Mfuko wa Pensheni LAPF umesema kuanzia
sasa misaada ya kijamii itakayotolewa na
mfuko huo utakuwa ni kati ya Sh 500,000 na Sh milioni tatu.
Uamuzi huo unatokana na mfuko huo
kupokea maombi mengi, wakati bajeti yake ya misaada kwa jamii ni Sh milioni
130.
"Kutokana na ufinyu wa bajeti na
maombi kuwa mengi sehemu kubwa ya misaada inayotolewa ni kati ya Sh 500,000
hadi Sh milioni tatu," haya yamo kwenye taarifa ya mfuko iliyotolewa kwa
vyombo vya habari.
LAPF
imesisitiza kwamba kusaidia jamii ni utaratibu wake wa kawaida na ni
sehemu ya vigezo vya utawala bora. Mfuko huo umefafanua kuwa misaada hiyo
hutolewa moja kwa moja kwa walengwa na si kwa kutoa fedha taslimu, bali kwa
kununua vifaa husika.
Taarifa hiyo pamoja na masuala mengine,
ililenga pia kukanusha kukopesha baadhi ya wabunge kama ambavyo taarifa
zilivyotolewa na baadhi ya vyombo vya habari hivi karibuni.
Katika taarifa yake kwa vyombo vya
habari, mfuko huo umesema pamoja na kuandikisha wanachama, kukusanya michango,
uwekezaji na kulipa mafao, mfuko huo unashiriki pia katika kusaidia jamii na
hivyo kusaidia katika kupunguza umasikini na kuchochea maendeleo.
"Utaratibu huu ni wa kawaida kwa
taasisi zote za hifadhi ya jamii pamoja na taasisi nyingine za umma na taasisi
za binafsi hapa nchini. Utoaji wa misaada ya kijamii ni sehemu ya vigezo vya
utawala bora," ilisema taarifa ya LAPF.
Ilielezwa kuwa LAPF imekuwa ikitoa
misaada ya kijamii katika sekta mbalimbali kama vile afya, elimu, vituo vya
kulelea watoto yatima, taasisi za watu wenye mahitaji maalumu, sekta ya michezo
na kusaidia katika matukio ya maafa.
Katika sekta ya afya, matukio ya maafa
na vituo vya kulelea watoto yatima, LAPF imesema imekuwa ikitoa msaada wa
chakula na vifaa mbalimbali kama vyandarua, magodoro, shuka, dawa na vifaa vya
maabara.
Kwa upande wa sekta ya elimu mfuko
umekuwa ukichangia madawati, mabati, saruji, taa zinazotumia nguvu ya jua na
mashine za kudurufu nyaraka. Aidha katika michezo, unachangia vifaa mbalimbali
vile kama vile mipira na jezi.
No comments:
Post a Comment