WAWILI KORTINI KWA KUSAFIRISHA NA KUUZA MENO YA TEMBO



Wafanyabiashara wawili wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashitaka ya kusafirisha na kuuza meno ya tembo yenye thamani ya Sh bilioni 5.4.
Washitakiwa hao Salivius Matembo (39) na Manase Philemon (39) walifikishwa mahakamani hapo jana na kusomewa mashitaka na Wakili wa Serikali, Pius Hilla akisaidiwa na Mwendesha Mashitaka Jackson Chidunda mbele ya Hakimu Mkazi Frank Moshi.
Wakili Hilla alidai kuwa, kati ya Januari 2000 na Mei 22 mwaka huu Dar es Salaam, washitakiwa hao walisafirisha na kuuza nyara za serikali ambazo ni vipande 706 vya meno ya tembo vyenye gramu 1889 na thamani ya Sh bilioni 5.4 bila kuwa na kibali kutoka kwa Mkurugenzi wa Wanyamapori.
Aliendelea kudai kuwa, siku isiyofahamika washitakiwa hao walikula njama za kutenda kosa kwa kukusanya, kusafirisha na kuuza meno hayo jambo ambalo ni kinyume cha sheria.
Katika mashitaka mengine, Hilla alidai Mei 21 mwaka huu katika Hospitali ya Sinza Palestina, Philemon alitoroka akiwa chini ya ulinzi halali wa askari D/koplo Beatus.
Hakimu Moshi alisema washitakiwa hawataruhusiwa kujibu mashitaka yao kwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo na hawajapata kibali cha kuisikiliza.
Wakili Hilla alidai upelelezi unaendelea na kuomba tarehe nyingine ya kutajwa kwa kwesi hiyo.
Hata hivyo upande wa utetezi ulidai kuwa hati hiyo haipo mahakamani kisheria kwa kuwa haijasajiliwa na kuomba washitakiwa wapewe dhamana kwa sababu mashitaka yao yanadhamana kisheria.
Akijibu hoja Wakili Hilla alidai hayo ni mambo ya kiutawala lakini kesi hiyo imesajiliwa kama ya Uhujumu Uchumi namba 21/2014 na kuhusu dhamana alidai kwa mujibu wa Sheria za uhujumu Uchumi, mahakama hiyo hairuhusiwa kutoa dhamana kama mashitaka yamehusisha zaidi ya Sh milioni 10.
Hakimu Moshi alisema hayo yalikuwa mambo ya kiutawala lakini kesi hiyo imesajiliwa na sheria ipo wazi kuwa washitakiwa wanatakiwa kupewa dhamana Mahakama Kuu ambayo ndiyo yenye mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo. Kesi itatajwa tena Juni 17 mwaka huu.

No comments: