WATOTO WENYE HOMA YA MANJANO WAANIKWA JUANI



Watoto wanaozaliwa katika Hospitali ya Mkoa wa Dodoma wakiwa na ugonjwa wa homa ya njano, inasadikiwa wamekuwa wakianikwa juani kutokana na ukosefu wa mashine maalumu ya kufanya kazi hiyo. 
Hata hivyo, Mwenyekiti wa Bodi ya Hospitali hiyo ya Rufaa ya Mkoa, Balozi Job Lusinde amesema hali hiyo haitajitokeza tena kutokana na hospitali hiyo kupatiwa msaada wa mashine ya kisasa ya matibabu kwa njia ya mionzi. 
Mashine hiyo ilitolewa na benki ya CRDB wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika, yaliyofanyika mjini hapa. 
 “Watoto walikuwa wakianikwa juani kama pumba ili kuwanusuru madhara ya ugonjwa huo, tunaishukuru sana CRDB kwani mashine hii itasaidia uhai wa watoto wengi,” alisema.
Daktari Bingwa wa uzazi na wanawake Enid Chiwanga alisema wanatumia njia ya kuanika watoto wachanga juani wanapozaliwa na homa ya manjano kutokana na kukosekana kwa mashine.
“Watoto wanapozaliwa  tulikuwa tukitumia njia ya asili kwa kuwaanika juani wakati wa asubuhi ili wapate mwanga wa jua,” alisema.
Alisema msaada huo utaokoa watoto wengi wanaozaliwa na manjano ambayo husababisha nyongo kuenea mwilini na kusababisha mwili kuwa wa njano hali inayosababisha pia matatizo ya ubongo. 
Mkurugenzi wa CRDB Tawi la Dodoma, Rehema Hamisi, alisema kwa kutambua umuhimu wa afya ya mtoto, wameamua kutoa mashine hiyo baada ya kubaini ukosefu wa kifaa hicho hospitalini hapo. 
Kwa mujibu wa Mkurugenzi huyo wa benki, mwaka 2010, CRDB ilikarabati wadi ya akinamama na watoto ya hospitali hiyo pamoja na kutoa vitanda 50, magodoro na mashuka.
Pia mwaka juzi, benki hiyo ilidhamini mashindano ya Kiswahili mkoani Dodoma  kuongeza ari ya vijana kujifunza lugha ya taifa.

No comments: