WASIOONA WAOMBA KUPATIWA MSAADA WA FIMBO NYEUPE



Chama cha Wasioona Tanzania (TLB) Manispaa ya Dodoma wamewaomba wasamaria kuwasaidia kupata fimbo nyeupe  zitakazowatambulisha.
Mratibu wa mradi wa Ulingo wa majadiliano kuhusu uwezeshwaji, ujumuishwaji na utetezi wa mahitaji na haki za wenye ulemavu wa macho Mathias Fyejeje  amesema ukosefu wa fimbo hizo unawaweka rehani walemavu hao.
Mratibu huyo alisema hayo katika mkutano wa ulingo uliofanyika Miyuji, Dodoma.
Fyejeje alisema tatizo hilo la ukosefu wa fimbo nyeupe kwa wasioona ni tatizo hasa wanapokuwa karibu na barabara kwani madereva hawawezi kutambua kwamba alio mbele yao ni mtu asiyeona.
Alisema kazi kubwa ya fimbo hizo nyeupe ni kumtambulisha asiyeona anapokuwa barabarani kwa madereva na watembea kwa miguu kwani anakuwa hawezi kukwepa hatari yoyote bali huyo anayeona anapaswa kufanya hivyo kutokana na kuiona fimbo hiyo.Mratibu huyo alisema wanahitaji fimbo 150 kutokana na idadi ya wasioona waliopo katika chama hicho cha wilaya ambazo kila moja inauzwa kati ya 30,000 na 35,000 na hivi sasa wamekwishapokea fimbo 40 toka kwa wahisani mbalimbali na hivyo kusaliwa na 110.
Aidha aliongeza kuwa miundombinu kwa wasioona ni tatizo hasa kwa majengo na barabara ambapo ameshauri ngazi zote za majengo ziwe na vizuizi vya pembeni, mifereji Êna madaraja yawekewe tahadhari ya watu wenye ulemavu huo.
Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Mnadani Manispaa ya Dodoma Stiven Masangia aliyefungua ulingo huo wa majadiliano aliwataka wahisani mbalimbali kuwanunulia fimbo hizo na Serikali kuwajengea miundombinu rafiki ili kuepusha ajali zisizo za lazima kwa wasioona.

No comments: