cha Kampuni ya Dangote, kinachojengwa  mkoani Mtwara kinatarajia kukamilika ujenzi wake na kuanza uzalishaji wa saruji mwishoni mwa mwaka 2015, ambapo mwekezaji wake, raia wa Nigeria,  Aliko Dangote, amesema kiwanda hicho kitakuwa moja ya viwanda bora duniani.
Kwa mujibu wa taarifa ya kampuni hiyo iliyotolewa mapema wiki hii, ujenzi wa kiwanda hicho nchini  ni moja ya  miradi ya uwekezaji wa kampuni za Dangote barani Afrika, unaolenga kuinua uchumi wa nchi hizo na kuboresha maisha ya wananchi wake.
Ripoti hiyo inasema Kampuni ya Dangote, imepanga kuwekeza kwenye miradi mipya ya viwanda vya saruji yenye thamani ya Dola za Marekani bilioni 3.9 na kwamba kwa miradi ya viwanda vya saruji kwa Afrika Mashariki, ikiwemo Tanzania, kampuni hiyo imewekeza mtaji wa Dola za Marekani milioni  600.
Dangote alisema hadi hivi sasa ujenzi wa kiwanda hicho cha saruji nchini, umekamilika kwa asilimia 25, na hadi mwisho wa mwaka ujao, ujenzi huo utakuwa umekamilika na kuanza uzalishaji wa saruji.
Alisema kiwanda hicho, kitakuwa na uwezo wa kuzalisha tani milioni tatu za metriki za saruji kwa mwaka.
Mbali na ujenzi wa kiwanda cha saruji nchini, rais huyo alisema kampuni yake pia imepanga kuwekeza kwenye viwanda vingine vya uzalishaji saruji barani Afrika  kwenye nchi 16.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, kampuni hiyo imejipanga kwa miaka ijayo, kuwekeza  zaidi kwenye nchi mbalimbali na kujenga viwanda bora vya saruji, ambapo kwenye mipango yao watawekeza pia kwenye  nchi za Senegal na Afrika Kusini.
Akizungumzia jinsi ya kukuza uchumi wa Bara la Afrika, Dangote alisema ili kuinua uchumi wa Afrika ni lazima ujenzi wa viwanda vyenye ushindani na mataifa mengine, uwepo ili kuchochea uchumi, hivyo uwekezaji wa saruji utafanywa pia kwenye nchi za Zambia, Ethiopia, Cameroon na Sierra Leone.

No comments: