MAJAMBAZI WAUA, WAPORA SHILINGI MILIONI 20 ARUSHA



Watu wawili wanaosadikiwa kuwa ni majambazi wakiwa na silaha aina ya shortgun wamepora kiasi cha Sh milioni 20 kutoka kwa mtumishi wa duka la kubadilishia fedha za kigeni la Northern Bureua de Change na kumpiga risasi mtu mmoja na kufa hapo hapo.
Tukio hilo lililotokea saa 3.30 asubuhi jana katika duka hilo mali ya Hotel ya Impala lililopo mtaa wa Maeda katikati ya Jiji la Arusha. Watuhumiwa hao wakiwa na pikipiki waliondoka eneo hilo kupitia barabara ya zamani ya Moshi kuelekea Kijenge mara baada ya tukio hilo.
Kwa mujibu wa watu walioshuhudia tukio hilo, walisema majambazi hao walifika eneo hilo pikipiki na kuegesha eneo zinapoegeshwa teksi na kumsubiri mtumishi wa duka hilo aliyetambuliwa kwa jina moja la mama Msuya ambaye jana aliingia kazini na usafiri mwingine tofauti na unaojulikana.
Mmoja wa watu hao ambaye hakuwa tayari kusema jina lake, aliendelea kusema mara baada mtumishi huyo kufika akiwa na mfuko mweusi wenye kiasi hicho cha fedha, ghafla alivamiwa mlangoni wakati akiwa anafungua duka hilo na kuanza kunyang'anyana mfuko huo.
Alisema wakati jambazi huyo mmoja akipambana na mama Msuya na kumpiga kibao huku akimuamurisha kutoa fuko hilo la fedha, mama huyo alipiga kelele kuomba msaada na madereza teksi walikwenda ghafla kutaka kumsaidia.
Lakini hali ilibadilika baada ya jambazi mwingine aliyebaki katika pikipiki kutelemka na silaha na kwenda kumpiga risasi mmoja wa watu aliyetaka kwenda kutoa msaada aliyetambuliwa kwa jina mmoja la Mmasi ambaye ni mchimba madini ya tanzanite na kufa hapo hapo.
Mtoa habari huyo alisema marehemu alikuwa ametoka kusali katika kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) usharika wa mjini kati na alikwenda kununua magazeti eneo hilo hilo  na alipoona mama akipiga kelele kuomba msaada, alikwenda kwa lengo kumukoa lakini kabla ya kufika alipigwa risasi  ubavuni na kufa hapo hapo na jambazi aliyekuwa pembeni na toyo.

No comments: