FASTJET YAONGEZA SAFARI ZA MBEYA NA MWANZA



Kampuni ya ndege ya Fastjet imetangaza kuongeza safari zake hapa nchini ambapo sasa itaruka kwenda Mbeya mara mbili kwa siku na Mwanza mara tatu.
Meneja wa Uchumi na Biashara wa kampuni hiyo, Jean Uku aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa wamefikia uamuzi huo baada ya kupokea maoni na maombi kutoka kwa wateja wake mbalimbali nchini.
“Kwa niaba ya shirika la ndege la Fastjet natangaza rasmi kuwa kuanzia leo huduma zitaongezeka katika maeneo mbalimbali hapa nchini, na namna hali itakavyoruhusu tutakuwa tukiongeza huduma hizi katika eneo la ndani ya nchi na nchi za jirani,” alisema Uku.
Aidha Uku aliongeza kuwa, Juni 30 mwaka huu, Fastjet itaongeza huduma zake katika Uwanja wa Ndege ya Kilimanjaro (KIA) kwa kufanya safari kila Alhamisi na Jumamosi mara tatu kwa siku na mara mbili kwa wiki.
Alisema sasa wasafiri kutoka na kwenda mikoa ya Mbeya, Mwanza na Kilimanjaro watafurahia huduma hiyo inayotokana na kuongezwa safari za ndege kwenda huko mara mbili.
“Kuongezwa kwa huduma hii katika mikoa iliyotajwa itaweza kuwahudumia hata wasafiri wa nchi jirani kama vile Zambia na Malawi wanaotumia viwanja vya ndege vya Tanzania kuingiza na kutoa bidhaa,” alisema Uku.
Kwa upande wao wafanyabiashara wanaotumia huduma ya safari za anga wamesema kuongezwa na kuimarishwa kwa huduma hiyo kutawasaidia kufanyikisha shughuli zao za kibiashara kwa wakati na nafuu.
Tiketi za Fastjet zimeanza kuuzwa katika vituo mbalimbali na kupitiwa katika mitandao ya internet ambapo tiketi ya moja kwa moja  ni shilingi 32,000 bila ushuru na gharama zinginezo kama mzigo.

No comments: