HATIMA YA KESI YA LUKAZA FEDHA ZA EPA OKTOBA 8



Hatima ya washitakiwa wawili wa kesi ya wizi wa Sh bilioni sita za Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kupitia Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA), itajulikana Oktoba 8 mwaka huu wakati Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu itakapotoa uamuzi kama wana kesi ya kujibu au la.
Endapo Mahakama itawaona  washitakiwa katika kesi hiyo Johnson Lukaza na ndugu yake, Mwesiga Lukaza, wana kesi ya kujibu watapanda kizimbani kuanza kujitetea, kama hawatakuwa na kesi ya kujibu wataachiwa huru.
Washitakiwa hao wanadaiwa kati ya mwaka 2004/2005 walikula njama za kughushi nyaraka mbalimbali na kujipatia Sh bilioni sita kwa udanganyifu wakidai Kampuni ya Changanyikeni Residential Complex Ltd ya Tanzania imepewa mamlaka ya kukusanya madeni ya Kampuni ya Marubeni Corporation ya Japan.
Hakimu Mkazi Edson Mkasimongwa alitoa tarehe hiyo baada ya upande wa jamhuri kufunga ushahidi wao wa mashahidi saba pamoja na vielelezo walivyowasilisha mahakamani.
Awali, shahidi wa mwisho wa Jamhuri, Ofisa wa Polisi kutoka Kenya Tom Olanga alidai kuwa, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Marubeni Corporation ya Kenya, Hisao Ikegai alikana kuifahamu Kampuni ya Changanyikeni Residential Complex.
Alidai kuwa, alimhoji Ikegai na alimuonesha hati ya makubaliano ya kukusanya deni kutoka kampuni hiyo kwenda kampuni ya kina Lukaza, hata hivyo alidai nyaraka hiyo siyo halali kwa kuwa iliandikwa cheo cha Mkurugenzi ambacho hawatumii kwenye kampuni yao.
Aidha, alidai hawamfahamu Mkurugenzi Nakasomi Nsuko ambaye alisaini katika hati hiyo kwa niaba ya kampuni yao na hajawahi kufanyakazi katika kampuni hiyo, pia hawana kumbukumbu yoyote ya kuwa na deni Tanzania wala kutoa mamlaka kwa kampuni yoyote kukusanya madeni yao.
Tom alidai katika maelezo yake, Ikegai alidai  kwa mujibu wa taratibu zao za kuhamisha fedha Kampuni ya Japan, lazima iwape taarifa kwa kuwa wao ndiyo wawakilishi wa Afrika Mashariki na hawawezi kuhamisha fedha bila kupata nguvu ya kisheria kutoka Japan.

No comments: